Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Damian Lubuva
 akizunguza na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya tume ya 
uchaguzi jijini Dar es salaam wakati alipozungumzia maandalizi ya 
uboreshaji wa daftari la wapiga kura, kura ya maoni ya Katiba mpya na 
uchaguzi mkuu mwezi oktoba mwaka huu, kulia ni Mkurugenzi wa Tume ya 
Uchaguzi Bw. Julius Mh.Julius Mallaba.
Baadhi ya waadishi wa  habari wakiwa katika kutano huo.
…………………………………………………………………………………………………..
Ndugu Waandishi wa Habari, 
Mkurugenzi wa Uchaguzi,
Watendaji wa Tume, 
Mabibi na Mabwana.
Kwa niaba ya Tume ya Taifa ya 
Uchaguzi, napenda kuchukua fursa hii kuwakaribisheni kwa mara nyingine 
katika Mkutano huu. Nawashukuru kwamba, pamoja na majukumu mengi mliyo 
nayo, mmeweza kuupa umuhimu wa pekee mkutano wetu huu na kuhudhuria kwa 
wingi. Kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, nasema Ahsanteni na 
Karibuni sana.
Katika mkutano huu, Tume inalenga 
kutoa taarifa kuhusu tathmini ya utekelezaji wa zoezi la majaribio ya 
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (Pilot Registration) kwa 
mfumo wa Biometric Voters Registration (BVR) zoezi ambalo lilikamilika 
wiki iliyopita.
Ndugu Wanahabari,
Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria 
Kuandikisha Wapiga Kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na 
kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania, Wabunge na Madiwani. Kwa mujibu wa Sheria ya Kura 
ya Maoni, Daftari hili la Kudumu pia litatumika katika Kura ya Maoni 
kuhusu Katiba Inayopendekezwa.
Ndugu Wanahabari; mtakumbuka kuwa,
 Tume ya Taifa ya Uchaguzi imekuwa katika mchakato wa Maandalizi ya 
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa kutumia Teknolojia 
Mpya ya ”Biometric Voter Registration” (BVR) na mara kwa mara imekuwa 
ikiomba kukutana nanyi ili kuwapa taarifa kuhusu hatua mbalimbali ambazo
 Tume imekuwa ikizipitia.
Kwa kuwa Uboreshaji huu ulihusisha
 matumizi ya vifaa vya teknolojia ya kisasa, vifaa ambavyo vilikuwa 
havijawahi kutumika katika Uboreshaji nchini, tuliona si vyema kuagiza 
vifaa vingi kabla ya kuvifanyia majaribio. Zoezi la majaribio 
lilifanyika ili kuwa na uhakika kuwa vifaa hivi vya Biometric 
Registration vina uwezo wa kuandikisha Wapiga Kura katika mazingira ya 
nchi yetu. Zoezi hili liliangalia uwezo wa watendaji kutumia BVR katika 
uandikishaji na pia uwezo wa vyombo vyenyewe katika Software na Hardware
 kwenye uandikishaji. Katika zoezi hili tuliangalia changamoto 
zilizojitokeza ili kuzipatia ufumbuzi kabla ya kuanza Zoezi halisi la 
Uandikishaji wa nchi nzima.
Ndugu Wanahabari,
Kama nilivyosema, Tume inakutana nanyi ili kuwapa taarifa kuhusu
 Tathmini ya Utekelezaji wa zoezi la Majaribio la Uboreshaji wa Daftari 
la Kudumu la Wapiga Kura lililofanyika kwa siku saba (7) katika Kata za 
Bunju na Mbweni katika Jimbo la Kawe, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar 
es salaam; Kata za Ifakara, Kakingiuka, Ipangala, Mlabani na Viwanja 
Sitini katika Jimbo la Kilombero Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero, 
mkoani Morogoro; na Kata za Ikuba, Usevya na Kibaoni katika Jimbo la 
Katavi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele mkoani Katavi.
Tume kwa namna ya pekee, 
inawashukuru sana Waandishi wa Habari kwa kujitokeza na kufuatilia zoezi
 hili la majaribio ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. 
Waandishi wa Habari wamesaidia sana katika kuhamasisha Wananchi wa 
Majimbo husika kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la 
Kudumu la Wapiga Kura. Vilevile, Waandishi wa Habari wamesidia katika 
kutoa taarifa za maendeleo ya zoezi hili kitu ambacho kimesaidia 
kufanikisha zoezi hili.
Jumla ya BVR Kits 250 zilitumika 
katika Uboreshaji huo kwa mgawanyo ufuatao:- Halmashauri ya Kilombero 
BVR Kits 80, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele BVR Kits 80 na Halmashauri 
ya Manispaa ya Kinondoni BVR Kits 90. Vituo katika Kata zote vilikuwa 
vinafunguliwa saa 2.00 asubuhi na kufungwa saa 12.00 jioni.


No comments:
Post a Comment