Katika maisha ya kila siku, mwananchi anapaswa kutambua wajibu wake katika jamii ikiwa ni pamoja na kutii Sheria bila shuruti.
Katika maisha ya sasa nchini 
kumekuwa na vitendo vya ukiukwaji wa Sheria katika jamii na jamii 
imekuwa ikihusika katika matendo makubwa ya kijinai ambayo ni kinyume na
 sheria.
Hali hii imekuwa ikitokana na aidha jamii kutojua sheria, na muda mwingine ni kupuuzia tu maagizo na sheria mbalimbali.
Siku za hivi karibuni kumekuwepo
 na ukatili mkubwa ukitendeka katika jamii kwa kutokea kwa mauaji ya 
watu wenye ulemavu wa ngozi ambapo wasiojua nini maana ya utu kwa 
makusudi wanakatiza uhai wa maisha ya binadamu wenzao na wengine 
kuwakata baadhi ya viungo vyao kwa tamaa ya kujipatia fedha pamoja na 
imani za kishirikina.
Jamii sio tu inaelewa kuwa 
kumdhuru mtu ni kosa la jinai bali pia jamii inatambua kuwa kuua pia ni 
kosa kubwa la jinai ambapo katika Sheria ya Kanuni ya adhabu Sura ya 16 
kifungu cha 197 kimeeleza jinsi ambavyo kosa la kuua kwa kukusudia 
linamgharimu mtu adhabu ya kifo, lakini licha kuwepo kwa sheria hiyo, 
bado jamii inajihusisha na makosa ya kuua kila kukicha.
Katika mikoa ya Kanda ya Ziwa 
Victoria, suala la mauaji ya watu wenye Ualbino limekuwa ni tatizo kubwa
 kwani mauaji haya yanafanyika katika mazingira tu ya watu kuwa na imani
 potofu za kuukwaa utajiri wa haraka haraka.
Wakili wa kujitegemea Bwana 
Edwin Webiro anaeleza kuwa watu wengi wanafahamu kuwa kuua ni kosa kubwa
 lenye adhabu ya kifo ama kifungo cha maisha, bado watu hao hawajali juu
 ya uwepo wa Sheria ya kunyonga kwasababu wamekuwa wakiiona haitekelezwi
 ipasavyo, jambo linalowafanya wao waone ni haki kwao kufanya unyama 
wowote kwa watu wasio na hatia (watu wenye ulemavu).
Katika hali nyingine jamii pia 
imekuwa ikikiuka Sheria na kusababisha madhara makubwa pale ambapo ajari
 nyingi zimekuwa zikitokea mfululizo hivi karibuni na kusababisha vifo 
na kuacha ulemavu wa kudumu wa jamii.
Ajali hizi zimekuwa 
zikisababishwa na uzembe wa baadhi ya madereva wa mabasi pamoja na 
magari madogo kwani kumekuwa na ukiukwaji wa Sheria za barabarani ambapo
 kwa makusudi madereva hao wamekuwa wakikiuka sheria mbalimbali na 
kufanya mambo yanayosabisha ajari.
Sheria ya Usalama barabarani 
Sura ya 168 Kifungu cha 44 Inazuia mtu kuendesha chombo cha moto akiwa 
ametumia kilevi, lakini Sheria hii inajulikana vema kwa madereva lakini 
kwa makusudi hawaijali wala kuizingatia na badala yake wamekuwa 
wakitumia kilevi kabla ama wakati wakiwa wanaendesha vyombo vya moto.
Swali la kujiuliza ni kwamba, kwanini madereva wamekuwa wakitumia kilevi wakiwa wanaendesha magari?
Josephat Munishi ni Dereva wa 
daladala moja linalofanya safari zake Jijini Dar es Salaam anaeleza kuwa
 kutumia kilevi wakati wa kuendesha gari ni kosa kisheria.
“Muda mwingine kilevi kinakupa 
nguvu na kujihisi kutochoka na unapata hamasa ya kuendesha gari, kama 
unavyojua kazi yetu ni ngumu kutwa nzima unasumbuana na abiria, sasa 
bila kinywaji kidogo hauwezi pata nguvu ya kufanya kazi’’, alisema 
Munishi.
Jamii kwa mara nyingeine imekuwa
 ikikiuka Sheria na kujikuta katika maovu makubwa ambapo baadhi ya 
wasichana wamekuwa wakijihusisha na utoaji mimba (Abortion)kinyume na Sheria.
Kwa hali ilivyo sasa wasichana 
wadogo hasa wanafunzi na hata watu wazima wamekuwa wakijihusisha sana na
 utoaji mimba kinyume na sheria huku wengi wao wamekuwa ni wale ambao 
wamepata mimba hizo katika mazingira ambayo hawakutegema.
Watoto wengi wa kike wamekuwa 
wakijihusisha na mapenzi wakati bado wakiwa shule, na pindi 
wanapojigundua kuwa wana ujauzito njia pekee ambayo wanahisi ni bora 
kuepukana na matatizo hayo wamekuwa wakitoa mimba, kitu ambacho ni 
kinyume na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika kifungu cha 219 Cha 
Sheria ya Kanuni ya adhabu Sura ya 16, kinaeleza wazi kuwa kitendo cha 
kuharibu ujauzito ambao unapelekea kukatisha maisha ya mtoto ambaye 
angezaliwa, ni kosa la jinai lakini sababu kubwa ambayo wamekuwa 
wakiitoa wanawake wengi ni kuwa mimba hizo zinakuwa ni zile ambazo 
hazikupangwa kutokea (unplanned pregnancy).
Jamii inapaswa kuzingatia Sheria
 mbalimbali na iepuke kutoa sababu na visingizio za kutojua sheria hizo,
 kwani ni vema kutii sheria bila shuruti kama vyombo vyetu vya Usalama 
vinavyotutaka.
No comments:
Post a Comment