TUZO
 za Wanamichezo Bora wa Tanzania zinazotolewa na Chama cha Waandishi wa 
Habari za Michezo Tanzania (TASWA) zinatarajiwa kufanyika Desemba 12 
mwaka huu, huku Kampuni ya Said Salim Bakhresa (SSB) Group Limited 
ikijitokeza kuwa mdhamini mshiriki wa tuzo hizo kwa kutoa Sh. Milioni 
10.
 Akizungumza
 na waandishi wa habari katika mgahawa wa City Sports Lounge, Dar es 
Salaam katika hafla ya kutangaza udhamini huo jana, Meneja Mkuu wa SSB 
Limited, Said Muhammad Said alisema wameamua kudhamini tuzo hizo kama 
hatua mojawapo ya kuinua michezo nchini.
 Aliupongeza
 uongozi wa TASWA kwa juhudi kubwa inazofanya katika kuhamasisha michezo
 na kwamba wameona waunge mkono juhudi hizo kwa kutoa fedha hizo.
 Kwa
 upande wake Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto alisema kampuni mbalimbali 
zimeonesha nia ya kudhamini tuzo hizo na watakuwa wanazitangaza kadri 
watakavyomalizana nazo.
 “Tunaishuku
 sana Bakhressa kwa mchango huu mkubwa kwetu, pia tunaomba wadau 
tushirikiane kwa kila hali kuhakikisha tuzo zetu zinafanikiwa na 
tunaomba kampuni zaidi zijitokeze.
 “Bajeti
 ya tuzo zetu ni Sh milioni 120, zipo kampuni zimeonesha nia ya 
kutusaidia, mwishoni mwa wiki hii au mwanzoni mwa wiki ijayo tutatangaza
 wadhamini wengine,” alisema Pinto.
 Kwa
 upande wake Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando alisema Kamati Maalum ya 
Tuzo hizo inaendelea na mchakato wake wa kupata wanamichezo hao na 
kwamba kadri watakavyokuwa wanapiga hatua watatoa taarifa kwa 
wanahabari.
 Alisema
 maandalizi mengine yanaenda vizuri na wanaamini zitakuwa tuzo bora 
kuliko zote zilizowahi kufanywa na chama hicho katika miaka ya hivi 
karibuni.
 Kwa
 miaka mitano iliyopita walioshinda Tuzo ya Mwanamichezo Bora wa TASWA 
walikuwa ni  Samson Ramadhani (2006),  Martin Sulle  (2007),  Mary Naali
 (2008), ambao wote ni wanariadha, wakati 2009 na 2010 alikuwa mcheza 
netiboli Mwanaidi Hassan na mwaka 2011 alikuwa beki Shomari Kapombe 
ambaye sherehe za kumkabidhi tuzo zilifanyika Juni mwaka 2012. Mwaka 
jana tuzo hizo hazikufanyika.
 Wakati
 huohuo, Mhando alisema chama chake kinaendelea na mazungumzo na 
wadhamini mbalimbali kuhusiana na tamasha kwa ajili ya vyombo vya habari
 ‘Media Day Bonanza’ na kwamba mapema mwezi ujao suala hilo litakuwa 
limemalizika.
No comments:
Post a Comment