NA MWANDISHI WETU
HATIMAYE Mkurugenzi wa Kampuni 
ya Msama Promotions ya jijini Dar es Salaam, Alex Msama, ameibuka na 
kutamka yeye si Meneja wa malkia wa nyimbo za injili nchini, Rose 
Muhando akisema amekuwa akishirikiana naye katika mazingira ya kawaida 
kama ilivyo kwa waimbaji wengine.
Kwa mujibu wa taarifa ya Msama 
kwa vyombo vya habari jana, yeye akiwa mlezi wa waimbaji wote wa muziki 
wa Injili, amekuwa akishirikana nao kwa karibu kutokana
na nafasi yake katika huduma hiyo ya uimbaji kwa kipindi cha miaka 15.
Msama, mtu aliyechangia kwa 
kiasi kikubwa maendeleo ya muziki wa injili nchini kutokana na kuandaa 
matukio ya muziki huo kama Tamasha la Pasaka, uzinduzi wa albamu na 
Tamasha la Krismas, alisema ameamua kutoa tamko hilo kutokana na 
malalamiko ya muda mrefu ambayo amekuwa akipata juu ya Rose.
“Nimekuwa nikipokea malalamiko 
mengi ikiwemo kutoka kwa viongozi wa kiroho wakiwemo wachungaji, kwamba 
pengine nimekuwa nikimzua Rose (Muhando) katika mtamasha wanayomualika 
na kushindwa kutokea.
“Lakini, naomba watumishi wa 
Mungu wanielewe katika hili, sipokei mialiko wala simzuii Rose. Mimi 
ninapokuwa na matamasha, nimekuwa nikimualika kama wafanyavyo wengine.
“Nimekuwa nikimlipa kiasi cha 
fedha anachotaka na hakuna zaidi, hivyo mimi sio Meneja wake,” alisema 
Msama katika taarifa hiyo na kuongeza:
“Agosti mwaka huu, kampuni yangu
 ilidhamini uzinduzi wa albamu yake ya Kamata Pindo la Yesu, haikuwa na 
maana kwamba ni Meneja wake.
“Nilimualika uzinduzi wa albamu 
ya Uko Hapa ya msanii John Lissu Oktoba mwaka huu, nilimlipa fedha, 
lakini hakutokea kama ambavyo amekuwa akifanya kwa wengine ambao 
wamekuwa wakilalamikia tabia hiyo,” alisema Msama.
“Pia wiki iliyopita nilikuwa na 
Tamasha la Krismasi tulikubaliana aje katika maonesho hayo, lakini 
hakutokea na tulishamlipa,” alisema Msama kwa masikitiko na kuongeza 
kuwa amemsamehe na anamuombea kwa Mungu aweze kubadilika.
Alieleza kuwa hana tatizo na 
mwimbaji huyo, wala hana ugomvi naye, lakini amekuwa akipata taabu 
kutoka kwa baadhi ya wachungaji pale Rose anapoalikwa halafu hatokei na 
inaonekana yeye ndiye amemzuia.
“Sijawahi kupokea mialiko kwa 
niaba ya Rose, kila kitu anafanya mwenyewe, hivyo ni vyema wadau 
wakafahamu hilo,” alisema Msama na kusema angekuwa mwepesi wa 
kulalamika, angeshafanya hivyo muda mrefu dhidi ya Rose.
Aidha, Msama amekana kuhusiana 
na madai ya Rose kutumia dawa za kulevya na kusisitiza kuwa hajawahi 
kumuona akijidunga kama ambavyo baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa 
vikiripoti na kuongeza kama ikiwa ni kweli, hilo pia ni suala binafsi.
“Baadhi ya vyombo vya habari 
vinaandika ni mjamzito, nafikiri pia hayo ni mambo yake binafsi na 
hakuna mtu mwenye haki au uhalali wa kuhoji hilo.Yule ni mtu mzima na 
mwenye kujielewa,” alisema Msama.
Rose ni mwimbaji mahiri wa 
muziki wa injili nchini aliyejipatia sifa ndani na nje ya ukanda wa 
Afrika Mashariki ambaye mwishoni mwa mwaka 2013, alisaini mkataba
wa kufanya kazi na kampuni ya muziki ya Sony ya Afrika Kusini.
Miongoni mwa albamu zilizompa 
umaarufu Rose kiasi cha kuwa alama ya mafanikio ya muziki wa injili 
nchini, ni ‘Uwe Macho,’ Nyota ya Ajabu (Zawadi ya Krismasi), Jipange 
Sawasawa, Kitimutimu, ‘Mungu Anacheka’ na Wololo na Kamata Pindo la Yesu
 aliyoachia hivyo karibuni.

No comments:
Post a Comment