Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa
 Pili wa Rais Mhe. Mohamed Aboud Mohamed amesema Serikali ya Mapinduzi 
ya Zanzibar imeshatayarisha kanuni za usalama wa barabarani za kutoza 
faini za papo kwa papo kama ilivyo sasa kwa upande wa Tanzania Bara.
Hayo ameyaeleza katika ukumbi wa 
Baraza la Wawakilishi Chukwani Zanzibar wakati akijibu swali la 
mwakilishi wa Jimbo la Kwahani Mhe. Ali Salum Haji.
Waziri Mohamed amesema kuwa kanuni
 za sheria ya usalama barabarani kwa upande wa Zanzibar zipo kwa 
Mwanasheria Mkuu kwa hatua za mwisho na zitaanza kutumiwa na Jeshi la 
Polisi mara baada ya kukamilika rasmi kwa kutoza faini ya papo kwa papo 
kwa wote watakaofanya makosa ya usalama wa barabarani.
Waziri Aboud ametanabahisha kuwa 
kwa sasa Zanzibar Sheria Nambari 7 ya Mwaka 2003 (R.E 2006) ndio 
inayosimamia masuala ya usalama barabarani na kwa mujibu wa sheria hiyo 
kifungu namabari 180 hadi 184 vimeelezea kuhusiana na utaratibu wa faini
 ya papo kwa papo kwa vyombo vya moto vinavyovunja sheria za usalama wa 
barabarani Nchini.
Aidha amesema Jeshi la Polisi lina
 jukumu la kusimamia na kutekeleza Sheria zilizotungwa na Bunge la 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar 
ambapo kwa upande wa Tanzania Bara Sheria inayohusika na usalama wa 
barabarani ni Sheria nambari 168 ya Mwaka 2002.
“Miongoni mwa majukumu ya Jeshi la
 Polisi ni kusimamia na kutekeleza Sheria zilizotungwa na Bunge la 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar”, 
alieleza waziri Mohamed.
Hivyo ameeleza kuwa kupitia Sheria
 hiyo Jeshi la Polisi hutekeleza sheria za faini ya papo kwa papo kwa 
vyombo vya moto vinavyovunja sheria za usalama barabarani na kusaidia 
Serikali kukusanya fedha nyingi zinazotokana na makosa hayo.
Jeshi la polisi ni Jeshi la 
Jamhuri ya muungano wa Tanzania na limeundwa kwa mujibu wa katiba ya 
Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 chini ya ibara ya 147 ya kuanzishwa 
kisheria chini ya kifungu nambari 3 cha sheria ya polisi na polisi 
wasaidizi Cap.322 R.E ya mwaka 2002.

No comments:
Post a Comment