WAZIRI
 wa Nishati na Madini, Mhe. Profesa Sospeter Muhongo jana ametia saini 
Mkataba wa Mradi kujenga Miundombinu ya kuuziana umeme kati ya Zambia, 
Tanzania na Kenya (ZTK) katika Mkutano  wa Kumi wa kujadili mradi huo.
Katika utiaji saini Mkataba huo,
 Profesa Muhongo alisema kuwa mchakato wa kuandaa Mkataba wa mradi huo 
ulikwishafanyika tangu mwaka 2001 ambapo ulikuwa na vipengele ambavyo 
kwasasa Mawaziri wa Nishati toka nchi zote tatu wameupitia na umefanyiwa
 marekebisho. 
Profesa Muhonga alisema kuwa 
katika marekebisho hayo wamebadili kipengele kilichokuwa kinaeleza juu 
ya uwepo wa Ofisi moja itakayosimamia mradi huo katika nchi zote tatu, 
na badala yake wamekubaliana kuwa kila nchi ijisimamie yenyewe badala ya
 kuwa na Ofisi moja pekee itakayosimamia mradi huo.
“Kwa upande wa Tanzania ujenzi 
wa mradi huu umeshaanza kazi na mpaka hivi sasa asilimia 90 ya vifaa vya
 ujenzi wa mradi vimeshawasili katika eneo la ujenzi,”alisema Profesa 
Muhongo.
Akizungumzia maeneo ambayo mradi
 huo utapita kwa upande wa Tanzania, Profesa Muhongo alisema kuwa, mradi
 huo utapita maeneo ya mikoa ya Singida- Arusha-Namanga, na 
Namanga-Isinya kwa Kenya, kwa upande wa Zambia utapita Mbeya–Iringa na 
Iringa-Singida-Shinyanga. Ambapo unatarajia kusambaza umeme wa kuanzia 
400kV.
Naye Katibu Mkuu wa Nishati 
nchini Kenya, Mhandisi Joseph Njoroge  alisema kuwa muungano huo wan chi
 tatu utasaidia kupunguza tatizo la umeme katika nchi zote na Afrika kwa
 ujumla kwani utapunguza gharama ya umeme pamoja na kuongeza ukuaji wa 
uchumi katika uzalishaji.
Aidha aliongeza kuwa Serikali 
yake itahakikisha kuwa Mkataba huo ndani ya siku Thelathini zijazo kabla
 ya mkutano ujao kuanza, Mwanasheria Mkuu wa Kenya atakuwa umekwisha 
usaini.
Kwa upande wake Waziri wa 
Nishati na Madini nchini Zambia, Mh. Christopher Yaruma alisema kuwa 
nchi yake imeshasaini Mkataba wa kuonyesha dhamira ya kuuziana umeme na 
nchi ya Malawi, Namibia na Botswana.
Utiaji saini wa Mkataba huo 
ulihusisha wadau mbalimbali wa maendeleo na wafadhili ikiwemo JICA, 
COMESA, EU, Korea, Benki ya Dunia, AFD, Ufaransa na Mabalozi wa nchi 
mbalimbali, ambapo wadau hao wameonyesha nia ya dhati katika kuendelea 
kuisaidia Serikali hususani katika sekta ya Nishati.
Sambamba na hilo, mkutano wa 
mwendelezo wa mradi huo badaa ya kuwa umesainiwa na viongozi wa Sheria 
katika nchi husika unatarajiwa tena kufanyika mwanzoni mwa mwezi wa Kumi
 na moja nchini Lusaka, Zambia.
No comments:
Post a Comment