24/9/2014 Ukosefu wa uelewa na 
imani potofu miongoni mwa wanajamii ni moja ya chanzo cha unyanyapaa kwa
 watoto wenye tatizo la usonji (Autism) .
Hayo yamesemwa jana na Mke wa Rais
 Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete Mama Salma Kikwete wakati akiongea na Prof. 
Andy Shih ambaye ni Makamu wa Rais mwandamizi wa Mambo ya kisayansi 
kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Autism Speaks yenye makao yake mjini New 
York. 
Mama Kikwete ambaye pia ni 
Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema jamii bado
 haina uelewa kuhusu tatizo la usonji kwani kuna baadhi ya watu 
wanahusisha tatizo hilo na mambo ya ushirikina lakini kama jamii itakuwa
 na uelewa tatizo la unyanyapaa litapungua au kwisha kabisa.
Alisema usonji bado ni tatizo 
nchini Tanzania na nchi zingine lakini wazazi wengi wanaona aibu kusema 
hadharani wana  watoto wenye matatizo hayo na hivyo kuwa vigumu kwa 
watoto hao kupata huduma muhimu ikiwemo elimu.
“Tunatakiwa kufanya kazi kwa 
pamoja na wataalamu waliobobea katika taaluma hii ili kuhakikisha  jamii
 inakuwa na uelewa kuhusu tatizo hilo kwa kufanya hivyo watoto hawa 
watapata huduma za muhimu kama elimu na afya”, alisema Mama Kikwete.
Kwa upande wake Prof. Shih alisema
 Taasisi yake iko tayari kufanya kazi na WAMA ili kuwasaidia watoto 
wenye tatizo la usonji ili waweze kupata elimu na huduma ya afya kama 
watoto wengine.
Prof. Shih alisema tatizo la 
unyanyapaa bado ni kubwa kwa watoto lakini kama jamii itapata elimu na 
kulifahamu tatizo hilo itaweza kuwasaidia watu wenye matatizo hayo na 
hivyo kupunguza tatizo la unyanyapaa. 
Usonji ni hali ya udhaifu katika 
ukuaji wa ubongo ambayo huleta athari kubwa katika mawasiliano, 
mahusiano ya kijamii na utambuzi.Tatizo hili ni la dunia nzima na bado 
hakuna maelekezo kamili ya chanzo chake wala tiba. 
Wanaoathirika zaidi ni watoto wa 
kiume kuliko wa kike kwa uwiano wa nne kwa moja hii ikiwa na maana kuwa 
kila watoto watano wenye usonji wanne ni wa kiume na mmoja wa kike.
Mwaka 1997 wizara ya Elimu na 
Utamaduni ikishirikiana na wanachama wa National Association for People 
with Autism in Tanzania (NAP-T) walianzisha kitengo cha watoto wenye 
usonji katika shule ya msingi Msimbazi Mseto ambacho ni kitengo mama cha
 kutoa huduma. 
Hivi sasa Serikali inavitengo 
vitano, viwili vipo Dar es Salaam, viwili Arusha na kimoja Morogoro. Pia
 kuna vitengo kadhaa vilivyoendeshwa na watu binafsi.

No comments:
Post a Comment