Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Naibu Rais wa Afrika Kusini Cyril
Ramaphosa (kulia) na Bw. Bw. Deng Alor Kuol wakifurahia wakati Rais
Salva Kiir Mayardiy wa Sudan ya Kusini (wa pili kushoto) na Makamu waRais wa zamani wa Sudan Dkt Riek Machar Teny (wa pili kulia) wakipeanamikono na kubadilishana nyaraka baada ya kutia saini mkatana wamakubaliano ya kukiunganisha upya chama cha SPLM cha Sudani Kusinikatika hoteli ya Ngurdoto jijini Arusha Jumatano Januari 21, 2015usiku.PICHA NA IKULU
………………………………………………………………………………
MKATABA wa kujenga tena umoja na 
kukiunganisha upya Chama Tawala cha Sudan Kusini cha Sudan People’s 
Liberation Movement (SPLM) ulitiwa saini usiku wa jana, Jumatano, 
Januari 22, 2015, katika sherehe ya kufana iliyofanyika katika Ukumbi wa
 Mikutano wa Hoteli ya Ngurdoto, Wilaya ya Arumeru, Mkoa wa Arusha.
Mkataba huo unaojulikana kama Agreement on the Re-unification of
 Sudan People’s Liberation Movement umepongezwa kuwa ni hatua muhimu 
katika kulitoa taifa changa la Sudan Kusini katika hali ya machafuko, 
vita vya wenyewe kwa wenyewe, kutoelewana na kutoaminiana, mambo ambayo 
yameligubika taifa hilo tokea mwishoni mwa 2013 wakati kutokuelewana 
kulipozuka ndani ya SPLM na hatimaye katika Serikali ya nchi hiyo.
Baada ya siku nzima ya mawasiliano na majadiliano baina ya pande
 zinazovutana ndani ya chama hicho pamoja na viongozi wa nchi jirani na 
rafiki na Sudan Kusini, viongozi watatu wa vikundi vinavyopingana ndani 
ya SPLM walitia saini Mkataba huo muhimu sana.
Viongozi waliotia saini ni Mheshimiwa Salva Kiir Mayardit, Rais 
wa Sudan Kusini ambaye pia ni Mwenyekiti wa SPLM na anayeongoza kundi 
linalojulikana kama SPLM in Government (SPLM-IG), Mheshimiwa Dkt. Riek 
Machar ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa SPLM na pia aliyekuwa Makamu 
wa Rais wa Sudan Kusini anayeongoza kundi la SPLM in Opposition 
(SPLM-IO) na Dkt. Deng Alor Kuol ambaye anaongoza kundi la SPLM Leaders-
 Former Detainees (SPLM Leaders – FD).
Sherehe hiyo ilishuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa 
Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho ndicho kimesimamia mazungumzo 
yaliyozaa Mkataba huo. Rais Kikwete pia ndiye mdhamini mkuu wa Mkataba 
huo.
Wengine walioshuhudia tukio hilo muhimu ni Rais wa Uganda, 
Mheshimiwa Jenerali Yoweri Kaguta Museveni; Rais Uhuru Muigai Kenyatta 
wa Kenya; Naibu wa Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mheshimiwa Cyril 
Ramaphosa, Makamu Mwenyekiti wa zamani wa CCM Mheshimiwa John Samwel 
Malecela ambaye ndiye alikuwa mwenyekiti wa mazungumzo yaliyozaa Mkataba
 huo na Katibu Mkuu wa CCM Mheshimiwa Abdulrahman Kinana ambaye alikuwa 
mwezeshaji wa mazungumzo.
Mazungumzo yaliyozaa Mkataba huo yalianza mwishoni mwa mwaka 
jana baada ya Rais Kikwete na Chama cha CCM kuombwa na Rais Kiir 
Mayardit kukubali chama hicho tawala cha Tanzania kutumia uzoefu na 
ujuzi wake wa miaka mingi wa uongozi na siasa kujaribu kuleta suluhu 
ndani ya SPLM. 
Mazungumzo hayo ya kutafuta suluhu ambayo yamefanyika kwa awamu 
mbili, ya kwanza yakiwa yamefanyika Oktoba mwaka jana na pili yakiwa 
yameanza mwanzoni mwa mwezi huu, Januari 2015, yameongeza thamani kwenye
 mazungumzo mengine yanayofanyika Addis Ababa, Ethiopia chini ya 
usimamizi wa taasisi ya IGAD na yanayojadili jinsi ya kurejesha amani 
nchini humo.
Viongozi wa SPLM wanaamini kuwa kwa sababu mgogoro wa kisiasa 
nchini mwao ulianzia ndani ya chama hicho na kwa sababu SPLM ndicho 
chombo pekee ambacho kinawaunganisha wananchi wote wa Sudan Kusini, basi
 busara inaelekeza kuwa suluhu ianze kutafutwa ndani ya chama hicho.
Mkataba wa jana, kimsingi, unalenga kuweka mazingira ya kujenga 
utulivu, maelewano, amani na umoja wa kudumu ndani ya chama hicho na 
nchini humo kwa kuhakikisha kuwa utekelezaji wa mambo ya msingi 
yaliyokubaliwa kuhusu shughuli za siasa, uongozi na oganisheni ya chama 
hicho yanafanyika bila kukawia.
Mkataba huo pia unalenga kuhakikisha kuwa chama cha SPLM 
kinabuni na kutekeleza sera za kuondokana na ukabila, makundi yenye 
mitazamo finyu na mwenendo wa kijeshi katika siasa za Sudan Kusini.
Aidha, Mkataba huo unalenga kuhakikisha kuwa chama cha SPLM 
kinafanya mageuzi ya kuanza kujenga utamaduni wa kuvumiliana na ujenzi 
wa misingi ya demokrasia.
Mkataba huo pia unataka watu wote ambao walishiriki katika 
mauaji na umwagaji damu katika vita vya wenyewe kwa wenyewe wasiruhusiwe
 kugombea wala kushika nafasi ya uongozi wa umma ndani ya chama hicho.
Pia viongozi wote wa Sudan Kusini wanatakiwa, chini ya Mkataba 
huo, kuwaomba radhi wananchi wa nchi hiyo ya Sudan Kusini kwa kuruhusu 
nchi hiyo kuingia katika machafuko ya umwagaji damu mkubwa.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
22 Januari,2015

No comments:
Post a Comment