Mtaalamu
 wa viwango kutoka mgodi wa Ngaka, Boscow Mabena akionyesha tofali 
maalumu (briquette) zilizobuniwa na mgodi huo kwa ajili ya matumizi ya 
kupikia majumbani na katika taasisi. Tofali hizo zina uwezo wa kuwaka 
kwa zaidi ya saa nne.
………………………………………………………………
Na Mohamed Saif – Mbinga
Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Ngaka 
uliopo wilayani Mbinga mkoani Ruvuma upo mbioni kuanza kuuza makaa 
yanayozalishwa na mgodi huo kwa ajili ya matumizi ya kupikia katika 
taasisi na majumbani.
Hayo yalielezwa hivi karibuni na 
Mtaalamu wa Viwango katika mgodi huo, Boscow Mabena alipokuwa 
akizungumza na ujumbe kutoka Wizara ya Nishati na Madini uliofanya ziara
 mgodini hapo kwa lengo la kufanya ukaguzi wa kimazingira.
Mabena alieleza kuwa utafiti wa 
kupunguza joto katika Makaa hayo ili kuweza kutumika kwa ajili ya 
kupikia umefanywa kwa kushirikiana na kikundi cha kina Mama cha 
Mbarawala Women Group kilichopo wilayani humo pamoja na Chuo cha VETA- 
Ruvuma.  
Aliongeza kuwa utafiti huo 
umefanyika kwa kipindi kirefu na tayari umekamilika na hivi sasa 
kinachosubiriwa ni kibali kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ili 
makaa hayo yaanze kuuzwa.
Mtaalamu huyo alieleza kuwa 
wamebuni tofali maalumu (briquette) kutokana na makaa hayo ambazo 
zitatumika kwa ajili ya matumizi ya kupikia kwa kutumia majiko maalumu 
ambayo yamebuniwa na wataalamu kutoka Chuo cha VETA.
Aidha, alibainisha kuwa tofali 
moja la mkaa huo (briquette) lina uwezo wa kuwaka kwa saa zisizopungua 
nne na hivyo kumuwezesha mtumiaji kupika vyakula mbalimbali kwa kutumia 
tofali kimoja.
Kuhusu suala la bei, Mabena 
alifafanua kuwa kila tofali litauzwa kwa kuanzia shilingi mia mbili na 
majiko yatatofautiana bei kulingana na mahitaji ya mtumiaji. “Unajua 
kuhusu jiko, inategemea mtu anahitaji jiko la namna gani, kuna majiko 
makubwa ya taasisi na pia madogo, hivyo mteja atatuambia anahitaji jiko 
la namna gani maana tuna uwezo wa kumjengea jiko maalumu 
lisilohamishika,” alisema.
Mabena alisema matumizi ya mkaa 
huo yanatazamiwa kupunguza uharibifu wa mazingira hususan ukataji hovyo 
wa miti kwa ajili ya mkaa na kuni.
Alieleza kuwa, tayari taasisi 
mbalimbali zimeonyesha nia ya kutumia majiko hayo. Mtaalamu huyo 
alizitaja baadhi ya taasisi kuwa ni Magereza wilayani Songea pamoja na 
Chuo cha Ualimu cha Songea. “Tulikuwepo siku ya Maonesho ya Nane Nane 
hapo Songea na wananchi wengi walivutiwa na mkaa huu na hii ilitusaidia 
tushike nafasi ya kwanza kwa ubunifu,” aliongeza.
No comments:
Post a Comment