Wanafunzi
 wa darasa la awali katika Shule ya Msingi Nakayaya Wilaya ya Tunduru 
mkoani Ruvuma wakiwa wamekaa chini na mwalimu wao pembeni kuonesha 
sehemu ambayo hutumika kama darasa wawapo masomoni.
 
 
WANAFUNZI wa darasa la awali 
katika Shule ya Msingi Nakayaya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma 
wanasomea chini ya mti kutokana na darasa hilo kuendeshwa bila ya kuwa 
na chumba maalum kwa ajili ya kusomea wanafunzi hao.
Hali hiyo imebainika baada ya 
mwandishi wa habari hizi kuitembelea shule hiyo hivi karibuni na 
kuwakuta wanafunzi wakiwa wamekaa chini huku wakiendelea na masomo hayo 
nje chini ya mti ulio na kivuli cha kuwahifadhi wakati wa jua kali.
Akizungumza shuleni hapo Kaimu 
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Nakayaya, Christina Mhowera alisema 
watoto hao wamelazimika kusomea nje baada ya huduma ya elimu hiyo 
kuanzishwa shuleni hapo bila ya kuwa na jengo maalum kwa wanafunzi wa 
awali.
Alisema awali wanafunzi hao 
walikuwa wakisomea kwenye gofu (jengo mbovu) lililokuwa jirani na shule,
 lakini walilazimika kuondolewa baada ya jengo hilo kutwaliwa kwa 
matumizi mengine. Aliongeza kuwa baada ya hapo walihamishiwa kwenye 
nyumba ya mwalimu kabla ya kukamilika lakini waliondolewa tena na kuanza
 kusomea nje (chini ya mti) hadi sasa.
Alisema darasa hilo lenye jumla 
ya wanafunzi 92 linaendeshwa bila ya kuwa na chumba cha darasa maalum 
wala madawati kutokana na shule hiyo kukabiliwa na uhaba wa vyumba vya 
madarasa hadi hapo watakapopata darasa maalum kwa ajili ya wanafunzi 
hao.
Kwa upande wake mwalimu wa 
darasa hilo, Teckla Milanzi alisema mbali na darasa hilo kutokuwa na 
chumba cha darasa, linakabiliwa na changamoto lukuki ikiwemo ya uhaba wa
 vitendea kazi kama vitabu na vyenzo zingine za kufundishia na hakuna 
bajeti yoyote inayotumwa kuliwezesha darasa hilo.
Aidha uchunguzi uliofanywa 
katika shule nyingine tatu za Wilaya ya Tunduru, yaani Shule ya Msingi 
Nanjoka, Majengo na Shule ya Msingi Tunduru Mchanganyiko kuangalia 
mazingira ya utoaji elimu ya awali katika shule hizo umebainisha 
kukabiliwa na changamoto nyingi hali ambayo inahatarisha msingi wa elimu
 kwa wanafunzi.
Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa 
Shule ya Msingi Nanjoka, Batadhari Mkwela alisema licha ya usajili wa 
wanafunzi wa awali kuongezeka kila mwaka kumekuwa hakuna bajeti ya 
kuendesha elimu hiyo.
“…Darasa la awali linahitaji 
vitendea kazi lakini havipo, hatuna vifaa kama vitabu vya kutosha, 
vyenzo za kufundishia, hakuna bajeti hata ya vifaa hivi toka Serikalini,
 hatuna madawati maalum kwa ajili ya wanafunzi wa awali,” alisema 
Mkwela.
Akizungumzia hali hiyo, Kaimu 
Ofisa Elimu Wilaya ya Tunduru, Abdul Kazembe alisema vyumba vya madarasa
 ni changamoto kubwa eneo hilo licha ya msisitizo kuendelea kutolewa wa 
kila shule ya msingi kuwa na darasa la awali. Alisema mwaka 2013/14 
halmashauri ya wilaya hiyo ilihitaji zaidi ya milioni 366.7 lakini 
ililetewa zaidi ya milioni 196.5 fedha ambayo ni karibia nusu tu ya 
kiasi kilichopitishwa kwenye bajeti hiyo. 
“…Kwa hiyo unaweza kuona kwamba 
ni ngumu kuigawa fedha hii katika matumizi maana kwanza haitoshi na pili
 hata kilichotegemewa kuja ni pungufu zaidi tena sana, sasa sijui 
unaweza kugawa kila shule ipate shilingi ngapi…kwani haitoshelezi,” 
Abdul Kazembe.
Akifafanua zaidi Kaimu Ofisa 
Elimu huyo alisema miundombinu ya madarasa ni changamoto kubwa, kwani 
mwaka 2013 idadi ya mahitaji ya madarasa kwa wilaya nzima ilikuwa ni 
1,715 lakini madarasa yaliopo ni 900 na kitu huku mengine yakiwa ni ya 
muda mrefu na yanaelekea kuchakaa.
No comments:
Post a Comment