LIGI KUU YA VODACOM YAINGIA RAUNDI YA 9.
Wakati raundi ya nane ya Ligi Kuu 
ya Vodacom (VPL) inakamilika leo (Desemba 29 mwaka huu) kwa mechi tatu, 
ligi hiyo itaingia raundi ya tisa Januari 3 mwakani kwa mechi tano.
Coastal Union itacheza na JKT Ruvu
 katika Uwanja wa Mkwakwani, Ruvu Shooting itaikaribisha Kagera Sugar 
kwenye Uwanja wa Mabatini, Azam itakuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar katika 
Uwanja wa Azam Complex, Stand United itakuwa mgeni wa Polisi Morogoro 
kwenye Uwanja wa Jamhuri wakati Mbeya City na Yanga zitaoneshana kazi 
kwenye Uwanja wa Sokoine.
Ligi hiyo ambayo itachezwa 
mfululizo (non-stop) hadi itakapomalizika Mei 9 mwakani, itakamilisha 
raundi ya tisa Januari 4 mwakani kwa mechi kati ya Mgambo Shooting na 
Simba kwenye Uwanja wa Mkwakwani, na Tanzania Prisons itakayokuwa 
mwenyeji wa Ndanda kwenye Uwanja wa Sokoine.
Nayo mechi kati ya Mtibwa Sugar na
 Stand United ambayo jana ilivunjwa na mvua dakika ya 6 imemaliziwa leo 
ambapo timu hizo zimetoka sare ya bao 1-1.
Wakati huo huo, mechi ya ligi 
iliyochezwa jana usiku kwenye Uwanja wa Azam Complex imemalizika kwa 
wageni Ruvu Shooting kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya JKT Ruvu. 
Bao hilo lilifungwa kipindi cha kwanza kwa mkwaju wa penalti uliopigwa 
na Hamisi Kasanga.  
MBAO FC YAKAMATA USUKANI SDL
Timu ya Mbao FC ya Mwanza 
imekamata uongozi wa Kundi B la michuano ya Ligi Daraja la Pili (SDL) 
baada ya jana (Desemba 27 mwaka huu) kuizamisha JKT Rwamkoma ya Mara 
mabao 2-1.
Kwa matokeo hayo katika mechi hiyo
 iliyochezwa Uwanja wa CCM Kirumba, Mbao FC imeitoa kileleni JKT 
Rwamkoma baada ya kufikisha pointi tisa kwa kushinda mechi zote tatu 
dhidi ya Arusha FC, Pamba na JKT Rwamkoma.
Mbao FC inafuatiwa na JKT Rwamkoma
 yenye pointi sita, Arusha FC pointi sita wakati Bulyanhulu na Pamba 
zikiwa za mwisho kwa pointi moja kila moja. Kundi hilo litakamilisha 
mzunguko wa kwanza Januari 3 mwakani kwa mechi kati ya JKT Rwamkoma na 
Arusha FC, na Bulyanhulu na Mbao FC.
Katika kundi A, Mji Mkuu (CDA) na 
Singida United ndizo zinazochuana kileleni kwa kufikisha pointi saba 
kila moja. Timu hizo zinafuatiwa na Milambo yenye pointi nne, Mvuvumwa 
FC yenye pointi moja wakati Ujenzi Rukwa ni ya mwisho ikiwa haina 
pointi.
Hata hivyo, Mvuvumwa FC na Milambo
 ziko nyuma kwa mechi moja. Mechi hiyo ya kukamilisha raundi ya tatu 
kati ya timu hizo itachezwa kesho (Desemba 29 mwaka huu) kwenye Uwanja 
wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.
Kiluvya United imeendelea 
kuchachafya kundi C baada ya kushinda mechi zote ne ilizocheza, hivyo 
kufikisha pointi 12. Inafuatiwa na Mshikamano yenye pointi saba huku 
Abajalo ikiwa katika nafasi ya tatu kwa pointi 6.
Nafasi ya nne inashikwa na Transit
 Camp yenye pointi nne, Cosmopolitan yenye pointi mbili ni ya tano 
wakati Kariakoo ambayo haina pointi ni ya mwisho. Hata hivyo, 
Cosmopolitan na Kariakoo zina mchezo mmoja mkononi.
Mechi zinazofuata za kundi hilo ni
 Januari 3 mwakani kati ya Kariakoo na Mshikamano na Mshikamano (Ilulu),
 Transit Camp na Abajalo (Mabatini), na Cosmopolitan na Kiluvya 
(Karume).
Kundi D, vinara bado ni Njombe Mji
 yenye pointi 12 ikifuatiwa na Wenda yenye pointi sita wakati Volcano FC
 iko nafasi ya tatu ikiwa na pointi tano. Mkamba Rangers ina pointi nne,
 Town Small Boys ina pointi moja wakati Magereza FC haina pointi.
Katika kundi hilo leo (Desemba 28 
mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Town Small Boys na Magereza 
itakayochezwa Uwanja wa Majimaji mjini Songea.  Januari 3 mwakani 
kutakuwa na mechi kati ya Town Small Boys na Njombe Mji, Volcano FC na 
Magereza, na Wenda na Mkamba Rangers.

No comments:
Post a Comment