Mke
 wa Rais na Mjumbe wa NEC Taifa ya Chama Cha Mapinduzi Mama Salma 
Kikwete akiwahutubia wananchi wa Kata ya Rasibura katika mkutano wa 
hadhara uliofanyika katika Tawi la Stendi huko Lindi Mjini tarehe 
27.12.2014.
 PICHA NA JOHN  LUKUWI     
Mke
 wa Rais na Mjumbe wa NEC Taifa ya CCM anayewakilisha Lindi Mjini Mama 
Salma Kikwete akizungumza na viongozi wa Tawi la CCM la Mbanja. Mama 
Salma alitembelea tawi hilo tarehe 27.12.2014 kwa ajili ya kukagua kazi 
ya utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi. 
 Baadhi ya wajumbe wa Tawi la Chama Cha Mapinduzi Mabano katika Kata ya 
Mbanja wakifurahia hotuba ya Mjumbe wa NEC Taifa wa Lindi Mjini Mama 
Salma Kikwete wakati alipotembelea Tawi hilo tarehe 27.12.2014. 
Katibu
 wa Shina la Wakereketwa Zahanati Kempu Ndugu Hidaya Chivi Ali 
akikabidhi risala ya wanachama wa Shina hilo kwa Mjumbe wa NEC Taifa na 
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete tarehe 27.12.2014. 
Mke
 wa Rais na Mjumbe wa NEC Taifa ya Chama cha Mapinduzi anayewakilisha 
Lindi Mjini Mama Salma Kikwete akiongea na vijana na wananchi mara baada
 ya kuzindua rasmi shina la wakereketwa Zahanati Kempu lililoko katika 
Kata ya Rasibura tarehe 27.12.2014.
………………………………………………………………………………
Na Anna Nkinda – Maelezo, Lindi
 Wakazi wa mkoa wa Lindi 
wametakiwa kushikamana kwa  pamoja, kufanya kazi kwa bidii  na kuzitumia
 rasilimali zilizopo ili kujiletea maendeleo.
Rai hiyo imetolewa jana Mjumbe wa 
Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia 
wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete wakati akiongea kwenye mkutano 
wa hadhara uliofanyika Mitwero Stendi Kata ya Rasibura wilayani humo.
Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais
 Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema mkoa wa Lindi  umejaliwa kuwa na 
rasilimali nyingi  ikiwa ni pamoja na zao la korosho, ardhi yenye 
rutuba, bahari  na  gesi lakini bado kuna changamoto zinazowakabili 
wananchi na hivyo kukwamisha maendeleo yao.
Alizitaja changamoto hizo kuwa ni 
pamoja na elimu kwani baadhi ya wanafunzi wafikapo darasa la tano 
wanaacha  shule kwa ajili ya utoro, mimba za utotoni na vijana 
kutokufanya kazi kwa bidii.
“Kuna baadhi ya watoto wakifika 
darasa la tano wanaanza tabia ya utoro hakikisheni wanakwenda shule 
kusoma kwani elimu itawasaidia katika maisha yao,  msikubali waache 
shule.  Kutokana na umri wao mdogo wanaona  raha kuacha shule na kwenda 
kucheza lakini wakifika umri wa utu uzima ndiyo watakapoona umuhimu wa 
elimu”. 
Maisha bora kwa kila mtanzania 
yanawezekana ikiwa kila mtu atapata elimu itakayomsaidia  katika maisha 
yake, wakati shule za Sekondari za Kata zinajengwa kuna baadhi ya watu 
walitubeza na kuziita majina ya ajabu ikiwa ni pamoja na shule za 
Yeboyebo lakini shule hizi zimewasaidia watoto wengi kutoka familia 
maskini ambao wameweza kupata elimu”, alisema Mama Kikwete. 
Kuhusu  tazizo la mimba za utotoni
 alisema ni hatari kwa maisha ya Mama na mtoto lakini kama kijana 
atasoma mimba zitaepukika,  jukumu la wananchi ni kuhakikisha watoto wao
 wanasoma  kwa bidii na kutokubali  kupewa  mimba ambazo zitawakatisha 
masomo. 
Kwa upande wa vijana MNEC huyo 
aliwahimiza kuangalia  mstakabali wa maisha yao na kutumia muda wao 
kufanya kazi kwa bidii kwa kufanya hivyo watapata maendeleo kwani hizi 
sasa kuna baadhi ya vijana wakati wa  asubuhi wanaacha kwenda shamba 
kulima na kucheza Pool kwa kufanya hivyo ni vigumu kupata maendeleo. 
“Vijana wengine wanatumia  madawa 
ya kulevya na kuvuta sigara wanajua kwa kufanya hivyo ndiyo ujanja 
kitendo ambacho siyo ukweli,  bali unaharibu afya yako na kujirudisha 
nyuma kimaendeleo. Kama wewe kijana unahitaji kuwa na maisha bora ni 
lazima uachane na vitendo hivyo na kufanya kazi”, alisisitiza.  
Licha ya kufanya mkutano huo wa 
hadhara  Mama Kikwete pia alifanya vikao na wajumbe wa Halmashauri kuu 
ya CCM matawi ya Mbanja, Mabano na Mitwero Stendi na kuwataka wajumbe 
hao kuwapa vijana  nafasi za uongozi pale watakapojitokeza kugombea 
nafasi hizo.        
Pia aliwahimiza wajumbe hao 
wakiwemo vijana, wanawake na wanaume kujitokeza kugombea nafasi 
mbalimbali za uongozi katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika hapo 
mwakani ili kuwe na ushindani wa kutosha ndani ya chama.
Mama Kikwete yupo wilayani humo 
kwa ajili ya shughuli za kichama na katika mkutano wa hadhara aligawa 
kadi kwa  wanachama wapya 23 walijiunga na Chama Cha Mapinduzi.
No comments:
Post a Comment