Napenda nichukue fursa hii kutoa 
ufafanuzi wa taharuki iliyotokea jana tarehe 02 Januari, 2015 katika 
jiji la Dar es Salaam ikiwahusisha baadhi ya vijana wanaojikusanya 
kwenye vikundi na kujiita Panya road na pengine kusababisha hofu kubwa 
kwa wananchi.
Chanzo cha taharuki hiyo, 
kulitokana na kuuawa kwa kijana mmoja ajulikanae kwa jina la Mohamed 
Ayub na wananchi tarehe 01/01/2015 katika maeneo ya Tandale kwa Mtogole 
kwa tuhuma za wizi wakati wa mkesha wa sikukuu ya mwaka mpya. Tarehe 
02/01/2015 majira ya saa tisa mchana yalifanyika mazishi ya kijana huyo 
katika makaburi ya Kihatu Kagera Mikoroshini na taarifa zilizokuwa 
zimelifikia Jeshi la Polisi Kanda ya Dar es Salaam ni kwamba baada ya 
mazishi hayo vijana wenzake na marehemu walijipanga kufanya fujo ili 
kulipiza kisasi cha mwenzao kuuawa. Aidha, kabla vurugu hizo 
hazijafanyika na kwa vile Polisi walishaona dalili ya vurugu hizo, 
tayari walifanikiwa kuzidhibiti.
Baada ya vurugu hizo kudhibitiwa 
na Polisi, vijana hao walitawanyika kwa kukimbia katika maeneo 
mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam na kuzua taharuki kubwa kwa wananchi
 kwamba huenda kila walipokimbilia wanampango wa kuwafanyia fujo raia 
wema, jambo ambalo wasingeweza kulifanya kwa vile Polisi walikuwa 
wameimarisha ulinzi katika maeneo yote ya jiji.
Kufuatia hali hiyo na Jeshi la 
Polisi nchini likiwa linaendelea na msako mkali wa kuwabaini na 
kuwakamata wote wanaojihusisha na uhalifu huo, tunawaomba wananchi 
watulie, wasiwe na hofu na waendelee na majukumu yao kama kawaida. Mpaka
 sasa tunawashikilia watuhumiwa 36 kwa mahojiano na uchunguzi 
utakapokamilika tutawafikisha mahakamani mara moja.
Aidha, Jeshi la Polisi linatoa 
onyo kwa vijana hao wananojihusisha na vikundi hivyo kuacha tabia hiyo 
mara moja. Tumejipanga vizuri katika mikoa yote kuhakikisha kwamba nchi 
inaongozwa kwa kufuata utawala wa sheria, hatutamwonea muhali mtu yeyote
 ama kikundi cha watu wanaotaka kuvuruga amani ya nchi na kutia hofu 
wananchi.
Wananchi waendelee kutupa 
ushirikiano kwa kutoa taarifa kupitia namba ya simu 0754 78 55 57, namba
 za makamanda au katika kituo chochote cha Polisi.
Imetolewa na:-
Advera John Bulimba – SSP
Msemaji wa Jeshi la Polisi.

No comments:
Post a Comment