Kipimo Abdallah
IDADI ya watu walioathirika na 
ulaji wa chakula na unywaji wa togwa katika Kijiji cha Litapwasi  Kata 
Mpitimbi Wilaya ya Songea Vijijini Mkoa wa Ruvuma imefikia 325.
Kati ya hao hadi tunakwenda 
mitamboni jana jioni watu 100 bado walikuwa wamelazwa ambapo 29 walikuwa
 katika hospitali ya Peramiho na wengine 71 walikuwa wamelazwa katika 
kituo maalum katika shule ya Msingi ya Kiwalawala.
Akizungumza na mwandishi wa 
gazeti hili kwa njia ya simu jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, 
Kamishna Msaidizi wa Polisi Mihayo Msikhela alisema hadi kufikia jana 
watu 225 waliokumbwa na kadhia hiyo walikuwa wameruhusiwa kutoka kwenye 
vituo vya matibabu.
Kamanda Msikhela alisema tukio 
hilo lilitokea katika sherehe ya kipaimara juzi jumapili kijijini 
Litapwasi na  limeacha majozi kwa watu wengi pamoja na ukweli kuwa hamna
 mtu aliyepoteza maisha hadi sasa.
Msikhela alisema wataalamu wa 
afya wanaendelea kuwapatia matibabu waathirika hao ili kuhakikisha kuwa 
wanapata nafuu wote na kurejea majumbani mwao.
Kamanda huyo alisema
 hadi sasa wamewashikilia watu watano ambao wanasadikiwa kuhusika na 
tukio hilo ambapo mmoja wapo ni baba wa mtoto aliyekuwa anafanyiwa 
sherehe, Enes Nungu ambaye pia ni mwathirika.
Msikhela alisema vyakula na 
vimiminika vingine ambavyo vilivyohusika vitafikishwa Dar es Salaam kwa 
Mkemia Mkuu wa Serikali kwa uchunguzi zaidi ambapo majibu yake yatakuwa 
na mwanga wa kuwaongoza kwenye uchunguzi wao.
Katika tukio jingine, Kamanda 
huyo alisema mwanachi mmoja aliyejulikana kwa jina la Nicolaus Pokela 
amekutwa amekufa nje ya nyumba ya mdogo wake Gidion Pokela baada ya 
kunywa sumu ambayo hutumika kuuwa wadudu wanaharibu kahawa.
Kamishna Msaidizi alisema 
taarifa za awali zinaonyesha kuwa marehemu alikuwa anatuhumiwa kuchoma 
nyumba ya mkewe ambaye walikuwa na ugomvi.
Pia Kamishna Msaidizi alisema 
jana majira ya saa tatu usiku vijana wawili waliuwawa na wananchi baada 
ya kuiba pikipiki na kukimbia nayo ambapo mmoja wao alinusurika na 
kukimbia kusikojulikana
Msikhela alitoa wito kwa 
wananchi kuacha tabia ya kuchukua sheria mkononi kwani kufanya hivyo ni 
uvunjifu wa sheria za nchi na kuwataka watoe taarifa Polisi pindi 
wakiwakamata watuhumiwa.

No comments:
Post a Comment