Posted: 02 Dec 2013 10:09 PM PST
- CHADEMA KIGOMA YASHTUKIA MCHEZO MCHAFU
 
- HOFU YA KUTOKEA VURUGU YATANDA MAJIMBONI
 
Na Mwajabu Kigaza, Kigoma
Chama
 cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), mkoani Kigoma, kimesitisha ziara
 ya Katibu Mkuu wa chama hicho Taifa, Dkt. Wilbrod Slaa, ambayo 
ilipangwa kufanyika mkoani humo kuanzia Desemba 5 hadi 13 mwaka huu, 
kutokana na hofu ya usalama miongoni mwa wanachama wake. 
Mwenyekiti
 wa chama hicho mkoani humo, Jafari Kasisiko, aliyasema hayo jana wakati
 akizungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa, usalama katika 
baadhi ya majimbo mkoani humo ni mdogo sana. 
Alisema
 kutokana na hali hiyo, wameona ni bora ziara hiyo isitishwe kwanza ili 
kuepusha machafuko yaliyoandaliwa na wanachama dhidi ya Dkt. Slaa kama 
atafika mkoani humo. 
“Uamuzi
 wa kusitisha ziara hii umefikiwa katika Kikao cha Baraza la Uongozi 
mkoani hapa kilichofanyika Desemba Mosi, mwaka huu na kushirikisha 
viongozi wa majimbo mengine. 
“Majimbo
 haya ni Kigoma Mjini, Kaskazini na Kusini ambao kwa pamoja walielezea 
uwepo wa njama za kuhujumu ziara hii ili kumdhalilisha Dkt. Slaa,” 
alisema. 
Aliyataja
 majimbo yaliyodaiwa kuchafuka kisiasa kutokana na maamuzi ya Kamati Kuu
 ya CHADEMA kumvua nyadhifa za uongozi aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa 
chama hicho Bara, Bw. Zitto Kabwe kuwa ni Kigoma Mjini, Kaskazini na 
Kusini, wakati ambapo majimbo ya Buhigwe, Kasulu, Muhambwe na Buyungu 
pia hali ya usalama imedaiwa kuwa ya mashaka. 
Akizungumzia
 msimamo wa chama hicho mkoani humo kuhusu uamuzi wa Kamati Kuu kumvua 
uongozi Bw. Kabwe kwa madai ya kutaka kukisaliti chama, alisema kikao 
hicho kilikuwa halali. 
“Hatua
 zote za kumvua uongozi Bw. Kabwe na wenzake Dkt. Kitila Mkumbo na Bw. 
Samson Mwigamba, zilifuatwa sasa kama anadhani ameonewa, ana haki ya 
kukata rufaa Baraza Kuu. 
“Ziara
 ya Dkt. Slaa hapa Kigoma, haina uhusiano na maamuzi ya Kamati Kuu kwani
 ilipangwa muda mrefu na kusitishwa kutokana na vikao vya Kamati Kuu, 
lengo la ziara hii ni maandalizi ya uchaguzi ujao ngazi za chini,” 
alisema. 
Aliwataka
 baadhi ya wanachama wanaoendesha vitendo vya vurugu na kuhujumu 
miundombinu ya chama kuacha kufanya hivyo kwani ni kinyume cha maelekezo
 ya chama kwani palipo na vurugu hakuna haki. 
Baadhi
 ya wanachama wa chama hicho kutoka majimbo yaliyotajwa kuwa na vurugu, 
walikutana Mjini Kigoma katika moja ya kumbi za mikutano kupinga ujio wa
 Dkt. Slaa, Desemba 5 mwaka huu. 
Akisoma
 tamko la wanachama hao, Fanuel Sindika alisema wameikataa ziara hiyo 
kwa sababu CHADEMA kimekuwa kikiwaonea baadhi ya viongozi hasa kutoka 
mikoa ya Magharibi na wapo tayari kufanya vurugu ili kumdhalilisha 
kiongozi huyo. 
Alisema hawakubaliani na maamuzi yaliyotolewa na Kamati Kuu dhidi ya Bw. Kabwe ambayo hayajazingatia haki kwa mujibu wa katiba. 
Aliongeza
 kuwa, kwa muda mrefu chama hicho kimekuwa na mgogoro unaotokana na hofu
 ya madaraka katika nafasi ya Mwenyekiti wa chama ambayo inadaiwa 
kuwaniwa na Bw. Kabwe akisaidiwa na rafiki zake kwenye kampeni ili 
kuhakikisha anashinda kiti hicho. 
Hivi
 karibuni, baadhi ya vijana kutoka Tawi la Mwandiga, Jimbo la Kigoma 
Kaskazini, walifanya maandamano ya pikipiki na kuburuza bendera 
barabarani, kuchoma kadi, bendera na kuvunja bango la Tawi la Msingi 
katika kijiji hicho
 
No comments:
Post a Comment