Na Mukhsin Mambo
………………………………………………………………
Waziri wa 
Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi Dr. Titus Kamani, amesema ili kwenda na 
kasi ya maboresho ya wizara hiyo, inahitajika dhana ya uwajibikaji na 
uwazi sambamba na kujitolea kwa nguvu zote katika kufanya kazi.
Waziri Kamani, 
ameyasema hayo leo katika mkutano wa kwanza uliowakutanisha wafanyakazi 
wote wa wizara hiyo, wakiwemo wastaafu wa mwaka jana katika ofisi za 
wizara hiyo zilizopo Temeke jijini Dar es Salaam.
Amesema kama 
kuna mtu ambaye ni kikwazo katika kukwamisha shughuli za wizara, ni bora
 akawapisha mapema na kwamba kila mtumishi kwa nafasi yake, anatakiwa 
kuifanya kazi kwa uwazi na akaitaka wizara kufanya kazi na vyombo vya 
habari kwani ndio njia pekee ya kuwafanya watanzania wajue wizara 
inafanya nini.
“Wewe upo 
ofisini, halafu unaogopa ogopa vyombo vya habari, kwani unatatizo gani, 
kuweni wazi mambo yenu yawe hadharani, watanzania wa Mbeya wayajue, 
Rufiji mpaka Pemba, hakuna kufichaficha jambo katika wizara yangu.” 
Alisistiza Dk Kamani.
Amesema wizara 
ya maendeleo ya mifugo na uvuvi ndio moyo wa taifa kwani huwajumuisha 
watanzania wengi wenye maisha ya kawaida, lakini amesikitishwa kwa jinsi
 ambavyo wizara hiyo imekuwa ikichukuliwa na baadhi ya watu kama ni 
wizara ya yenye migogoro na kuleta hasara maeneo mengine.
“N’gombe hawa 
wamekua wakiingia kwenye hifadhi, wanapigwa risasi, wanaaribu mashamba 
ya watu na kuleta njaa kwa wananchi, ngombe hawa wamekuwa wakiambiwa 
wanaleta uharibifu wa mazingira kwa wananchi kwa sababu ya kuhamahama, 
kama ngombe hawa ungepatikana utaratibu mzuri wa kuwatunza, kuwahifadhi 
basi, taifa hili lingeingiza kipato kikubwa ikiwemo kuuza nyama hadi nje
 ya nchi, maziwa na kuboresha afya za watanzania” alisema Dk Kamani.
Dk. Kamani, 
amesema anafahamu Wizara yake ina changamoto nyingi katika kutekeleza 
majukumu yake, ikiwemo bajeti kuwa ndogo, lakini kwa kutumia taaluma 
yake pamoja na ushirikiano wa wafanyakazi wote wa wizara hiyo, anaamini 
wizara hiyo badala ya kuonekana ni laana kwa watanzania, itakuwa ni 
wizara yenye neema kwa watanzania, yenye kueneza ajira na kipato kwa 
sababu hakuna jambo lisilowezekana kama kila mmoja atafanya kazi kwa 
dhamira moja.
Akizungumzia juu
 ya ranchi za taifa, waziri Kamani amesema ana nia ya dhati ya kuona 
ranchi za taifa zinafufuka na kutengeneza uchumi imara wa taifa, 
kuzalisha Ngombe wenye ubora ambao watatoa mazao ya mifugo 
yatakayoliingizia taifa hili kipato kikubwa.
Akizungumzia 
sekta ya uvuvi, Waziri Kamani, amesema sekta hiyo ni tabu tupu, amesema 
leo tunaambiwa kuna uvuvi haramu, nyavu zisizokidhi viwango, huku wavuvi
 wakiendelea kuwa masikini, katika nchi yenye bahari, maziwa na mito 
mikubwa kila kona, ameuliza ni kweli wanahitaji bajeti kubwa ya 
kushughulika na mambo hayo?. 
“Tunahitaji 
utashi wa kuwasadia wavuvi wetu, kwa kutoa elimu na kufanya mazungumzo 
nao ya mara kwa mara, kuwatembelea maeneo yao ya kazi na kubaini 
matatizo yao kisha kuyafanyia kazi” Alibainisha Dk Kamani.
Kuhusu zao la 
kuku, Waziri Kamani amesema sasa hivi kuna tatizo la mayai feki na 
chanjo feki, alihoji ni kweli kwamba wafanyakazi wa wizara hiyo haiwajui
 wahusika au kuna baadhi ya watumishi ndio miradi yao? ambapo aliagiza 
wizara kubaini wanaofanya biashara hiyo feki ambayo inaleta madhara hasa
 wakazi wa mjini ambao ni watumiaji wakubwa wa bidhaa hizo.
Awali, kaimu 
katibu mkuu wa wizara hiyo Dk Yohana Budeba alipongeza uteuzi wa Dk 
Kamani, kuingia katika wizara hiyo kwakuwa ajira yake ya kwanza mwaka 
1982  alikuwa chini ya wizara hiyo kama afisa Mifugo wa kata ya Kisongo 
wilaya ya Arumeru Mkoani Arusha, hivyo changamoto nyingi anazifahamu, ni
 mwenzao na anaamini watashirikiana vyema katika kukabiliana nazo.

No comments:
Post a Comment