Rais Dkt.Jakaya Kikwete na mkewe Mama Salma Kikwete wakifariji familia 
ya Marehemu Dkt. Sengodo Mvungi nyumbani kwao Kibamba Dar es Salaam 
jana.
- SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZAZIDI KUMIMINIKA
 
- MWILI WAKE KUWASILI KESHO,KUAGWA JUMAMOSI 
 
 Na Waandishi Wetu 
 
  Rais
 Jakaya Kikwete, amesema ameshtushwa na kufadhaishwa na taarifa za kifo 
cha Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Dkt. Sengondo Mvungi, 
kilichotokea juzi kwenye Hospitali ya Milpark, Johannesburg, Afrika 
Kusini. 
 
Katika
 salamu za rambirambi ambazo amemtumia Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji 
Joseph Warioba, Rais Kikwete alisema amepokea kwa mshtuko mkubwa na 
taarifa za kifo cha Dkt. Mvungi. 
 
"Kwa
 hakika ni taarifa iliyonisumbua na kunipa huzuni kubwa," alisema Dkt. 
Kikwete. Rais Kikwete alisema hakuna shaka kuwa katika maisha yake Dkt. 
Mvungi alitoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Tanzania kwa namna 
mbalimbali na kuwa kifo kimemfika wakati Taifa la Tanzania lilikuwa bado
 linahitaji busara, hekima na mchango wake katika mchakato mzima wa 
kusaka Katiba mpya. 
 
"Kuanzia
 alipokuwa mwandishi wa habari katika Magazeti ya Chama Cha Mapinduzi 
(CCM) ya Uhuru na Mzalendo, hadi uhadhiri wake katika Chuo Kikuu cha Dar
 es Salaam, hadi uwakili katika Kampuni ya South Law Chambers, hadi 
uongozi wake katika Chama cha NCCR-Mageuzi, hadi uamuzi wake wa kugombea
 Urais wa Tanzania mwaka 2005 na sasa akiwa Mjumbe wa Tume ya Katiba, 
Dkt. Mvungi ametoa mchango wake mkubwa sana katika maendeleo ya nchi 
yetu. Na hili sitalisahau," alisema Rais Kikwete na kuongeza; 
 
"Kwa
 masikitiko makubwa, nakutumia wewe Jaji Joseph Warioba, Mwenyekiti wa 
Tume ya Mabadiliko ya Katiba salamu za rambirambi za dhati ya moyo wangu
 nikiomboleza kifo cha Dkt. Mvungi. 
 
“Nakupa
 pole nyingi wewe Mwenyekiti, wajumbe wa Tume na wafanyakazi wote wa 
Tume kwa kuondokewa na mwenzenu. Naungana nanyi kuombleza msiba huo 
mkubwa. 
 
“Kupitia
 kwako, natuma pole nyingi kwa wana-familia, ndugu, marafiki na majirani
 wa Dkt. Mvungi kwa kuondokewa na mhimili, msimamizi wa familia na 
ndugu. 
 
“Wajulishe
 kuwa niko nao katika msiba huu mkubwa. Wajulishe kuwa msiba wao ni 
msiba wangu pia. Muhimu waelewe kuwa binafsi naelewa machungu yao katika
 kipindi hiki kigumu na namwomba Mwenyezi Mungu awape subira waweze 
kuvuka kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake. 
 
Mbatia anena 
 
Wakati
 huo huo, mwili wa Dkt. Mvungi unatarajia kuwasili nchini kesho na 
utapokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius 
Nyerere na kisha kupelekwa nyumbani kwake Kibamba Msakuzi. 
 
Akizungumza
 na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa 
NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema baada ya mwili huo kuwasili 
itafanyika misa takatifu katika Kanisa la Mt. Joseph saa nne asubuhi 
Jumamosi. 
 
Alisema
 baada ya misa hiyo saa sita mchana mwili wake utapelekwa viwanja vya 
Karimjee kwa ajili ya kuagwa na kisha kusafirisha kwenda Mwanga, mkoani 
Kilimanjaro kwa ajili ya maziko. 
 
Alisema katika kipindi hiki cha msiba bendera za chama hicho zitapepea nusu mlingoti kwa muda wa wiki moja. 
 
Waziri Chikawe 
 
Naye
 Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, alisema msiba huo ni pigo 
kwa taifa kwani marehemu alikuwa ni kiungo muhimu na alitumia ujuzi, 
elimu na nafasi aliyonayo kwa jamii hasa katika kipindi hiki muhimu cha 
mchakato wa katiba mpya. 
 
Alisema
 ni wananchi waelewe kuwa ikitokea kuyumba au kuwepo kwa pengo lolote 
katika mchakato huo basi litakuwa limechangiwa na kutokuwepo kwake Dkt. 
Mvungi. 
 
Jaji Warioba amlilia 
 
Kwa
 upande wake Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph 
Warioba, alisema Dkt. Mvungi ni mtu muhimu ambaye alikuwa na mchango 
mkubwa kwenye Tume yake. 
 
Alisema alitumia utaalam wake wa sheria na uzoefu katika kuhakikisha hoja zake alizokuwa akizitoa anazisimamia ipasavyo. 
 
CUF yatuma rambirambi 
 
Kwa upande wake Chama cha Wananchi (CUF), kimesema kimepokea kwa mshituko na majonzi makubwa taarifa ya kifo 
 
 cha Dkt. Mvungi. 
 
"Kifo cha Dkt.Mvungi kimeishtua Tanzania nzima hasa kwa vile tulitazamia kuwa angeishi kwa muda mrefu zaidi. 
 
Kifo
 hicho kinazidi kusikitisha kwa vile kimetokana na kushambuliwa kikatili
 na watu wasiojulikana wanaodaiwa kuwa ni majambazi," ilieleza taarifa 
ya CUF. 
 
Mwenyekiti
 wa Taifa wa Chama cha Wananchi CUF, mimi mwenyewe na viongozi 
waandamizi wa CUF walimjua vizuri sana Marehemu Dkt. Mvungi kwani 
tulifanya kazi naye kwa karibu," alieleza taarifa ya CUF iliyotolewa na 
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad. 
 
Maalim
 Seif, alisema Dkt. Mvungi alikuwa mpambanaji jasiri asiyeyumba katika 
mapambano ya kuiletea Tanzania mfumo wa kidemokrasia halisi unaolenga 
kulinda haki za kila Mtanzania bila ya ubaguzi wa aina yoyote ile. 
 
Alisema Dkt. Mvungi alichukia uonevu, manyanyaso, ukandamizaji na dhuluma dhidi ya binadamu yoyote. 
 
"Tulishirikiana
 naye kwa karibu katika mchakato wa kudai Katiba mpya ya Tanzania na 
pale vyama vya siasa vilipounda kamati ya kufanya rasimu ya Katiba mpya 
Marehemu Dkt. Mvungi ndiye aliyekuwa Mwanasheria wa Kamati hiyo. 
 
Alitoa mchango mkubwa katika kuandaa na kukamilisha rasimu hiyo," alisema Maalim Seif na kuongeza; 
 
"Wengi tulifarijika pale alipoteuliwa kuwa miongoni mwa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya Tanzania. 
 
Tulijua
 uwezo wake, umahiri wake, utendaji kazi makini wake na dhamira yake ya 
kuona Tanzania inapata Katiba nzuri kwa masilahi ya wananchi wote bila 
kujali itikadi za vyama." 
 
Alisema Dkt. Mvungi alikuwa ni wakili mahiri, msomi makini na kiongozi shupavu. 
 
Alisema
 alikuwa jasiri hasa katika kuwatetea wanyonge na katika kutoa mawazo 
yake. Alikuwa ni mchambuzi hodari wa mambo ya kisheria, hasa sheria 
inayoambatana na masuala ya Katiba. 
 
Hali
 kadhalika alikuwa mchambuzi aliyebobea katika masuala ya kijamii na ya 
kisiasa na aliguswa sana na umuhimu wa kuendeleza elimu bora nchini 
Tanzania. 
 
Maalim
 Seif alisema kifo chake ni pigo zito kwa familia yake, Chama cha 
NCCR-Mageuzi, Chuo Kikuu cha Bagamoyo, Tume ya Mabadiliko ya Katiba na 
kwa jamii nzima ya Watanzania. 
 
"Kwa
 niaba ya Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, Wajumbe wa Baraza Kuu la 
Uongozi la CUF na Wanachama wote wa CUF na kwa niaba yangu mwenyewe, 
tunatoa mkono wa tanzia kwa familia ya Marehemu, Mwenyekiti wa Taifa wa 
NCCR-Mageuzi, Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na wafiwa wote," 
alisema. 
 
CCM yatoa pole 
 
Umoja
 wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesikitishwa na kifo cha Dkt.
 Mvungi na umeonya kuwa umaskini usifanye Watanzania kuwa chanzo cha 
kuua watu wengine. 
 
Akizungumza
 Dar es Salaam jana Mkuu wa Idara ya Hamasa na Chipukizi wa UVCCM Taifa,
 Paul Makonda, alisema wamepokea kwa masikitiko taarifa ya msiba huo. 
 
"Umaskini
 wetu wa kipato, akili na mawazo, usiwe sababu ya kuumizana na kugharimu
 maisha ya mtu kwani hata wale waliomvamia na kumjeruhi huenda 
wamesukumwa na tamaa zao za kimaisha," alisema. 
 
Polisi yanasa mwingine 
 
Jeshi
 la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia mtu mmoja 
anayetuhuniwa kuhusika katika tukio la mauaji ya marehemu Dkt.Sengondo 
Mvungi. 
 
Akizungumza
 na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Kamishna wa Polisi 
Kanda, Maalum Suleiman Kova alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa juzi 
katika maeneo ya Twiga Jangwani. 
 
Kamishina
 Kova alisema kuwa; "mtuhumiwa alitambuliwa na kukamatwa kisha kuhojiwa 
na Polisi na alikubali kuhusika katika tukio hilo na askari waliongozana
 naye hadi nyumbani kwake Kiwalani Migombani ambapo alikutwa na silaha 
ambayo ni bastola aina ya REVOLVER No.BDN 6111 pamoja na risasi 21 za 
bastola hiyo ikiwa ni mali ya Dkt.Mvungi,"alisema Kova. 
 
Pia
 katika upekuzi uliofanywa na Jeshi la Polisi katika chumba cha 
mtuhumiwa vilipatikana baadhi ya vifaa vya mlipuko vya aina tofauti 
vikiwemo,baruti aina ya Explgel, Tambi mbili ambazo ni viwashio vya 
baruti pamoja na mlipuko. 
 
Aliongeza
 kuwa mtuhumiwa alipohojiwa kuhusu umiliki wa silaha hiyo alikiri kuwa 
hana kibali cha kumiliki silaha. Alisema silaha hiyo ni miongoni mwa 
vitu vilivyoibwa kwa Dkt. Mvungi.
 

 
No comments:
Post a Comment