Posted: 08 Mar 2012 10:51 PM PST
Na Charles Mwakipesile, Mbarali
MKUU wa Mkoa wa Mbeya Bw. Abbas Kandoro, amewataka watumishi wenye tabia ya kuwasema wenzao ofisini 'majungu', kuacha mara moja ambapo watakaobainika kuwa na tabia hiyo, watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Bw. Kandoro aliyasema hayo juzi katika hafla ya kumuaga aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri Wilaya ya Mbaarali, mkoani hapa Bw. George Kagomba.

Hafla hiyo ilifanuyika katika Makao Makuu ya halmashauri hiyo baada ya kustaafu utumishi wa umma na kuongeza kuwa, siri ya mafanikio kwa mtendaji yeyote wa Serikali ni kuchapa kazi kwa bidii, kuepuka majungu.

Alisema kitendo cha kuwagawa wafanyakazi kinakwamisha maendeleo ya wannchi na utekelezaji wa shughuli za Serikali.

“Kiongozi ambaye leo tunamuaga, amefanya kazi kwa bidii na kufanikiwa kuleta mabadiliko makubwa, kufyeka kichaka porini na kujenga Makao Makuu ya Halmashauri.

“Bw. Kagomba ni kielelezo cha watendaji bora wa serikali wasio na majungu  ambaye amewaunganisha wafanyakazi kuwa kitu kimoja na kuharakisha maendeleo,” alisema.


Alisema watendaji wa Serikali ambao wanaendeleza majungu badala ya kufanya kazi, huambulia kufukuzwa na kutokumbukwa kwa lolote walilofanya wakati wa utumishi wao serikalini.

“Sipendi kusikia Mkoa wetu unakosa maendeleo kwa sababu watumishi hutumia muda mwingi kuzungumza habari za majungu badala ya kufanya kazi kwa bidii,” alisema.

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Bw. Keneth Ndingo, alisema Bw. Kagomba atakumbukwa kwa mambo mengi pamoja na kujenga Makuu Makuu ya halmashauri hiyo ambayo ina majengo ya kisasa yaliyozinduliwa na Rais Jakaya Kikwete.

Mbali ya kufanikisha ujenzi wa majengo hayo pia ameweza kukuza pato la halmashauri na ujenzi wa majengo ya sekondari za kata hivyo aliiomba Serikali iangalie uwezekano wa kumuongezea muda wa utumishi kwa mkataba maalumu.

Kwa upande wake, Bw. Kagomba alisema bila kupata ushirikiano kutoka kwa watumishi wengine, asingeweza kufanikisha majukumu aliyopewa ambayo yamezaa matunda.
Posted: 08 Mar 2012 10:45 PM PST
Na Zahoro Mlanzi
SERIKALI imesema mpaka kufikia mwishoni mwa Aprili mwaka huu Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam utakuwa tayari umekamilika kwa asilimia 75 na utaanza kutumika kwa shughuli mbalimbali rasmi Juni, mwaka huu.

Uwanja huo awali ulitakiwa kukamilika kabla ya sherehe za miaka 50 ya Uhuru lakini mpaka kufikia Desemba 9, mwaka jana ulikuwa haujakamilika, hivyo sherehe hizo kulazimika kufanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Serikali ulisimamisha shughuli za uwanja huo, tangu kuanza kwa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara msimu wa 2010/2011.

Akijibu swali kuhusu uwanja huo utakamilika lini, baada ya kushindwa kukamilika kabla ya kuanza kwa sherehe za Uhuru wa miaka 50 Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Leonard Thadeo alisema ni kweli ulitakiwa kukamilika kabla ya sherehe za Uhuru, lakini kikubwa kilichokwamisha ni mkandarasi alichelewesha baadhi ya mambo muhimu.

“Hivi sasa ujenzi unaendelea kama kawaida na ninakuhakikishia mpaka kufikia mwishoni mwa Aprili, mwaka huu utakuwa umekamilika kwa asilimia 75, kwani kazi kubwa iliyobaki ni kuweka viti katika jukwaa mbalimbali zilizojengwa,” alisema Thadeo.

Alisema wakati maboresho hayo yakiendelea kwa kuhakikisha viti vinawekwa na mambo mengine, mpaka kufikia Juni mwaka huu ana imani kila kitu kitakuwa kimekamilika na shughuli mbalimbali zilizokuwa zikifanyika katika uwanja zitaendelea kama kawaida.

Thadeo alisema kukamilika kwa uwanja huo kutapunguza matumizi ya Uwanja wa Taifa, kwani mechi zitakazokuwa si za lazima kuchezewa kwenye uwanja huo, zitafanyika Uwanja wa Uhuru kama ilivyokuwa hapo awali.

Pia alitoa wito kwa mashabiki na wanamichezo kwa ujumla kuhakikisha kuutumia vizuri uwanja huo, pindi utakapokamilika ili kuepusha madhara yatakayoweza kujitokeza kama ilivyokuwa katika mechi ya Kombe la Shirikisho kati ya Simba na Kiyovu ya Rwanda.

Katika mechi hiyo ya Simba, viti 152 viliharibiwa na 11 vilivunjwa kutokana na mashabiki hao kuvunja na kurushiana wakati mechi hiyo ikiwa mapumziko.

You are subscribed to email updates from MAJIRA - GAZETI HURU LA KILA SIKU:
To stop receiving these emails, you may unsubscribe now.
Email delivery powered by Google
Google Inc., 20 West Kinzie, Chicago IL USA 60610