Waziri
 wa Ajira na Kazi, Gaudensia Kabaka (kushoto), akitembelea moja ya 
miradi mikubwa ya ujenzi wa shule inayotekelezwa na mgodi wa North Mara 
unaomilikiwa na kampuni ya African Barrick Gold (ABG) wakati wa ziara 
yake kwenye mgodi huo uliopo wilaya ya Tarime mkoa wa Mara hivi 
karibuni. Kushoto kwa waziri ni Mkurugenzi wa ABG wa Mahusiano na 
Serikali, Bw. Emmanuel ole Naiko.
…………………………………………………………
MWANDISHI WETU
Tarime
 SERIKALI imewataka wafanyakazi wa
 sekta ya madini kuwa watulivu wakati inafanyia kazi malalamiko yao 
kuhusu fao la kujitoa katika mifuko ya hifadhi ya jamii, ambapo amesema 
inaandaa utaratibu maalumu utakaowawezesha wanachama wa mfuko husika 
kunufaika nao wakiwa kazini ama baada ya kumaliza utumishi wao.
 Serikali imewasisitizia wafanyakazi nchini kuwa suala hilo limepewa kipaumbele ili kupatiwa ufumbuzi haraka iwezekanavyo.
 Ari hiyo ilitolewa hivi karibuni 
na Waziri wa Ajira na Kazi, Gaudensia Kabaka, wakati akizungumza na 
wafanyakazi wa mgodi wa dhahabu wa North Mara unaomilikiwa na kampuni ya
 African Barrick Gold (ABG) wakati wa ziara yake kwenye mgodi huo uliopo
 wilaya ya Tarime, mkoa wa Mara.
 Waziri huyo aliwasihi wafanyakazi
 wenye mawazo ya kuacha kazi ili tu wachukue mafao yao ya kujitoa 
kuachana na fikra hizo potofu ambazo alisema zitaleta athari kwa familia
 zao.
 Bi.Kabaka amesema serikali 
imesikia kilio cha wafanyakazi we sekta ya madini na wengine na kwamba 
kwa pamoja na Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya 
Jamii (SSRA), wako katika jitihada za kuangalia jinsi ambavyo wanachama 
walioandikishwa kwenye pensheni kama wanaweza kuanzishiwa utaratibu wa 
kuweka na kukopa yaani “supplementary scheme.”
 ”Serikali haijafikia uamuzi 
wakati wowote wa kufanya kuhusiana na mtu ama watu wanaotaka kujitoa  
katika fao hilo ndio maana niko hapa,” alisema.
 Alitangaza kuwa serikali 
itakutana na SSRA na watu wa sekta ya madini jijini Dar es Salaam tarehe
 7 Januari, kwa ajili ya kupata mawazo yao juu ya suala la mafao ambapo 
wafanyakazi wa Migodini watawakilishwa na wawakilishi  wao amabo ni 
chama cha wafanyakazi.
 Alisema kuwa serikali haina haraka juu ya suala hilo kwa kuwa inataka kusikiliza mawazo yawananchama wote, Watanzania, wabunge na wadau mbalimbali ili kupata maoni ambayo yatatafsiriwa kisheria.
 Alisema serikali itawasikiliza 
Watanzania ili kujua ni nini wanapenda kiwepo katika masuala ya hifadhi 
ya jamii kwa sababu sheria na sera siyo msahafu hivyo inaweza kubadilika
 kila mara kutokana na mahitaji ya wakati husika.
 Waziri Kabaka pia alitembelea 
miradi mbalimbali ya jamii inayofadhiliwa na mgodi huo wa Barrick na 
kuisifu kampuni hiyo kwa kusaidia jamii.
 Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa shule mpya na ukarabati mkubwa wa kituo cha afya cha Nyangoto.

No comments:
Post a Comment