“Waziri
 hana mamlaka ya kumwondoa mkurugenzi wa halmashauri, taasisi, shirika 
na katibu wa wizara yake kutokana na kubanwa na mfumo.” Makamba. 
…………………………………………………………………………….
Mwanza. Naibu
 Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba amesema 
ipo haja ya kubadili mfumo wa watendaji serikalini ili wanapoboronga nao
 wajibishwe na mawaziri.
Akizungumza katika mahojiano 
yaliyofanyika mwishoni mwa wiki mjini hapa, Makamba alisema mfumo uliopo
 sasa, hauwapi nguvu mawaziri  ili kuwawajibisha watendaji pale 
wanapokosea na badala yake unawabana wenyewe hivyo kuendelea kuwa 
kitanzi kwao.
“Mimi ni waziri, akikosea katibu
 nawajibishwa huyu anabaki, mimi siwezi kumwajibisha hivyo wanafanya 
lolote na sisi tunalazimishwa kuwajibishwa kisiasa kwa makosa ya 
watendaji,” alisema.
“Baada ya Kamati ya Maliasili 
Ardhi na Mazingira iliyo chini ya Mwenyekiti wake, James Lembeli kuomba 
kwa Spika kutumia ushahidi kwa kuweka kanda za video ili kuonyesha 
kilichotokea kwenye Operesheni Tokomeza Ujangili, hali ilichafuka ndani 
ya kikao cha Bunge na kila mmoja akawa na hisia na wengine kuanza 
kububujikwa na machozi na wabunge kuchangia hoja za kutaka mawaziri 
kuachia ngazi, hawakuangalia kiini cha tatizo, waliwabana mawaziri tu,” 
alisema.
Alisema
 Serikali kupitia mamlaka za juu, inapaswa kuangalia mfumo uliopo kwa 
lengo la kuubadilisha na kuingiza mapendekezo na mfumo mpya kwenye 
Katiba Mpya kuhusu uwajibikaji wa mawaziri na watendaji wakuu kwenye 
wizara, taasisi, idara, halmashauri na mashirika ya umma ambao ni 
wataalamu mbalimbali kuwajibishwa na mawaziri husika endapo kutaonekana 
utendaji wao haukidhi ama kwenda kinyume na maadili na sheria zilizopo.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment