Abiria
 37 waliokuwa wamesafaria ndege ya Shirika la Precision Air, akiwamo 
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, jana walinusurika kifo, baada ya 
magurudumu manne ya ndege hiyo kupasuka ilipokuwa ikitua katika Uwanja 
wa Ndege wa Arusha. 
………………………………………………………………………..
Arusha. Abiria
 37 waliokuwa wamesafaria ndege ya Shirika la Precision Air, akiwamo 
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, jana walinusurika kifo, baada ya 
magurudumu manne ya ndege hiyo kupasuka ilipokuwa ikitua katika Uwanja 
wa Ndege wa Arusha.
Tukio hilo la aina yake, 
lilitokea saa 6:15 mchana, wakati ndege hiyo, ikitua kutoka jijini Dar 
es Saalam, ikiwa na abiria hao 37, marubani wawili na wahudumu wawili.
Kamanda wa polisi mkoani Arusha, Liberatus Sabas alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kueleza hakuna majeruhi aliyeripotiwa.
“Hadi sasa hali ni shwari, ndege
 iliweza kusimama licha ya kupasuka magurudumu. Kiutaratibu uchunguzi 
umeanza kufanywa na wataalamu husika,”alisema Kamanda Sabas.
Ofisa Mwendeshaji wa Mamlaka ya 
Viwanja vya Ndege nchini (TCAA), wa Uwanja wa Ndege Arusha, Roland 
Mwalyambi, alisema kuwa katika tukio hilo, hakuna abiria aliyejeruhiwa 
licha ya kupata mshtuko mkubwa.
“Uchunguzi wa ajali hii umeanza, lakini hakuna majeruhi, abiria wote walifanikiwa kushuka salama,”alisema Mwalyambi.
Alisema ndege hiyo, kama ingetua
 salama ilitarajiwa kusafiri kurejea Dar es Salaam kupitia Zanzibar, 
lakini abiria waliotarajia kusafiria ndege hiyo, walipelekwa Uwanja wa 
Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro ili kuendelea na safari.
Katika ndege hiyo, pia kulikuwa 
na maofisa mbalimbali wa Serikali na Jeshi la Wananchi, ambao leo 
wanatarajia kuhudhuria sherehe ya kutolewa kamisheni kwa maofisa wa 
jeshi katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli(TMA), ambapo Rais 
Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Tukio hilo la ndege kupata ajali
 katika uwanja huo ni la pili kutokea mwaka huu, kwani mapema mwaka huu,
 mfanyabiashara maarufu wa Mkoa wa Kilimanjaro na Arusha, Babu Sambeki 
alipata ajali pia katika uwanja huo, wakati akijiandaa kutua na ndege 
yake.
Mfanyabiashara huyo, alifariki 
papo hapo baada ya moja ya mabawa ya ndege kunasa katika matawi ya mti 
jirani na uwanja huo. Hata hivyo, taarifa ya ajali hiyo hadi sasa 
haijawekwa hadharani.
Kukosekana
 kwa taa katika uwanja huo, ambao umekuwa ukitumiwa na ndege nyingi 
ndogo hasa za watalii, imekuwa ni kero kubwa na mara kadhaa safari 
zimeahirishwa kutokana na tatizo hilo.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment