Shirikisho la Mpira wa Miguu 
Afrika (CAF) limefanyia marekebisho kanuni zake za michuano ya ngazi ya 
klabu kwa upande wa malazi ambapo sasa timu zitachagua na kujilipia 
zenyewe hoteli zinapokuwa kwenye mechi za ugenini.
Kabla ya marekebisho ya kanuni 
hiyo, timu ngeni ilikuwa ikilipiwa hoteli na timu mwenyeji kwa msafara 
usiozidi watu 25. CAF ilikuwa imepitisha hoteli maalumu katika kila nchi
 ambapo mwenyeji alitakiwa kuziweka timu ngeni.
Kwa marekebisho hayo, Chama cha 
Mpira wa Miguu cha nchi mwenyeji kitakuwa na wajibu wa kuitafutia hoteli
 timu ngeni iwapo tu kitaombwa kufanya hivyo, lakini jukumu la kulipia 
malazi litakuwa la timu yenyewe.
Mwaka huu Tanzania inawakilishwa 
na timu mbili za Azam na Yanga katika michuano ya CAF. Azam inacheza 
Ligi ya Mabingwa (CL) ambapo itaanzia nyumbani Februari 15 mwaka huu kwa
 kuikaribisha El Merreikh ya Sudan kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini 
Dar es Salaam.
Nayo Yanga itacheza michuano ya 
Kombe la Shirikisho (CC), na imepangiwa kucheza mechi ya kwanza nyumbani
 dhidi ya BDF IX ya Botswana. Mechi hiyo itafanyika Februari 14 mwaka 
huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

No comments:
Post a Comment