Kiongozi
wa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, Amina Makilagi
akinywa maji yaliyotoka kwenye kisima cha mradi wa maji Ikwiriri
wilayani Rufuji mkoani Pwani, kwenye ziara ya kamati hiyo kukagua miradi
ya maji katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.
Hussein Makame, MAELEO, Pwani
KAMATI ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji imeeleza kuridhishwa
na maendeleo ya utekelezaji wa miradi ya maji ya Kibiti na Ikwiriri
iliyopo wilayani Rufiji mkoani Pwani kutokana na kuonesha mafanikio
makubwa.
Hayo yamesemwa na Kiongozi wa Wajumbe wa Kamati hiyo Amina
Makilagi (Mb) baada ya kukagua miradi hiyo ikiwa ni sehemu ya ziara ya
ukaguzi wa miradi ya maji Tanzania Bara inayofanywa na baadhi ya wajumbe
wa kamati katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.
Alisema pamoja na miradi hiyo kukabiliwa na changamoto
mbalimbali, imeweza kutoa huduma kwa wakazi 34,428 wa maeneo hayo na
wananchi kupitia viongozi wao kuthibitisha mafanikio ya miradi hiyo.
“Kimsingi tumefurahishwa na maendeleo ya utekelezaji wa miradi
hii,tulipokuwa Dar es Salaam tuliambiwa miradi ya Kibiti na Ikwiriri
imekamilika na inaendelea vizuri na wananchi wamekiri hilo kupitia kwa
viongozi wao” alisema Makilagi.
Mradi wa Kibiti wenye visiwa virefu vitano vinavyozalisha maji
safi na salam, huzalisha meta za ujazo 55 kwa saa huku ule wa Ikwiriri
ukiwa na kisima kirefu chenye urefu wa meta 60 na kipenyo cha 14 cha
ujazo na wenye una matanki mawili yenye uwezo wa mita za ujazo 500 kila
moja.
Mtandao wa mradi huo wa maji una pampu inayoweza kusukuma maji
kwa saa 12 na bomba kuu lenye urefu wa kilometa 10 na mabomba
yanayosambaza huduma hiyo kilometa 21 na vituo vya kuchotea maji 5.
Hata hivyo, Makilagi aliwataka wakazi wa maeneo husika kuacha
tabia ya kuiba vipuri vya mabomba ya miradi hiyo kwani Serikali
imewapelekea huduma hiyo kuondokana na ukosefu wa huduma ya maji safi na
salama.
Alisema kamati hiyo imekagua miradi hiyo kutekeleza jukumu la
bunge la kuisimamia serikali katika shughuli za maendeleo ambapo hatua
hiyo italifanya bunge kujihakikishia kile kinachotekelezwa na serikali
katika miradi hiyo.
Kwa upande wake Meneja wa Mradi wa Maji wa Kibiti Mhandisi Juma
Ndaro alieleza changamoto zinazokabili mradi huo ikiwemo kutokuwepo kwa
mamlaka ya kudumu ya maji kwa kuwa mji mdogo wa Kibiti bado
haujatangazwa rasmi kuwa Mji mdogo.
Changamoto nyingine inayokwaza mradi huo ukatikaji wa umeme
unaosababisha mota za maji kuungua na changamoto hiyo kusababisha
upatikanaji wa maji kutokuwa wa kudumu kutokana na kutegemea umeme.
Katika mradi wa Ikwiriri, Mjumbe wa Bodi ya Maji ya Ikwiriri
Kasimu Mpeliwe ambaye ni mwakilishi watumiaji wa maji Ikwiriri,
aliishukuru Serikali kuwapelekea mradi huo kwani umeonesha mafanikio
makubwa.
Hata hivyo aliomba mradi huo upanuliwe ili kukidhi ongezeko la wakazi wa Ikwiriri ambalo limefikia wananchi 45,000.
Ziara ya wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji
inaendelea leo katika mkoa wa Lindi ambapo itakagua miradi ya maji
iliyopo Rombomnara na Ng’apa iliyopo mkoani humo.
No comments:
Post a Comment