Rais
 Kikwete akiendesha kikao cha baraza la Mawaziri siku za hivi karibuni. 
Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM chini ya Mwenyekiti wake Rais 
Jakaya Kikwete, imeanza kuwahoji mawaziri waliotajwa ni ‘mzigo’ kwa 
Serikali. Picha na Maktaba.
………………………………………………………………
Dodoma. Kamati
 Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM chini ya Mwenyekiti wake Rais Jakaya 
Kikwete, imeanza kuwahoji mawaziri waliotajwa ni ‘mzigo’ kwa Serikali.
Katibu
 wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, jana alilithibitishia gazeti 
dada la Mwananchi, The Citizen juu ya kuanza kwa kikao cha Kamati Kuu 
(CC), lakini hakuwa tayari kuingia kwa undani kuhusu ajenda.
Hata 
hivyo, habari za ndani zilieleza kwamba miongoni mwa ajenda kuu za CC ni
 kuwahoji mawaziri wanaolalamikiwa na wananchi, kwamba wameshindwa 
kutekeleza majukumu yao.
Wakiwa
 Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Nape aliwatupia lawama mawaziri 
wakati akielezea changamoto zinazowakabili wakulima ambao ni asilimia 80
 ya Watanzania, huku mawaziri husika wakikaa kimya.
Mawaziri
 waliotajwa mzigo ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru 
Kawambwa; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza na 
Naibu wake, Adam Malima, kwamba wameshindwa kazi na alipendekeza 
wang’olewe.
Hata 
hivyo, gazeti hili jana lilishuhudia mawaziri kadhaa wakifika na kuingia
 kwenye mkutano wa CC, taarifa zingine zilisema mawaziri waliofika 
kwenye kikao hicho walihojiwa na wajumbe wa CC.
Kuhojiwa na CC
Mawaziri
 waliohojiwa na CC hadi kufikia saa 8:00 mchana jana walitajwa kuwa ni 
Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na Waziri wa Kilimo, Chakula na 
Ushirika, Christopher Chiza. Mkuya ndiye ambaye kwa sasa anaisimamia 
Wizara Fedha kutokana na Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa kulazwa 
nchini Afrika Kusini akisumbuliwa na maradhi ambayo hayajatajwa.
Waandishi
 wa gazeti hili jana waliwashuhudia takriban mawaziri 10 wakiingia 
katika ofisi za makao makuu ya CCM, Dodoma, maarufu White House, huku 
baadhi wakiwa si wajumbe wa CC.
Habari
 zilizotufikia jioni ziliwataja wengine kuwa ni Dk David Mathayo David 
(Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi), Hawa Ghasia (Waziri wa Nchi, 
Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa-Tamisemi), Dk
 Kawambwa, Celina Kombani (Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya 
Utumishi wa Umma).
Dk 
Kawambwa wakati akitoka kwenye kikao cha CC aliulizwa na waandishi wa 
habari kilichotokea na yeye alijibu kwa kifupi; “Mawaziri mizigo ndiyo 
tunatoka.”
Mawaziri
 ambao si wajumbe wa CC ni Mkuya, Chiza, Dk Kawambwa, Hawa Ghasia na 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulikia Utawala Bora, George 
Mkuchika ambaye naye taarifa zilidai alihojiwa.
Tayari
 Bunge limepitisha azimio la kumtaka Ghasia pamoja na naibu mawaziri 
wake wawili, Aggrey Mwanry na Majaliwa Kassim Majaliwa, kupima na 
kutafakari kama bado wanatosha kusimamia wizara hiyo.
Kiini
 cha Bunge kupitisha azimio hilo ni taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu
 za Serikali kubainisha kuwapo wizi, ubadhirifu na mtandao wa ufisadi 
ndani ya Tamisemi, Halmashauri na Hazina.
Waziri
 Mkuu, Mizengo Pinda ambaye baadhi ya wabunge wamemtaja kama waziri 
mzigo namba moja, amesema yuko tayari kuachia ngazi kama Rais ataamua 
kumwondoa katika wadhifa huo.
Pinda
 alitoa kauli hiyo juzi bungeni mjini Dodoma wakati akijibu swali la 
papo kwa hapo kutoka kwa Mbunge wa Viti Maalumu, Rukia Ahmed (Cuf) 
aliyetaka aeleze anajisikiaje kuitwa mzigo namba moja.
Akijibu
 swali hilo, Pinda alisema yeye anasimamia wizara 20, hivyo kama wapo 
watakaomhukumu kwa sababu ya wizara moja ama mbili kutofanya vizuri basi
 watu hao watakuwa hawamtendei haki.
Alisema
 kama Rais atamwona ameshindwa kuwajibika yuko tayari kuachia ngazi na 
endapo Rais hatafanya hivyo na wabunge bado wakaona ipo haja hiyo, 
wampigie kura ya kutokuwa na imani naye.
Kauli ya CCM
Katibu
 wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, mbele ya Katibu Mkuu wa chama
 hicho, Abdulrahman Kinana, alisema kuwa mawaziri hao wameshindwa 
kutimiza wajibu wao wa kuwatumikia Watanzania.
Alisema
 kuwa Waziri Chiza na Malima wamebaki wakifunga tai na kuvaa suti mjini 
wakati wakulima wa Ruvuma na mikoa mingine ya Tanzania wakiteseka.
Nape 
alisema Waziri Kawambwa naye anatakiwa kuchukuliwa hatua kwa kuingia 
mkataba na kampuni ya ujenzi ya Progressive iliyopewa zabuni ya 
kutengeneza barabara ya Namtumbo hadi Tunduru wakati mkandarasi huyo 
hana uwezo wa kuijenga na matokeo yake amefukuzwa kazi.
Dk 
Kawambwa ametupiwa lawama hizo kutokana na kuipa kazi kampuni hiyo 
wakati akiwa Waziri wa Miundombinu pamoja na kushindwa kusimamia elimu.
“Katibu
 Mkuu (Kinana), nilimuuliza Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Chiza na Malima 
wamefika lini kusikiliza matatizo ya wakulima wa tumbaku, korosho na 
mahindi, alinijibu hakumbuki kama wamefika mkoani hapa. Nikafuatilia na 
kubaini si yeye tu hata Waziri aliyetangulia Profesa Jumanne Maghembe 
naye hakuwahi kufika. Najiuliza sababu nini, hakuna majibu,” alisema 
Nape.
Alisema
 anasikitishwa na kitendo cha mawaziri hao waliopewa dhamana kushindwa 
kutambua wajibu wao na kwamba umefika wakati wa kuhojiwa na Kamati Kuu 
(CC) ya CCM, ili wachukuliwe hatua kwani bila kufanya hivyo aibu itarudi
 kwa chama chake.
Wabunge wajitosa
Kikao
 hicho cha CC kinafanyika huku kikiwa na taarifa kwamba wabunge wa chama
 hicho tawala wameanza kukusanya saini za wabunge, ili kushinikiza 
kuitishwa kwa kikao cha wabunge hao au Party Cocas.
Uchunguzi
 wa gazeti hili, uliofanywa kwa siku kadhaa mjini hapa, umebaini kuwa 
wabunge wa CCM zaidi ya 160 wametia saini katika fomu hiyo wakiwamo 
mawaziri zaidi ya 10.
Chanzo
 kimoja cha kuaminika kilisema kuwa fomu hiyo iliwasilishwa katika ofisi
 ya katibu wa wabunge wa CCM, ikiambatana na barua inayotaka kuitishwa 
kwa kikao kitakachowakutanisha.
“Tuliwaomba
 waitishe kikao cha wabunge wa CCM ili mawaziri ambao tunawaona 
hawatimizi majukumu yao kikamilifu waweze kuhojiwa lakini wakawa 
wanasuasua,”kilisema chanzo hicho.
“Lakini
 mmoja wetu akasema kwa kuwa wamepiga chenga ya kukiitisha basi kuna 
nafasi ya kikanuni ya kukusanya saini za wabunge zaidi ya nusu 
kushinikiza kuitishwa kwa kikao,”alisema mbunge huyo.
Taarifa ya ziada na Habel Chidawali
Mbunge
 mwingine wa CCM alisema katika kikao hicho wabunge walitaka 
kukutanishwa kwa pamoja kati yao, mawaziri wanaoonekana kuwa mzigo na 
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
“Kikao
 hicho tulitaka kiwe Desemba 12 mwaka huu ili tuanze kuwahoji mawaziri 
kabla ya CC lakini Mwenyekiti (Mizengo Pinda), amekuwa akipiga danadana 
hadi leo (jana) inapokutana”alisema.
Habari
 zaidi zilisema baadhi ya wabunge wa CCM walikutana faragha na Kinana 
juzi jioni na kumtahadharisha kama mawaziri hao wasipowajibishwa, CCM 
kitakuwa na wakati mgumu.
Vuguvugu
 linaloendelea hivi sasa ndani ya wabunge wa CCM, liliwahi kujitokeza 
Bunge la Aprili mwaka jana na kumlazimisha Rais Kikwete kupangua Baraza 
lake Mawaziri Mei 4,2012.
Kung’olewa
 kwa mawaziri sita waliokuwa wakishinikizwa na wabunge wajiuzulu 
kulitokana na taarifa za kamati za kudumu za bunge na za Mdhibiti na 
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Katika
 baraza lake hilo jipya, Rais aliwatosa mawaziri waliokuwa 
wakishinikizwa kujiuzulu akiwemo Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo na 
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Cyril Chami.
Wengine
 waliotoswa kwa shinikizo hilo lililoungwa mkono na kambi ya upinzani ni
 wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, wa Nishati na Madini, William 
Ngeleja na wa Uchukuzi, Omar Nundu.
Pia 
Naibu Waziri wa Uchukuzi wa wakati huo, Dk Athuman Mfutakamba naye 
alitoswa sambamba na Waziri wa Afya, Dk Haji Hussein Mponda na Naibu 
wake, Dk Lucy Nkya.

No comments:
Post a Comment