Dar es Salaam. Waziri
 wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda amesema kuwa, Serikali 
itaendelea kutengeneza mazingira mazuri ya kufanya biashara ili 
wawekezaji wa nje na ndani waweze kutekeleza majukumu yao bila kikwazo.
Dk
 Kigoda aliyasema hayo juzi usiku alipokuwa kwenye hafla ya kuzitambua 
Kampuni 100 Bora zinazokua kwa kasi nchini (Top 100 Mid–Sized 
Companies), ambapo Kampuni ya Kipipa Millers Limited ya jijini Mwanza 
ilishika nafasi ya kwanza.
Kampuni
 hizo zilitambuliwa na kupewa tuzo kutokana na shindano linaloendeshwa 
na Kampuni ya Mwananchi Communications (MCL) na KPMG Tanzania na 
kudhaminiwa na Benki ya NBC pamoja na Soko la Hisa la Dar es Salaam 
(DSE).
Dk
 Kigoda alisema shindano hilo linaimarika kila mwaka na lina nafasi 
kubwa ya kuimarisha uchumi kwa Kampuni za Afrika Mashariki.
Alisema
 ili kampuni hizo ziweze kufikia mafanikio, Serikali itajitahidi kuweka 
mazingira yatakayoziwezesha kufanya shughuli zake vizuri na kufanya 
uzalishaji kwa gharama nafuu.
Alizitaka
 kampuni zilizofanikiwa kuingia kwenye kundi la kampuni 100 bora, 
kujitambua kuwa sasa wao ni washindi na hivyo wajitahidi kufanya 
shughuli zao kitaalamu zaidi.
“Kwa kiwango hiki mlichofikia sasa ni washindi, mfanye kazi zenu kitaalamu zaidi,”  alisema Dk Kigoda.
Alisema
 kwa sasa Tanzania imeshuka kwenye nchi zenye viwango vizuri vya kufanya
 biashara duniani, hali inayofanya baadhi ya wawekezaji kukimbia.
Alieleza
 suala hilo linaipa Serikali changamoto ya kutengeneza mazingira bora na
 rafiki ili kuvutia wawekezaji kufanya shughuli zao kwa faida.
Kwa
 upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Mwananchi Communications Limited 
(MCL), Zuhura Muro alisema kwa kushirikiana na KPMG, wanaendesha 
shindano hilo kwa sababu wanaelewa kuwa hiyo ni njia muhimu ya 
kuhamasisha kampuni kufanya vizuri.
Alisema
 kuwa, kampuni hizo ni muhimu kwa uchumi wa nchi na ustawi wake kwani 
kodi wanazolipa ndizo zinazotumika kwa maendeleo ya nchi.
“Sasa
 ni wakati wetu wa kuinuka, lakini hatuwezi kuinuka bila kuwa na watu 
muhimu kama ninyi (kampuni 100 bora) kwani ndiyo mnaotengeneza ajira, 
nyie ni watu muhimu sana kwa uchumi wa nchi hii,” alisema Muro.
Huu
 ni mwaka wa tatu wa shindano hilo, mwaka 2011 Kampuni ya BQ Contractors
 ya Dar es Salaam ilishika nafasi ya kwanza, huku mwaka 2012 Kampuni ya 
Helvetic Solar Contractors ya jijini Arusha ikichukua nafasi hiyo.
Mara
 baada ya kutangaza kuwa mshindi jana,  Mkurugenzi Mkuu wa Kipipa 
Millers Limited, Oliver Matemu alisema hakutarajia kushika nafasi hiyo.
“Nilipokuwa
 hapo ndani nilikuwa nasikia tu wakitangaza, walipofika nafasi ya 50 
bila kusikia tukiitwa nilijua kuwa sisi tumerukwa,” alisema Matemu.
Matemu
 alisema kuwa, kampuni yake inajishughulisha na usagaji wa nafaka na 
kuzisambaza pamoja na kusambaza bidhaa za Kiwanda cha Bia cha Tanzania 
(TBL).
“Kilichotufanya tukaibuka washindi ni namna ambavyo tunajitahidi kuandaa hesabu zetu,” alisema Matemu.
Alisema
 kuwa, alianza shughuli hiyo kwa kununua unga kwenye mashine za watu na 
kuusambaza wakati huo akiwa na mtaji wa kati ya Sh1.5 milioni.
“Kwa sasa kwa mwaka nafanya biashara ya kama Sh5 bilioni,” alisema.
Kampuni
 nyingine zilizoingia kwenye 10 bora ni Otonde Group of Companies 
Tanzania Limited, iliyoshika nafasi ya pili, SEEDCO Tanzania Limited ya 
tatu, Kays Logistics Company Limited ya nne, Sihebs Technologies Company
 Limited  ya tano na Techno Brain Tanzania Limited ya sita. 
Kampuni
 nyingine ni Anjari Soda Factory Limited nafasi ya saba, NPK 
Technologies Limited nane, Palray limited ya tisa na Fomcom 
International Limited  nafasi ya 10.

No comments:
Post a Comment