Shirika la Ndege la Taifa la 
Shelisheli, Air Seychelles limeanza kufanya safari zake kati ya mji mkuu
 wa nchi hiyo, Mahe na Dar es Salaam ambapo leo, Desemba 2, 2014, ndege 
yake ya abiria HM 777 ilifanya safari yake ya kwanza ya uzinduzi kwa 
kutua Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam.
Ujio wa shirika hilo la ndege 
unafanya mashirika ya ndege yaliyoanzisha safari zake kuja Dar es Salaam
 kwa siku za hivi karibuni kufikia matatu, Air Seychelles, Flydubai ya 
Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Rwandair ya Rwanda. Shirika lingine 
la ndege, Etihad la Abudhabi (UAE) linatarajiwa kuanza safari zake mwaka
 2015.
Uzinduzi wa safari za ndege ya Air
 Seych elles ulifanywa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhandisi Dk. Charles
 Tizeba na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mahmoud 
Mgimwa, wabunge na viongozi kadhaa wa Serikali na wadau wa masuala ya 
sekta ya usafiri wa anga na maliasili na utalii nchini.
Katika hotuba yake, Naibu Waziri 
wa Uchukuzi, Mhandisi Dk. Tizeba alisema ujio wa Air Seychelles 
umefungua ukurasa mpya wa safari kwa wananchi wa nchi za zisizopakana na
 bahari ya Hindi (landlocked) na fursa zaidi za utalii kwani sasa 
watakuwa na uhakika wa kuunganisha safari zao kwenda kokote duniani kwa 
ndege hiyo.
Naibu Waziri Tizeba alisema ujio 
wa ndege hiyo utakuza sekta ya utalii kati ya nchi hizo na kunufaisha 
wananchi wake na kwa kujua umuhimu wa sekta ya usafiri wa anga kwa nchi 
hizo, alizitaka Tanzania na Shelisheli kutekeleza mikakati ya kitaifa, 
kikanda na dunia ya usafiri wa anga kuleta maendeleo ya sekta hiyo nchi 
mwao.
Alitoa rai kwa wafanyabiashara ya 
sekta ya utalii kutumia fursa hii kukukuza biashara kati ya nchi hizi 
kwani Tanzania ina hazina ya vivutio vya utalii ikiwemo maeneo ya 
kihistoria Zanzibar na Bagamoyo, mlima mrefu kuliko yote Afrika, 
Kilimanjaro na moja ya maajabu saba ya dunia, Kreta ya Ngorongoro mkoani
 Manyara.
Naibu Waziri Dk. Tizeba alisema, 
Serikali itafanya kila iwezalo kuhakikisha safari za ndege kati ya 
Tanzania na Shelisheli zinadumu na kwamba Serikali za nchi hizo 
zitahakikisha mkataba wa ushirikiano wa sekta ya usafiri unasainiwa 
haraka iwezekanavyo na mamlaka husika za usafiri wa anga nchini kwa 
mujibu wa masharti ya ICAO.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), 
Mhandisi Suleiman S. Suleiman alisema ujio wa ndege hiyo ni mafanikio 
makubwa kwani unaongeza idadi ya ndege zinazotua JNIA ambapo juzi tu 
ilikuja Flydubai na wanatarajia mwakani, 2015 Emirates itaongeza safari 
kutoka 12 hadi 14 kwa wiki.
“Sisi (TAA) hatulali. Tunafanya 
kazi kwa ushirikiano na mshauri mwelekezi wa biashara ya ndege ambaye 
kazi yake ni kushawishi mashirika zaidi ya ndege kuja Tanzania. Mpaka 
sasa kuna ndege 18 zinazokuja na Januari mwakani, 2015, ndege ya Etihad 
inatarajiwa kuanza safari zake pia”, Mkurugenzi Mkuu huyo wa TAA 
alisema.
Akizungumza katika hafla hiyo, 
Meneja Mkuu wa Mahusiano wa Air Seychelles, Alan Renaud alisema safari 
za ndege hiyo kati ya Mahe – Dar es Salaam zitakuza utalii na biashara 
kati ya Tanzania na Shelisheli na kuwa kiungo cha safari za mashirika 
mengine ya ndege duniani ambako abiria wataunganisha safari zao.
“Dar es Salaam ni njia nyingine 
muhimu ya safari za ndege yetu tulizoongeza na inaonesha hatua mpya ya 
kukua kwa shirika letu. Ikiwa na watu zaidi ya milioni nne na ya pili 
kwa ukubwa ukanda wa bahari ya Hindi, kiungo kikubwa kwenda mbuga na 
hifadhi maarufu za wanyama na vivutio vingine vya utalii kama Mlima 
Kilimanjaro wenye theluji, Dar es Salaam ni chachu kubwa ya utalii na 
biashara,” alisema Renaud katika hotuba yake.
Alisema, ujio wa ndege hiyo ni 
matokeo ya ushirikiano mkubwa kati yao na Shirika kubwa la ndege la 
Etihad Airways lenye hisa asimia 40 lililowawezesha kupata ndege ya 
kwanza aina ya Airbus A320 na kuifanya Mahe kama kitovu cha abiria 
kutoka Afrika Mashariki kwenda nchi za Mashariki ya Kati, Asia na za 
Bara Hindi.
Air Seychelles ilianzishwa mwaka 
1978 na ilianza safari za masafa marefu mwaka 1983. Kwa sasa shirika 
hilo la ndege linafanya safari kwenda Abudhabi, Antananarivo 
(Madagascar), Hong Kong, Johannesburg (Afrika Kusini), Mauritius, Mumbai
 (India) na Paris (Ufaransa) na safari 200 za ndani mwake kwa wiki. Air 
Seychellles itafanya safari zake kati ya Mahe na Dar es Salaam (JNIA) 
mara mbili kwa wiki, Jumanne na Jumapili.


No comments:
Post a Comment