TAN

TAN

Bayport

Bayport

Kikoa

Kikoa

Myway entertainment

Myway entertainment

FORE PLAN CLINIC

FORE PLAN CLINIC

MPINGA CUP 2016

MPINGA CUP 2016

Mashujaa Fm 89.3, Lindi

Monday, March 17, 2014

Mchungaji atuhumiwa kuchochea uhalifu Muleba

Muleba. Watu watatu akiwamo Mchungaji wa Kanisa la Chochea Moto, Elmes Fabian, wanashikiliwa na polisi mkoani Kagera kwa tuhuma za kufanya uhalifu, kufyeka mashamba ya migomba na kuvunja nyumba tatu za wakazi wa Kijiji cha Kishulo wilayani Muleba wakiwatuhumu kwa uchawi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, George Mayunga alithibitisha kuwapo kwa tukio hilo na kudai kuwa mchungaji wa kanisa hilo, wakiwamo watu watatu wanashikiliwa kwa kosa la kuchochea vurugu, kuidhuru miili na kuharibu mali kinyume cha sheria.
Kamanda Mayunga aliwataja walionusurika kuuawa kuwa ni Fabian Albert na mkewe Gaudensia Fabian, Methodia Leonard na Georgina Kayonga wote wakazi wa Kijiji cha Kashulo wilayani humo mkoani Kagera.
Alisema uchunguzi wa jeshi hilo umebaini baadhi ya wananchi wakiwamo watoto wa watuhumiwa wa ushirikina walifanya ukatili huo wakishirikiana na baadhi ya wananchi waliokuwa na lengo la kuwaua wazee wa familia hizo.
Tukio hilo limesababisha wananchi zaidi ya 12 wakiwamo watoto na wanafunzi wa shule za msingi kukosa makazi, huku wazazi wao wakilazimika kukimbilia kwenye Taasisi ya Kusaidia Wazee na Yatima ya “Kwa Wazee” iliyopo Kata ya Nshamba wilayani Muleba ili kupata hifadhi ya muda.
Aidha, alisema mchungaji wa kanisa hilo anadaiwa kuwahubiri waumini wake kuwa ana uwezo mkubwa wa kuwabaini wachawi ambao wamekuwa wakisumbua kijijini humo kabla ya kuanza kuwataja kwa majina.
Hatua hiyo, ilionekana kupokewa kwa hisia kali na waumini wake wakiwamo watoto wa watuhumiwa, hivyo kuungana na wananchi wengine kwenda kuharibu mali na kuwadhuru wazee hao kwa mapanga.
Kwa upande wake, Mratibu wa “Kwa Wazee”, Lydiah Lugazia alisema kutokana na ukatili huo kwa wazee hao wamelazimika kuwachukua na kuwahifadhi kwa muda, ili kunusuru maisha yao kutokana na wananchi kutaka kuwaua kwa imani potofu za kishirikina.
Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Lambris Kipuyo akiongea na gazeti hili alitoa onyo kwa wananchi wote wenye tabia ya kujichukulia sheria mkononi na kwamba wanapaswa kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama iwapo kuna mtu mwenye tuhuma mbaya katika jamii husika.
Alisema vitendo vya kujichukulia sheria mkononi ni kuvunja sheria za nchi na kuondoa uhai wa mtu ni kuvunja sheria za mungu, hivyo wazingatie maadili ya kiimani na kufuata sheria.

No comments:

Post a Comment