TAN

TAN

Bayport

Bayport

Kikoa

Kikoa

Myway entertainment

Myway entertainment

FORE PLAN CLINIC

FORE PLAN CLINIC

MPINGA CUP 2016

MPINGA CUP 2016

Mashujaa Fm 89.3, Lindi

Friday, January 24, 2014

UCHAGUZI WA UDIWANI SOMBETINI ARUSHA MOTO MOTO

UCHAGUZI mdogo wa udiwani Kata ya Sombetini umeanza kwa vurugu baada ya wanachama watatu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kujeruhiwa na kundi la vijana walinzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Green Guard.
Aidha, mgombea wa CCM kwenye kata hiyo, David Lesikari, akiwa na watu wengine  anadaiwa kuwashambulia na kitu chenye ncha kali wanachama wawili wa CHADEMA na kumjeruhi mwingine kichwani na mgongoni.
Mwenyekiti wa CHADEMA wilayani Arusha, Ephata Nanyaro, aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa vurugu hizo zilitokea Januari 20 mwaka huu na kwamba licha ya wanachama wao kuumizwa, Jeshi la Polisi liliwakamata na kuwageuzia kesi kuwa wao ndio waliofanya vurugu.
Alisema siku hiyo saa nane mchana mwanachama wao, Vitalis Bernad, alipigwa shoka la kichwa na kijana aliyedai kuwa kiongozi wa CCM wakati akipita kwenye kona ya Mbauda akiwa kwenye pikipiki yenye bendera ya CHADEMA wakielekea kwenye mkutano wa mgombea wa chama chao, Ally Bananga.
“Kwa bahati Bernard alikuwa amevaa kofia ngumu za waendesha pikipiki hivyo hakuumia sana lakini watu waliokuwa pale walijaribu kumkimbiza mhusika lakini hawakufanikiwa, kwani alikimbilia kwenye ofisi ya CCM ambapo walitokea kundi la watu wenye mapanga kutoka ndani ya ofisi hizo jambo lililowafanya wananchi kutawanyika kwa hofu,” alisema Nanyaro.
Alisema Bernard akiwa na viongozi wa CHADEMA walienda polisi kufungua taarifa namba Ar/RB/982/2014 kwenye kituo kidogo cha Mbauda karibu na ofisi hizo za CCM ambapo waliwaeleza polisi kuwa mtuhumiwa yuko ndani ya ofisi hizo lakini hawakutaka kwenda kumkamata.
Mwenyekiti huyo wa wilaya alisema siku hiyo hiyo saa 12 jioni Wanachadema wawili, Loserian Laisi na Mozec Joseph wakitokea kwenye mkutano wa kampeni wakiwa wamepakizana kwenye pikipiki walivamiwa na kundi la watu wakiongozwa na mgombea wa CCM ambapo waliwashambulia kwa mapanga na silaha za jadi.
Nanyaro alisema katika tukio hilo Loserian alikatwa kichwani na kiunoni kwa kitu chenye ncha kisha kutelekezwa migombani kabla ya kusaidiwa na wasamaria wema waliompeleka Kituo cha Polisi cha Sombetini kupata fomu ya matibabu (PF3) na kwenda hospitali.
“Polisi bila weledi walichukua maelezo kwa saa mbili huku Loserian akiwa kwenye maumivu na damu zikimtoka hata hivyo alipatiwa matibabu katika hospitali ya Kaloleni, akiwa anaendelea na matibabu polisi walifika hospitalini na kumchukua hadi Kituo Kikuu cha Polisi na kumweka rumande,” alilalamika Mwenyekiti huyo wa CHADEMA.
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alikiri ofisi yake kupokea taarifa za vurugu za jioni huku akibainisha kwamba taarifa za tukio la mchana hakuzipata.
Akizungumza na Tanzania Daima, Kamanda Sabas alisema kwenye tukio hilo la jioni vijana wa CHADEMA wakiwa kwenye pikipiki mmoja alishuka na kumpiga vibao mgombea wa CCM, Lesikari, ambapo wananchi walioona walipandwa na hasira hivyo kuwashambulia na kukiri kwamba vijana wa CHADEMA kuhojiwa na polisi kuhusu tukio hilo.
“Unaweza kupigwa karibu ya kituo cha polisi haimaanishi waliokupiga ni polisi, hivyo huyo inawezekana kabisa alipigwa hapo kona ya Mbauda karibu na ofisi za CCM lakini wahusika si Wana CCM, kwenye kesi kinachotafutwa ni ushahidi si hisia,” alisema kamanda huyo.

No comments:

Post a Comment