Tigo Tanzania imeshinda tuzo ya “Huduma
 Bora ya Kibunifu” kutokana na huduma yake ya kutuma na kupokea fedha 
kimataifa kati ya Tigo Pesa Tanzania na Tigo Cash Rwanda katika 
kongamano na maonyesho ya kimawasiliano barani Afrika ijulikanayo kama 
AfricaCom iliyofanyika Cape Town, Afrika Kusini hivi karibuni.
Meneja Mkuu wa Tigo Tanzania, Diego Gutierrez, alisema kwamba 
tuzo hii ni matokeo ya kuwa na mwaka wenye mafanikio tele katika huduma 
zake za kifedha, Tigo Pesa, ambayo imeweza kupiga hatua kubwa na 
kusababisha huduma hiyo kupaa kitaifa na kimataifa. 
“Ni heshima kubwa kuweza kufika kwenye sita bora na hatimaye 
kuweza kunyakua ushindi wa tuzo ya AfricaCom 2014 katika Huduma Bora ya 
Kibunifu. Huu ni udhihirisho tosha wa ubunifu wetu kwa ajili ya kutoa 
huduma zilizo bora zaidi kwa wateja wetu wanaotumia huduma yetu ya 
kutuma na kupokea fedha kupitia simu,” alisema Gutierrez wakati 
akizungumza na waandishi wa habari kutoka makao makuu jijini Dar es 
Salaam.
Aliongeza, “Huu umekuwa mwaka 
mzuri sana kwetu katika huduma za kifedha kupitia simu. Tumeweza kuwa wa
 kwanza kuanzisha na kuzindua huduma ya kwanza ya kutuma na kupokea 
fedha ya kimataifa yenye uwezo wa kubadilisha moja kwa moja ankara ya 
fedha kati ya Tigo Pesa na Tigo Cash Rwanda ambayo imeweza kushinda tuzo
 hiyo ya AfricaCom 2014. Huduma ingine ya kwanza duniani ambayo tumeweza
 kuianzisha na kuzindua mwaka huu ni gawio la Tigo Pesa kwa wateja wetu 
ambao wameanza kupokea marejesho ya fedha kila baada ya miezi mine 
katika akaunti zao za Tigo Pesa, ambayo imeweza kutusaidia kutimiza 
wajibu wetu wa kuwajumuisha wale ambao hawajafikiwa bado na huduma za 
kifedha kupitia simu.”
Huduma zingine za kibunifu ambazo 
Tigo imeweza kuzindua mwaka huu pia ni ushirikiano kati ya Tigo, Airtel 
na Zantel ambao inawaruhusu wateja kuweza kutuma na kupokea fedha moja 
kwa moja katika akaunti za mitandao hii ya simu bila ukiritimba wowote.
Mapema mwaka huu, kampuni iliweza 
kushirikiana na benki 17 nchini Tanzania ili kuwawezesha watumiaji wa 
Tigo Pesa, kutuma na kupokea fedha kwa akaunti zao za benki kutoka 
kwenye mifuko yao ya Tigo Pesa. Hii inawapatia wateja wetu fursa ya 
kupata huduma ya kutoa na kuweka fedha kupitia Tigo Pesa na akaunti zao 
za kibenki kwa masaa ishirini nan ne.
“Napenda kuwashukuru wateja wetu wa Tigo Pesa milioni 3.6 ambao 
wamekuwa wakitumia huduma zetu kila siku. Wao ndio uti wa mgongo wa 
motisha yetu Tigo kuweza kufanya vizuri zaidi, pamoja na kuja na huduma 
za kibunifu zaidi,” alisema Gutierrez.
AfricaCom ni kongomano na maonesho ya kimawasiliano ya kila 
mwaka barani Afrika. Ilifanyika Cape Town, Afrika Kusini kati ya tarehe 
11 – 13 Novemba, 2014.
Tuzo za mwaka huu ziliweza kujumuisha mashindano ya tuzo 16 
tofauti katika sekta ya mawasiliano kuanzia kwenye masuala ya mtandao 
mpaka mambo ya masoko.

No comments:
Post a Comment