Akifafanua zaidi, Jaji Warioba alisema kila mtu 
anaweweseka kuhusu kiongozi anayefaa ingawa ni kazi rahisi kumjua 
kutokana na ujuzi tulionao wa miaka zaidi ya 50 ya uhuru.
===================================================
Na Florence Majani, Mwananchi
===================================================
Na Florence Majani, Mwananchi
Dar es Salaam. Wakati Taifa 
zima likiwa katika kitendawili cha kumjua kiongozi wa nchi 
atakayepatikana baada ya Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka huu, Mwenyekiti wa 
iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema Rais
 ajaye anafahamika.
Akizungumza katika mahojiano maalumu jana, Jaji 
Warioba alisema si kazi ngumu kwa Watanzania kumfahamu rais ajaye kwa 
kuwa katika miaka 50 tangu tupate uhuru, Watanzania wanazijua sifa za 
kiongozi bora.
Jaji Warioba alisema; “Tatizo la kumjua rais 
afaaye tunalikwepa lakini linafahamika. Wanaotumia fedha na lugha chafu 
katika kampeni na hao ndiyo wasiotakiwa.” “Katika miaka 50 tunazijua sifa za kiongozi bora. 
Hapa tunakwepa tatizo tu. Tatizo ni matumizi ya fedha na lugha chafu 
katika kampeni,” alisema Jaji Warioba ambaye pia ni waziri mkuu mstaafu.
Hadi sasa wanasiasa zaidi ya 20 wakiwamo wa CCM na
 upinzani wamekuwa ama wanatajwa au wameonyesha nia ya kugombea nafasi 
ya urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Ukiacha wale wanaotajwa, wanasiasa waliotangaza 
nia hiyo kutoka CCM ni Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Januari 
Makamba, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, Mbunge wa 
Nzega, Hamis Kigwangala na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, huku Mbunge wa 
Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed akitangaza nia kupitia ADC.
Akifafanua zaidi, Jaji Warioba alisema kila mtu 
anaweweseka kuhusu kiongozi anayefaa ingawa ni kazi rahisi kumjua 
kutokana na ujuzi tulionao wa miaka zaidi ya 50 ya uhuru.
Kadhalika, Jaji Warioba alisema viongozi wa 
Serikali hawana budi kuangalia taswira ya uchaguzi mkuu ujao kupitia 
uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambao umeonekana kuwa na kasoro 
zilizosababisha vurugu.
“Nchi hii ina amani na tujitahidi kuilinda amani 
yetu. Katika uchaguzi huu tufanye kila tuwezalo kuweka maandalizi yenye 
umakini,” alisema Warioba na kuongeza: “Nasisitiza amani. Uchaguzi wa 
Serikali za Mitaa ni funzo.”
Tetesi kuwania urais
Hivi karibuni baadhi ya vyombo vya habari, 
likiwamo gazeti la chama tawala, viliripoti tetesi kuwa Jaji Warioba 
anaandaliwa kuwania urais kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), 
tetesi ambazo kiongozi huyo alizikanusha vikali.
Jaji Warioba alisema amelitumikia Taifa kwa muda mrefu na aling’atuka kwa mapenzi yake, hivyo hawezi kurudi tena katika siasa.
                
              
“Nimetukanwa sana, nimebezwa, nimekejeliwa kwa mambo mengi 
lakini ukweli ni kuwa nilifanya uamuzi wa kung’atuka katika siasa miaka 
20 iliyopita na siwezi kubadili uamuzi wangu,” alisema.
                
              
Akizungumzia baadhi ya wanasiasa kutumia jina lake
 katika majukwaa na baadhi kumkashifu kwa madai kuwa alimsaliti Baba wa 
Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Jaji Warioba aliwataka wanaofanya hivyo 
wasitumie jina lake kusafisha njia zao katika siasa.
                
              
“Nimeitumikia nchi hii kwa miaka 30, kuanzia mwaka
 1966 hadi 1995 nikang’atuka. Niliufanya uamuzi huo miaka 20 iliyopita, 
nikabaki katika uongozi wa chama nako nikaachia ngazi 2002. Mjue kuwa 
nilifanya hayo kwa umakini mkubwa,” alisema.
                
              
Utata Kura ya Maoni
                
              
Katika mahojiano hayo, pia Jaji Warioba 
alizungumzia mchakato wa kuboresha Daftari la Wapigakura na Sheria ya 
Kura ya Maoni kuwa mwingiliano wake hasa katika kipindi cha uchaguzi 
utaleta mkanganyiko.
                
              
Akizungumzia mkanganyiko huo, Jaji Warioba alisema
 sheria inaweka utaratibu maalumu wa mchakato wa kura ya maoni ambao 
alisema hautaendana na ratiba ya uandikishwaji katika daftari hilo.
                
              
“Kwa utaratibu uliowekwa, Tume ya Taifa ya 
Uchaguzi (NEC) itamaliza kazi Machi na wakati huo kura ya maoni 
imepangwa kufanyika Aprili. Kwa hali hiyo hatuna uhakika kama Tume 
itakamilisha kazi yake katika kipindi hicho,” alisema.
                
              
Jaji Warioba alisema Sheria Kura ya Maoni Na. 3 ya
 mwaka 2014 inasema kuwa wananchi wanatakiwa kupewa elimu ya kura ya 
maoni kwa kipindi cha miezi miwili na mwezi mmoja wa kampeni lakini hadi
 sasa hakuna ratiba inayoeleweka, jambo ambalo linaleta mwingiliano.
                
              
“Hii ni Januari, kama watafuata sheria na kuanza 
kutoa elimu kwa kipindi cha miezi miwili, ina maana itakuwa ni Aprili na
 Mei, ukijumlisha mwezi mmoja wa kampeni ambao ni Juni ina maana kura 
itapigwa Julai. Ikumbukwe kuwa mwezi huo mbio za uchaguzi zitakuwa 
zimepamba moto,” alisema. Kura hiyo ya maoni imepangwa kufanyika Aprili 
30.
                
              
Jaji Warioba alisema ni vyema kama mchakato wa 
Katiba mpya ukaenda kama sheria inavyosema kwani kinyume na hapo mambo 
yataharibika na pengine vurugu zinaweza kutokea katika uchaguzi mkuu.
                
              
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju hakupatikana kuzungumzia utata huo wa kisheria.
Kuhusu matumizi ya BVR
                
              
Kadhalika, Jaji Warioba alisema kwa matumizi ya 
teknolojia BVR katika hatua ya maboresho ya daftari la kudumu la 
wapigakura, kwa uzoefu alio nao, vifaa hivyo vina utata mkubwa hivyo 
unahitajika umakini mkubwa.
                
              
“Nilikwenda Malawi mwaka 2004 nikaona utaratibu wa
 BVR umeleta changamoto kwa sababu tu ni teknolojia mpya. Inahitajika 
elimu ya kina kabla ya matumizi yake,” alisema Jaji Warioba.
                
              
Alitoa mfano wa utata wa BVR kuwa iwapo mpigakura 
atafanya udanganyifu na kujiandikisha mara mbili au zaidi (hata kama 
atatumia majina tofauti), mashine itafuta majina yaliyozidi na kubaki na
 taarifa zake katika kituo kimoja tu.
                
              
Hata hivyo, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian
 Lubuva alisema tume hiyo imeshazifanyia majaribio mashine hizo katika 
majimbo matatu na zimeonyesha ubora na upungufu ulikuwa mdogo huku zile 
zenye kasoro zikifanyiwa marekebisho.

No comments:
Post a Comment