Na Abdulla Ali Maelezo- Zanzibar 
Vitendo vinavyokwenda kinyume na 
maadili ya kijamii vimekuwa vikishamiri kwa kasi miongoni mwa vijana wa 
Zanzibar licha ya viongozi wa Dini, Wazee na Walimu kuvikemea vitendo 
hivyo.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri 
Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mhe. Bi Hindi Hamad Khamis wakati 
akijibu swali la mwakilishi wa Jimbo la Muyuni Mhe. Jaku Hashim katika 
mkutano wa 18 wa Baraza la Wawakilishi ulioanza leo Chukwani Zanzibar.
Amesema kuwa hivi sasa imekuwa ni 
jambo la kawaida kwa baadhi ya vijana wa kiume hususan wa Kizaanzibari 
kutoboa masikio, kusuka nywele na kujipodoa jambo ambalo ni kinyume cha 
sheria, Silka na Utamaduni wa Mzanzibari.
Mhe Bi Hindi amesema Serikali 
imechukua hatua mbalimbali katika kupambana na tatizo la uvunjifu wa 
Mila, Silka na Desturi ikiwa ni pamoja na kushajihisha kutolewa elimu ya
 Dini na Malezi, Kulinda na Kuhimiza uendelezaji wa Utamaduni pamoja na 
kusambaza ustaarabu wa Mzanzibari kwa njia ya Sanaa ya Maonyesho, Semina
 na Makongamano.
Mhe. Bi Hindi ametanabahisha kuwa 
ili kuondokana na vitendo hivyo viovu, Serikali inapitia upya sheria 
zilizopo zinazohusiana na mambo ya Mila, Silka na Desturi kwa lengo la 
kuzipa nguvu ili kupunguza kasi ya vitendo vinavyoipaka matope Zanzibar 
ambavyo kwa kiasi kikubwa vinachangiwa na uwepo wa utandawazi duniani 
kote.
Aidha amesema tatizo liliopo sio 
kutokuwepo kwa sheria bali ni usimamizi wa sheria hizo na kuthibitishwa 
kwa makosa mbele ya vyombo vya sheria ili kuweza kuchukuliwa hatua 
zinazofaa.
“Kwa kulipatia ufumbuzi tatizo hili, sisi sote hapa ni viongozi na wananchi kwa ujumla tunatakiwa kushirikiana kupiga vita vitendo hivyo na kutilia nguvu usimamizi wa sheria tunazozitunga”, alieleza Naibu waziri Bi hindi.
“Kwa kulipatia ufumbuzi tatizo hili, sisi sote hapa ni viongozi na wananchi kwa ujumla tunatakiwa kushirikiana kupiga vita vitendo hivyo na kutilia nguvu usimamizi wa sheria tunazozitunga”, alieleza Naibu waziri Bi hindi.
Mhe. Bi Hindi amewataka Viongozi, 
Walimu, Viongozi wa Dini na Wananchi kwa ujumla kushirikiana pamoja 
katika kupiga vita vitendo hivyo viovu na kutilia mkazo usimamizi wa 
sheria ili kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.

No comments:
Post a Comment