Mechi ya Nani Mtani Jembe 2 kati 
ya Simba na Yanga zinazodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itachezwa
 Jumamosi, Disemba 13, 2014 saa kumi kamili jioni kwenye Uwanja wa Taifa
 jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari
 leo jijini Dar es Salaam, Meneja Udhamini wa TBL, George Kavishe 
amesema kwamba “Tayari Simba na Yanga zimesaini makubaliano ya kucheza 
mechi ya Nani Mtani Jembe 2 (Nani Mtani Jembe 2 Match). Pambano hili ni 
zawadi ya kufungia mwaka kwa mashabiki na kila timu imetia saini 
makubaliano kwamba itachezesha kikosi cha kwanza ili kuwapa mashabiki 
burudani ya uhakika.”
Kavishe aliongeza kuwa mechi hii 
ni maalumu kwa ajili ya kuhitimisha kampeni ya Nani Mtani Jembe 2 ambayo
 imeendeshwa kwa zaidi ya miezi miwili ikiwapa fursa mashabiki wa timu 
hizi kuchangia timu zao kila wanapoburudika na bia ya Kilimanjaro 
Premium Lager.
Alisema Nani Mtani Jembe 2 
inahusisha mashabiki wa klabu za Simba na Yanga ambapo zawadi ya 
shilingi milioni 100 itatolewa na kugawanywa ifuatavyo.
Shilingi Milioni 20 ni zawadi ya 
mechi ya Nani Mtani Jembe ambapo timu itakayoshinda itapata sh milioni 
15 na timu itakayofungwa itapata shilingi milioni 5.
 Kampeni hii inaendeshwa kwa njia ya sms ambapo mashabiki 
wanapiga kura kwa njia ya sms na shilingi milioni 80 zimegawanywa kati 
ya timu hizo mbili ambapo kila timu ilianza na shillingi milioni 40 
kwenye benki maalumu mtandaoni.
Meneja wa Bia ya Kilimanjaro 
Premium Lager, Pamela Kikuli alisema mashabiki wa Simba na Yanga 
wanaweza kushiriki kwa kununua bia ya Kilimanjaro Premium Lager yenye 
ujazo wa mililita 500 ambapo mteja atabandua ganda la kizibo cha bia ya 
Kilimanjaro Premium Lager na kuona namba maalumu. Ataandika jina la timu
 yake (SIMBA au YANGA) ikifuatiwa na namba hiyo ya kwenye kizibo ambayo 
anatuma kwenda namba 15415 na kwa kufanya hivyo anakuwa amepunguza pesa 
taslimu shilingi 10,000 kutoka timu pinzani na kuichangia timu yake.
Kikuli pia alizikabidhi timu hizo 
jezi maalumu itakayovaliwa mahususi kwa ajili ya mechi hiyo na 
kuwahimiza mashabiki waendelee kuzipigia kura timu zao na kikubwa 
kuhakikisha wanafika uwanja wa taifa na kujionea wenyewe pambano hilo 
ambalo lazima mshindi apatikane.
Mkurugenzi wa Mashindano wa 
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Boniface Wambura 
aliwakaribisha mashabiki na kuwaomba wajitokeze kwa wingi kwani hivi 
sasa timu hizo ziko kambini zikijiandaa na mtanage huo wa kukata na 
shoka unaotarajiwa kuwa na msisimko mkubwa.
Alitaja viingilio vya mechi hiyo 
kuwa ni shilingi 30,000 kwa VIP B, 20,000/= VIP C, 15,000/= kwa viti vya
 rangi ya chungwa kiingilio kitakuwa ni sh 15,000 huku viti vya bluu na 
kijani tiketi zikiuzwa kwa sh. 7,000/=.
Wambura alisema pambano hilo 
litakalosimamiwa na TFF litaanza saa kumi kamili na litachezwa kwa 
dakika 90 tu ambapo kama muda huo timu hizo hazitafungana basi mikwaju 
ya penati itapigwa ili mshindi apatikane.
Taji la Nani Mtani Jembe linashikiliwa na Simba ambao waliwafunga mahasimu wao 3-1 katika mechi iliyochezwa Disemba 21, 2013.

No comments:
Post a Comment