Katibu 
Mkuu wa Chama cha Kijamii (CCK), Renatus Muabhi (katikati), akizungumza 
katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kwa niaba ya 
vyama 10 visivyo na uwakilishi wa wabunge Bungeni wakati wakitoa tamko 
kuhusu viongozi wa dini kutojihusisha na masuala ya siasa wakati huu wa 
kuelekea uchaguzi mkuu 2015 . Kutoka kushoto ni Katibu Mkuu wa Chama cha
 Sauti ya Umma (Sau), Ali Kaniki na Katibu Mkuu wa Chama cha Wakulima 
Tanzania (AFP), Rashid Rai.
 Katibu
 Mkuu wa Chama cha Wakulima Tanzania (AFP), Rashid Rai (katikati), 
akizungumza katika mkutano huo. Kulia ni Naibu  Katibu Mkuu wa Chama cha
 UMD, Moshi Kigundula na Katibu Mkuu wa Chama cha Kijamii (CCK), Renatus
 Muabhi.
 Katibu Mkuu wa Chama cha Sauti ya Umma (Sau), Ali Kaniki (kulia),
 akizungumza katika mkutano huo kuhusu suala zima la Nishati ya umeme 
nchini na sakata la Escrow. Kushoto Kiongozi wa chama cha Jahazi Asilia 
Mbwana Kibande na Amina Mcheka kutoka chama cha Chausta.
 Naibu Katibu Mkuu wa wa Chama cha UPDP, Felix Makuwa (kulia), akichangia jambo kwenye mkutano huo.
 Mwakilishi kutoka chama cha Chausta, Amina Mcheka akitoa ufafanuzi wa masuala kadhaa katika mkutano huo.
 Mwakilishi kutoka chama cha Jahazi Asilia, Mbwana Kibande (kushoto) naye akichangia jambo kwenye mkutano huo.
 viongozi wa vyama hivyo wakiwa kwenye mkutano huo.
Wanahabari wakichukua taarifa hizo.
…………………………………………………………………………….
Dotto Mwaibale
VYAMA 
kumi visivyokuwa na uwakilishi bungeni vimewaonya  viongozi wa dini 
nchini katika kipindi cha mwaka huu ambako kutafanyika uchaguzi mkuu 
kutojihusisha na masuala ya siasa kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha 
sheria na katiba ya nchi.
Aidha, 
vyama hivyo vimeitaka serikali kupitia upya mikataba ya makampuni 
yanayozalisha umeme nchini kwa kuwa baadhi yanauza nishati hiyo kwa 
gharama kubwa licha ya kwamba baadhi yanazalisha umeme kwa kutumia gesi 
na kusababisha wananchi kuingia gharama kubwa.
Tamko 
hilo limetolewa na makatibu wakuu wa vyama vya AFP, CCK, SAU, UMD, 
Chausta, UPDP, NRA, Jahazi, Chauma na DP ikiwa ni salamu za kukaribisha 
mwaka mpya wa 2015.
Katibu 
Mkuu wa AFP, Rashid Rai, akisoma tamko hilo jana jijini Dar es Salaam 
kwa niaba ya wenzake, alisema katika miaka ya hivi karibuni kumejitokeza
 tabia ya viongozi wa dini kujihusisha na masuala ya siasa hususani 
kipindi cha uchaguzi mkuu na hivyo kuwachanganya wananchi.
Rai 
alisema viongozi hao wamekuwa wakitoa matamko kwenye vyombo vya habari 
kupendekeza au kutoa sifa ya kiongozi anayefaa kuongoza nchi au asiyefaa
 kupewa nafasi ya uongozi wa umma katika Taifa.
Alisema 
viongozi wa dini lazima watambue kuwa sheria inazuia viongozi wa dini 
kujihusisha na masuala ya siasa kwani hali hiyo inawachanganya wananchi 
kushindwa kujua kama viongozi hao wamebadilisha majukumu yao.
“Unakuta 
kiongozi wa dini anasema Rais ajaye awe ni mwadilifu na mcha Mungu, au 
anasema  kiongozi huyu ni chaguo la Mungu, maana yake ni nini,kila dini 
au dhehebu lina vigezo vyake vya uadilifu na ucha  Mungu,”alisema.
Rai 
alisema kama viongozi wa dini wanaona watu waliopo kwenye siasa 
wanafaidi sana ni bora wakaachana na masuala ya kuhubiri dini badala 
yake waanzishe vyama vya siasa au wajiunge na vyama vya siasa ili 
waendelee kupata neema wanayohisi inapatikana huko.
Kwa 
upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha SAU, Ali Kaniki, alisema sakata la 
akaunti ya Tegeta Escrow limetoa fundisho kwa serikali kuona umuhimu wa 
kupitia upya mikata ya makapuni yote ya makampuni yanayozalisha umeme.
Alisema 
baadhi ya makampuni yanayozalisha umeme na kuliuzia Shirika la Umeme 
nchini (Tanesco) yanatoza tozo kubwa hali ambayo imekuwa ikisababisha 
gharama za umeme kuwa kubwa hapa nchini.
“Tunayo 
makampuni yanayozalisha umeme hapa nchini ambayo ni Songas, IPTL Aggreko
 na Symbion, ukiangalia yote IPTL ndiyo inayouza umeme kwa bei ndogo 
ukilinganisha na mengi, tunataka serikali ipitie mikataba ya makampuni 
haya,”alisema.
Naye 
Katibu Mkuu wa CCK, Renatus Muabhi, alisema katika hali ya kushangaza 
baadhi ya makampuni licha ya kwamba yanatumia nishati ya gesi kuzalisha 
umeme lakini yamekuwa yakiuza umeme kwa bei ya juu.
No comments:
Post a Comment