Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir Minja akitoa hotuba yake 
fupi katika Baraza la kufunga Mwaka 2014 na kuukaribisha Mwaka Mpya 2015
 katika Ofisi za Makao Makuu ya Magereza(kulia) ni Kamishna wa Sheria na
 Uendeshaji wa Magereza, Dkt. Juma Malewa(kushoto) ni Mnadhimu Mkuu wa 
Jeshi la Magereza, Kamishna Mwandamizi Msaidizi wa Magereza, Mmeta 
Manyala. 
Baadhi
 ya Maafisa na Askari wa Jeshi la Magereza kutoka Ofisi ya Makao Makuu 
ya Magereza pamoja na Mkoa wa Dar es Salaam wakisikiliza kwa makini 
hotuba ya Kamishna Jenerali wa Magereza. 
 Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, Dkt. Juma Malewa akitoa 
neno la shukrani kwa Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir 
Minja(katikati) mara baada ya kutoa hotuba fupi katika Baraza la kufunga
 Mwaka 2014 na kuukaribisha Mwaka Mpya 2015. 
 Maafisa na Askari wa Jeshi la Magereza kutoka Ofisi ya Makao Makuu ya 
Magereza pamoja na Mkoa wa Dar es Salaam wakiwa wamesimama kwa ajili ya 
kuwakumbuka na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu Watumishi wenzao ambao 
wametangulia mbele ya haki kwa mwaka huu 2014.
………………………………………………………………………………..
Na Inspekta Lucas Mboje, Jeshi la Magereza
Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini, John Casmir Minja amewaasa
 Maafisa na Askari wa Jeshi la Magereza nchini kuzingatia Sheria, 
Kanuni, Taratibu na Miongozo katika utendaji wao wa kazi za kila siku 
ili kuleta ufanisi kazini.
Kamishna Jenerali John Minja 
ameyasema hayo leo wakati wa Baraza la Kufunga Mwaka 2014 na 
kuukaribisha Mwaka 2015 lililowahusisha baadhi ya Maafisa na Askari 
kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Magereza pamoja na Magereza Mkoa wa 
D’Salaam.
Aidha, amewataka Maofisa, Askari 
na Watumishi wote kuacha tabia ya kufanya kazi kwa mazoea bali wawe 
wabunifu kwa kutumia raslimali zilizopo kwenye maeneo yao ya kazi ili 
kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo.
” Kila mmoja wenu atimize wajibu 
wake katika eneo lake la kazi kwa bidii, ari na moyo wa kujituma ili 
kuliwezesha Jeshi kupata ufanisi unaotarajiwa”. Alisisitiza Jenerali 
Minja.
Wakati huo huo Kamishna Jenerali 
wa Magereza Nchini, John Casmir Minja pia ametumia fursa hiyo kuelezea 
baadhi ya mafanikio mbalimbali yaliyopatikana kwa Mwaka uliopita 2014 
ambapo Jeshi la Magereza limepata jumla ya leseni 102 za uchimbaji wa 
madini ya ujenzi kama vile chokaa, mawe, kokoto, mchanga na Murram 
katika maeneo mbalimbali ya magereza ambayo ni Gereza Wazo Hill – 
D’Salaam, Gereza Msalato – Dodoma, Kambi Bahi – Dodoma, Gereza Maweni – 
Tanga, Gereza Lilungu – Mtwara, Gereza Butimba – Mwanza na Gereza 
Kalilankulukulu – Katavi. Leseni hizo zitatumika kuingia ubia na 
wawekezaji wenye nia ya kushirikiana na Jeshi katika uchimbaji wa 
madini.
Pili, Shirika la Magereza 
limeeingia Mkataba wa ubia na Kiwanda cha Saruji Wazo (Twiga Cement) 
katika uchimbaji wa madini ya ujenzi Gereza Wazo Hill. Aidha, Kiwanda 
hicho katika kutekeleza wajibu kwa jamii wametoa msaada wa mifuko ya 
saruji 1200 na Tzs.100, 000, 000.00 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za 
makazi ya askari Gereza Wazo Hill. Pia Shirika la Magereza limeingia 
makubaliano na Mfuko wa Mafao ya Kustaafu wa GEPF kwa ajili ya ujenzi na
 uendeshaji wa vituo vya biashara (business malls) kwenye maeneo ya 
Gereza Kihonda, Morogoro na Gereza Karanga, Moshi. 
Tatu, Rasimu ya kwanza ya Sera ya Taifa ya magereza imekamilika 
na tayari imewasilishwa kwenye mamlaka za juu kwa hatua zaidi. 
Kukamilika kwa sera hiyo kutawezesha Jeshi kutekeleza Mpango Mkakati wa 
Sera na Maboresho ya Jeshi kwa ujumla.
Pamoja na Mafanikio hayo, Kamishna
 Jenerali Minja ameelezea maeneo yatakayopewa kipaumbele kwa Mwaka huu 
wa 2015 ikiwemo Jeshi litaendeleza jitihada za kuimarisha na kuongeza 
uzalishaji kwenye miradi mbalimbali ya Jeshi la Magereza. Jitihada hizi 
ni pamoja kutangaza fursa zilizopo ili kuwavutia wawekezaji mbalimbali 
wa ndani na nje ya nchi waje kuingia ubia katika miradi hiyo kwa kuleta 
mitaji na teknolojia, pia Kuendeleza mikakati ya kupunguza msongamano 
magerezani
Baraza la kufunga Mwaka na 
kuukaribisha Mwaka unaofuata ni utamaduni wa siku nyingi ambao unaenziwa
 na Viongozi Wakuu wa Jeshi la Magereza. Baraza la aina hii hufanyika 
kila Mwaka ambapo Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini hupata fursa ya 
kuongea na Watumishi wote wa Jeshi la Magereza nchini kupitia Baraza 
hilo lengo ikiwa ni kufanya tathmini ya yale yaliyojiri katika Jeshi kwa
 kipindi cha Mwaka unaisha kwa kuzungumzia mafanikio na changamoto 
zilizojitokeza na kutazama matarajio ya Mwaka mpya.
No comments:
Post a Comment