Wananchi
 wa Afrika ya Kusini wakishuhudia mwili wa rais Mstaafu Hayati Mzee 
Nelson Mandela ulipokuwa ukitoka Ikulu. Picha na mpigapicha wetu 
……………………………………………………………………………..
Pretoria. Maelfu
 ya wananchi wa Afrika Kusini wameshindwa kutoa heshima za mwisho kwa 
mwili wa Rais wa Kwanza mzalendo wa nchi hiyo, Nelson Mandela kutokana 
na muda uliopangwa kumalizika.
Kuanzia Jumatano wiki hii hadi 
jana, mwili wa Mandela aliyefariki dunia Desemba 4 mwaka huu, ulikuwa 
ukiwekwa katika Ikulu ya Pretoria, iliyopo ndani ya Majengo ya Umoja 
(Union Buildings), kila asubuhi kwa ajili ya wananchi kutoa heshima za 
mwisho.
Jana ilikuwa siku ya mwisho ya 
utoaji wa heshima hizo na hadi muda uliowekwa ulipokwisha saa 11:30 
jioni, kulikuwa na maelfu ya watu waliokosa fursa ya kumuaga mpendwa wao
 huyo.
Dalili za idadi kubwa ya watu 
kukosa nafasi hiyo adhimu zilianza kuonekana Jumatano na baadaye juzi 
Alhamisi kwani hadi muda wa kufunga ulipofika jioni, maelfu ya watu 
walirejea nyumbani bila kupata fursa ya kuaga.
Jana mchana, Serikali ilitoa 
taarifa kwamba kwa kuzingatia idadi ya watu waliojitokeza kutoa heshima 
zao za mwisho, ilikuwa vigumu kwa watu wote kufikiwa.
“Hatuwezi kuahidi kwamba kila 
mtu ambaye amejipanga hivi sasa kwenye mstari atapata nafasi ya kufika 
katika Majengo ya Umoja, tunawaomba wananchi wasiende tena huko,” 
ilisema taarifa iliyotolewa na Idara ya Habari na Mawasiliano ya 
Serikali (GICS) jana na kuongeza:
“Tunawashukuru sana wananchi kwa
 kujitokeza, lakini sasa tunawaomba wale ambao hawakuweza kupata fursa 
ya kutoa heshima zao za mwisho, wafanye hivyo kwa kutumia njia zao 
wenyewe.”
Waziri katika Ofisi ya Rais, 
Collins Chabane, alisema kuwa hakuna jinsi ya kuwasaidia watu 
watakaokosa fursa ya kuaga na kwamba Serikali pamoja na familia 
wamejitahidi kiasi cha kutosha.
Serikali ilisitisha utaratibu wa
 usafiri kwa watu waliokuwa wakienda kuaga kuanza saa 8:00 mchana hali 
iliyozua mvutano baina ya maelfu ya waombolezaji na vyombo vya usalama.
Wengine waliokuwa wameishapanda 
kwenye mabasi na kufika Ikulu waliambiwa kwamba hawataweza kufikiwa hali
 iliyozidisha manung’uniko.
Ulinzi ni mkali na Rais Jacob 
Zuma jana aliliarifu Bunge kwamba amewaajiri kwa siku 15 Askari 11,894 
kutoka Jeshi la Afrika Kusini (SANDF), ili wasaidiane na polisi katika 
ulinzi na usalama wakati wa maombolezo na mazishi ya Mandela.
Wakesha viwanjani
Maelfu
 ya wananchi walikuwa katika makutano ya barabara za kuelekea Ikulu 
kuanzia saa 10 alfajiri na wengine walisema walilala jirani na eneo hilo
 ili waweze kupata fursa ya kumuaga Mandela.
Miongoni mwa waliotoa heshima za
 mwisho ni ujumbe kutoka Venezuela, ambao ulimzawadia Mandela upanga wa 
dhahabu na kumkabidhi mjukuu wake wa kwanza, Mandla.
Mandla kwa siku tatu mfululizo 
amekuwa akiketi pembeni mwa jeneza la babu yake, wakati waombolezaji 
wakiaga na wakati wote ameonekana mwenye mawazo mengi na huzuni kubwa.
Ndani ya kibanda ambamo mwili wa
 Mandela uliwekwa kulikuwa na ukimya, ambao mara kadhaa ulivunjwa na 
kelele za vilio na majonzi kutoka kwa watu walioshindwa kujizuia.
Polisi na wasaidizi mara kadhaa 
walikuwa wakiwasaidia wale waliozidiwa au wale walioanguka baada ya 
kuona sura ya marehemu Mandela.
Mapema asubuhi, wengi 
walijipanga pembezoni mwa barabara kutoka Hospitali ya Jeshi hadi Ikulu,
 wakiimba nyimbo za kumsifu Mandela na wakati msafara uliokuwa 
ukisindikiza mwili wake ulipokuwa ukipita, wengine walisikika wakisema; 
“Siyabinga Tata Madiba…” (wakimaanisha ahsante Baba Madiba).
Wengine walionekana wakiwa 
wamekwea juu ya miti ili kuweza kuuona vizuri msafara huo wa magari 
zaidi ya 40, huku baadhi ya watu waliokuwa kazini wakionekana kutoka na 
kupungia msafara huo.
Wakati
 huo helikopta za SANDF na polisi zilikuwa zikizunguka katika anga la 
Jiji la Tswane ndani ya Pretoria na wakati mwili wa Mandela ulipoingizwa
 Ikulu zilizunguka eneo hilo kwa zaidi ya nusu saa kabla ya kuondoka.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment