TAN

TAN

Bayport

Bayport

Kikoa

Kikoa

Myway entertainment

Myway entertainment

FORE PLAN CLINIC

FORE PLAN CLINIC

MPINGA CUP 2016

MPINGA CUP 2016

Mashujaa Fm 89.3, Lindi

Tuesday, December 2, 2014

Air Seychelles yazindua safari za ndege Mahe – Dar es Salaam

unnamed
unnamed1
Shirika la Ndege la Taifa la Shelisheli, Air Seychelles limeanza kufanya safari zake kati ya mji mkuu wa nchi hiyo, Mahe na Dar es Salaam ambapo leo, Desemba 2, 2014, ndege yake ya abiria HM 777 ilifanya safari yake ya kwanza ya uzinduzi kwa kutua Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam.
Ujio wa shirika hilo la ndege unafanya mashirika ya ndege yaliyoanzisha safari zake kuja Dar es Salaam kwa siku za hivi karibuni kufikia matatu, Air Seychelles, Flydubai ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Rwandair ya Rwanda. Shirika lingine la ndege, Etihad la Abudhabi (UAE) linatarajiwa kuanza safari zake mwaka 2015.
Uzinduzi wa safari za ndege ya Air Seych elles ulifanywa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhandisi Dk. Charles Tizeba na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mahmoud Mgimwa, wabunge na viongozi kadhaa wa Serikali na wadau wa masuala ya sekta ya usafiri wa anga na maliasili na utalii nchini.
Katika hotuba yake, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhandisi Dk. Tizeba alisema ujio wa Air Seychelles umefungua ukurasa mpya wa safari kwa wananchi wa nchi za zisizopakana na bahari ya Hindi (landlocked) na fursa zaidi za utalii kwani sasa watakuwa na uhakika wa kuunganisha safari zao kwenda kokote duniani kwa ndege hiyo.
Naibu Waziri Tizeba alisema ujio wa ndege hiyo utakuza sekta ya utalii kati ya nchi hizo na kunufaisha wananchi wake na kwa kujua umuhimu wa sekta ya usafiri wa anga kwa nchi hizo, alizitaka Tanzania na Shelisheli kutekeleza mikakati ya kitaifa, kikanda na dunia ya usafiri wa anga kuleta maendeleo ya sekta hiyo nchi mwao.
Alitoa rai kwa wafanyabiashara ya sekta ya utalii kutumia fursa hii kukukuza biashara kati ya nchi hizi kwani Tanzania ina hazina ya vivutio vya utalii ikiwemo maeneo ya kihistoria Zanzibar na Bagamoyo, mlima mrefu kuliko yote Afrika, Kilimanjaro na moja ya maajabu saba ya dunia, Kreta ya Ngorongoro mkoani Manyara.
Naibu Waziri Dk. Tizeba alisema, Serikali itafanya kila iwezalo kuhakikisha safari za ndege kati ya Tanzania na Shelisheli zinadumu na kwamba Serikali za nchi hizo zitahakikisha mkataba wa ushirikiano wa sekta ya usafiri unasainiwa haraka iwezekanavyo na mamlaka husika za usafiri wa anga nchini kwa mujibu wa masharti ya ICAO. Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mhandisi Suleiman S. Suleiman alisema ujio wa ndege hiyo ni mafanikio makubwa kwani unaongeza idadi ya ndege zinazotua JNIA ambapo juzi tu ilikuja Flydubai na wanatarajia mwakani, 2015 Emirates itaongeza safari kutoka 12 hadi 14 kwa wiki.
“Sisi (TAA) hatulali. Tunafanya kazi kwa ushirikiano na mshauri mwelekezi wa biashara ya ndege ambaye kazi yake ni kushawishi mashirika zaidi ya ndege kuja Tanzania. Mpaka sasa kuna ndege 18 zinazokuja na Januari mwakani, 2015, ndege ya Etihad inatarajiwa kuanza safari zake pia”, Mkurugenzi Mkuu huyo wa TAA alisema.
Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja Mkuu wa Mahusiano wa Air Seychelles, Alan Renaud alisema safari za ndege hiyo kati ya Mahe – Dar es Salaam zitakuza utalii na biashara kati ya Tanzania na Shelisheli na kuwa kiungo cha safari za mashirika mengine ya ndege duniani ambako abiria wataunganisha safari zao.
“Dar es Salaam ni njia nyingine muhimu ya safari za ndege yetu tulizoongeza na inaonesha hatua mpya ya kukua kwa shirika letu. Ikiwa na watu zaidi ya milioni nne na ya pili kwa ukubwa ukanda wa bahari ya Hindi, kiungo kikubwa kwenda mbuga na hifadhi maarufu za wanyama na vivutio vingine vya utalii kama Mlima Kilimanjaro wenye theluji, Dar es Salaam ni chachu kubwa ya utalii na biashara,” alisema Renaud katika hotuba yake.
Alisema, ujio wa ndege hiyo ni matokeo ya ushirikiano mkubwa kati yao na Shirika kubwa la ndege la Etihad Airways lenye hisa asimia 40 lililowawezesha kupata ndege ya kwanza aina ya Airbus A320 na kuifanya Mahe kama kitovu cha abiria kutoka Afrika Mashariki kwenda nchi za Mashariki ya Kati, Asia na za Bara Hindi.
Air Seychelles ilianzishwa mwaka 1978 na ilianza safari za masafa marefu mwaka 1983. Kwa sasa shirika hilo la ndege linafanya safari kwenda Abudhabi, Antananarivo (Madagascar), Hong Kong, Johannesburg (Afrika Kusini), Mauritius, Mumbai (India) na Paris (Ufaransa) na safari 200 za ndani mwake kwa wiki. Air Seychellles itafanya safari zake kati ya Mahe na Dar es Salaam (JNIA) mara mbili kwa wiki, Jumanne na Jumapili.

No comments:

Post a Comment