![]()  | 
| Rais Jakaya Kikwete | 
Na: Said Mwishehe.
Kwa uwezo wa Mwenyezi  Mungu, tayari tumeingia mwaka 2015 pamoja na mataifa mengine duniani na kuuaga mwaka  2014.
Tuna kila sababu ya kumshukuru Mungu kwa kuendelea kutupa pumzi yake. Ametujaalia afya njema. Hili ni jambo la kushukuru.
Pia nitumie nafasi hii kutoa pole kwa ndugu, rafiki na jamii zetu ambao leo hii hatunao tena. Wametangulia mbele za haki.
Hiyo inatokana na mapenzi yake muumba wa mbingu na ardhi. Tuwaombee dua njema huko waliko.Mbele zao, nyuma zetu.
Wakati tumeingia  mwaka 2015, nitumie nafasi hii kuowambea wale wote wenye kusumbuliwa na magonjwa mbalimbali.
Imani yangu Mungu atawaponya na kuwarejesha kwenye afya njema na hatimaye kuendele na ujenzi wa taifa.
Wakati tumeingia  mwaka mpya, kuna mambo mengi ambayo yametokea kwenye mwaka huu wa 2014.
Yapo ambayo yametunufaisha kama taifa lakini wakati huo huo yapo ambayo yametufedhehesha.
Mwaka 2014 ulikuwa mwaka wa 
matukio mengi katika nyanja mbalimbali. Nikiri kuna mambo ya kujivunia 
na kuna mambo ya hovyo ambayo yametokea kwenye taifa hili ambalo 
linaendelea na juhudi za kusaka maendeleo yake.
Sote ni mashahidi Watanzania kwa 
nafasi zao mbalimbali wameendelea na ujenzi wa taifa leo. Wameendelea 
kudumisha umoja na mshikamano wao.
Wameendelea kuungana kupigania 
maisha yao. Ni watu ambao hawataki kukataa tamaa. Wanafanya kila juhudi 
kuhakikisha taifa linasonga mbele.
Nikiri kauli ambayo inaliumiza 
taifa hili ni kuendelea kuimba wimbo wa “Sisi maskini”. Wimbo ambao 
kwangu mimi unaniumiza kichwa. Sitaki hata kuusikia. Sitaki kuusikia 
kwasababu ni sehemu ya adui wetu wa maendeleo yetu.
Sisi maskini ni kauli ambayo 
imetukwamisha kwa miaka mingi sasa. Hata mwaka huu wa 2014, kauli ya 
sisi maskini imeturudisha nyuma.
Kujiita kila siku maskini ndio matokeo yake tunashinda kuishi maisha ya kuendelea kuomba misaada. Kisa tu nchi yetu eti maskini.
Kwangu naamini sisi si maskini ila
 huenda tunakosa mipango na usimamizi mzuri wa kufikia malengo yetu.hili
 ndilo tatizo ambalo linatusumbua kwa miaka mingi.
Mwaka 2015 ni mwaka wa kubadili 
mitazamo na fikra zetu. Tukitumia vema rasilimali zetu, tutapiga hatua. 
Kila kitu tunacho.tunachotakiwa ni mipango na usimamizi mzuri. Tuache 
akili za kuwa tegemezi kwa kila jambo.Inashangaza tunapokuwa na msitu 
mkubwa wa misitu kama ule wa Sao hili Iringa halafu kijiti cha 
kusafishia meno kinatoka China. Ama kweli!
Inasikitisha kuona imefika mahali 
eti kila kitu lazima kitoke nje. Kasumba hii inatokana na yale yale 
ambayo wengi yametutawala kwenye akili zetu kuwa lazima tuwe tegemezi.
Hatupaswi kuwa na akili hiyo kwa mwaka 2015. Ni mwaka wa kutafakari kama taifa nini tufanye ili tusonge mbele.
Kwa bahati mbaya tumekuwa na kundi
 kubwa ambalo linatumia muda mwingi kupiga soga vijiweni kwa ajenda 
ambazo hazina mashiko ya kimaendeleo. Ni rahisi kusikia watu wanajadili 
nani kavaa nini. Fulani analula nini?
Wanaojadili tunapigaje hatua kama 
taifa ni wa chache. Hata hao tunaowategemea kutupigania wamekuwa wa 
kuishi kwa matukio. Likija tukio hili wamo, likija lingine wamo.Mafundi 
wa kuongoa kuliko kutenda.
Inasikitisha sana.Tumeyaona hayo 
mwaka 2014.Si vizuri yakajirudia tena mwaka 2015. Kufanya kosa si kosa 
ila kurudia kosa, ndio kosa. Tusimamie kama nchi tuangalie maisha yetu. 
Tumetoka wapi na tunakwenda wapi.
Tukisoma vitabu vya historia 
tunaambia Tanzania na China zilianza harakati za kusaka maendeleo mwaka 
mmoja. Nenda leo China kaingalie.
Hatufanani nayo kwa namna yoyote 
ile.Watu tulianza nao kwenye harakati za kutafuta maendeleo, eti leo 
tunawapigia magoti kuwaomba msaada.
Wachina wameijenga nchi 
yao.Wameamua kusimama kidete kuhakikisha taifa lao linapiga hatua na 
kuwa lenye nguvu duniani.  Sishangai Marekani inapokwenda kuomba misaada
 ya kifedha China.
Kwetu sisi maendeleo yetu yamekuwa
 ya mwendo wa kinyonga. Wananchi wamekata tamaa ya maisha. Kila kukicha 
wanasema afadhali ya jana. Ndio maisha ambayo tumeamua kuishi.
Imefika mahali Wachina wameamua 
kuja nchini kwetu na kufanya kazi ambazo tumeshindwa kuzifanya. Nenda 
Kariakoo jijini Dar es Salaam, Wachina wanauza maua.Wanauza karanga.
Inasikitisha inapofika mahali hata
 karanga tunashindwa kuuza. Tunasibiri Wachina waje wauze. Halafu 
tumebaki kupiga kelele tu.Tumefika mahali pabaya.
Sifa ya taifa kupiga hatua za maendeleo linahitaji kuwa na siasa safi, utawala bora, ardhi na watu.
Nikiri tunaweza kuwa tumekosa 
siasa safi na uongozi bora lakini tuna ardhi ya kutosha na watu. Kwa 
bahati mbaya watu wapo lakini kasi ya maendeleo haiendani na idadi yetu.
Kitendo cha kukosa siasa safi 
imefika mahali, wanasiasa wengi wametugeuza kama vile kichwa na 
mwendawazimu. Wanatuongopea watakavyo.
Wanajua hatuna tunaloweza 
kulifanya. Hakika mwaka 2014, licha ya kufanya mambo ya maendeleo, yapo 
ambayo tunapaswa kujiepusha nayo mwaka 2015.
Msomaji wa safu hii, baada ya 
kutoa maelezo hayo ambayo kwangu mimi kwa siku ya leo ni kama utangulizi
 sasa nije kwenye ajenda yangu ya Jumatano ya leo.
Ajenda yenyewe ni hili sakata la 
Escrow.Sakata ambalo limekuwa gumzo kwenye kila kona ya nchi yetu. 
Limekuwa likizungumza na kila mtu. Kama hulizungumzi wewe basi 
analizungumza mwenzio.
Sakata la Escrow limetikisa nchi 
yetu kwa sehemu kubwa. Sote tunafahamu mjadala huo wa Escrow unatokana 
na utata wa fedha wa sh. bilioni 306 zilizopo kwenye akaunti ya Tegeta 
Escrow, wajanja kuamua kuzichukua.
Wanasiasa wa kada mbalimbali 
wamekuwa wakilizungumza hilo kwa kina. Wamekuwa wakipambana kwa hoja. 
Wamekuwa wakijadili na kuelezea umma kuhusu fedha hizo.
Nikiri mwaka 2014, mjadala wa 
Escrow kwangu mimi naona ulikuwa ni mjadala uliochokuwa sehemu kubwa ya 
mazungumzo kuliko mijadala mingine.
Ni kweli kulikuwa na mjadala 
kuhusu Katiba mpya lakini ujio wa sakata la Escrow umefunika kabisa 
mazungumzo ya Katiba inayopendekezwa.
Kwa kuwa hata wanasiasa wetu nao 
wanaishi kwa matukio. Wengi wao wameachana na ajenda ya Katiba mpya 
ambayo wananchi wanahitaji kuelimisha licha ya wao wenyewe kujisomea 
Katiba inayopendekezwa kabla ya kufanya uamuzi kwa kupiga kura ya ndio 
au hapa.
Leo hii ili mwanasiasa aonekane amezungumza jambo la maana basi anaamini akizungumzia Escrow ndio nyota ya siasa inasafishika.
Sina tatizo na wanasiasa ambao 
wamelizungumzia sakata hilo hadi hapa lilipofikia. Tunajua Bunge limetoa
 maazimio nane kwa Serikali.
Maazimio ambayo kwa sehemu kubwa 
Serikali ya Rais Jakaya Kikwete inatakiwa kuamua kwa kuchukua hatua 
dhidi ya wanaohusishwa na uchotaji fedha wa Escrow.
Ndio maana aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Frederick Werema ameamua kuachia ngazi.
Uamuzi huo unatokana na ukweli kwamba ushauri wake kisheria hakueleweka. Jaji Werema anasema amechafua hali ya hewa.
Pia tunafahamu Katibu Mkuu wa 
Wizara ya Nishati na Madini Eliakim Maswi naye amsimamishwa kazi ili 
kupisha uchunguzi. Kisa sakata hilo hilo la Escrow.
Nani ambaye hafamu kama aliyekuwa 
Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Profesa Anna Tibaijuka 
naye ametemwa kwenye baraza la mawaziri.
Kilichomuondoa ni kupokea fedha za Escrow.Prof. Tibajuka aliwekewa kwenye akaunti yake binafsi sh. bilioni 1.6.
Wakati mjadala huo unaendelea, 
hakuna mwanasiasa ambaye ameweza kupata ujasiri wa kuliambia taifa fedha
 hizo ni za umma au si za umma. Nani mwenye fedha hizo?.
Ujasiri ambao wanasiasa wetu walio
 wengi wanao hadi sasa ni kwamba sh. bilioni 306 za Escrow ni za umma. 
Wamesema hivyo wakiwa bungeni na wanaendelea kusema hivyo nje ya Bunge.
Kwangu mimi na hata kwa Watanzania
 wengine, nimefurahishwa na hotuba ya Rais Kikwete.Hotuba ambayo aliitoa
 Desemba 22 mwaka huu. Alikuwa anazungumza na wazee wa mkoa wa Dar es 
Salaam.
Kama kiongozi wa nchi ameonesha kulifahamu vema suala hilo. Akatumia nafasi hiyo kuelezea historia nzima ya sakata la Escrow.
Akaeleza namna ambavyo Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na IPTL walivyokuwa wanalipa.
Pia, akaeleza namna ambavyo 
akaunti ya Tegeta Escrow iliovyofunguliwa hadi hatua ya IPTL na wanahisa
 wenzake kuuziana hisa na kisha kufunga akaunti ya Tegeta Escrow na 
kuchukua fedha zilizomo.
Rais Kikwete baada ya kutoa 
maelezo mengi ya kueleweka pengine kuliko yale yaliyokuwa yanatolewa na 
wanasiasa walio wengi akatumia nafasi hiyo kuwahakikishia Watanzania 
kuwa fedha hizo ni za IPTL.
Rais Kikwete katika hotuba yake 
alisema”Fedha hizo ni za IPTL maana ni malipo ambayo yalikuwa yanalipwa 
kutoka Tanesco ambazo ni tozo la uwekezaji, lakini toafuti yake fedha 
zilikuwa zinawekwa kwenye akaunti maalumu”.
Kimsingi hotuba ya rais imejibu 
swali la msingi ambalo Watanzania wengi walikosa kulisikia.Pamoja na 
kusema fedha hizo ni za IPTL bado akauthibitisha umma kuna kodi ya 
Serikali ndani yake.
Hivyo tunapoumaliza mwaka 2014, 
naamini rais amesema kile ambacho wengi tulipaswa kukisikia.Akasisitiza 
uchunguzi ufanyike na kisha sheria ichukue mkondo wake.
Akaagiza mamlaka zinazohusika na uchunguzi zitakapokamlisha taarifa , yeye atakuwa na uamuzi wa kufanya.
Baada ya kulifafanua kwa kina 
suala hilo, rais akatumia nafasi hiyo kuweka wazi Waziri wa Nishati na 
Madini Profesa Sospeter Muhongo amemuweka kiporo.
Bwana we! kauli hiyo ya Prof.Muhongo kuwekwa kiporo imeamsha hasira za wanasiasa hasa za wapinzani.
Wametoa matamko ya kumtaka Rais Kikwete kumuwajibisha Prof.Muhongo kwa kumuondoa kwenye nafasi hiyo.
Wengine wametangaza kufanya maandamano nchi nzima.Najiuliza sababu za  msingi za kufanya maandamano hayo.
Najiuliza hivi wanaotaka 
Prof.Muhongo aondolewe kwenye nafasi hiyo ni kweli wanashinikiza kwa 
maslahi ya Taifa au kwa maslahi binafsi.
Hapa kuna siri kubwa, ambayo wenye
 kumshinikiza rais amuondoe Prof.Muhongo kwenye nafasi ya uwaziri 
wanaijua. Nani ambaye hajui kazi ambayo imefanywa na Prof.Muhongo kwenye
 wizara hiyo.
Amefanya mambo makubwa kwa maslahi
 ya nchi.Waziri Muhongo kwa usimamizi wake mzuri umeme umekwenda kwenye 
vijiji mbalimbali vya nchi yetu.
Nimezunguka wilaya za nchi hii 129 hadi sasa.Naiona kazi ambayo Prof.Muhongo ameifanya katika nishati ya umeme.
Nani ambaye hajui umuhimu wa 
nishati ya umeme kwa wananchi. Misimamo yake katika wizara hiyo 
imefanikisha ujenzi wa bomba la gesi.Angekuwa Waziri legelege , bomba la
 gesi kutoka Mtwara kuja(kwenda) Dar es Salaam lisingejengwa.
Alijua anasimamia maslahi ya 
taifa.Pia najua kwenye eneo la gesi amekasirisha wengi.Wapo ambao 
hawataki hata kumsikia.Leo si wakati wake kuzungumzia hilo.
Wanasiasa wanataka rais amuondoe 
Prof.Muhongo, hivi waziri mwingine ambaye atakwenda kwenye wizara hiyo 
na kukaa kwa miezi nane iliyobaki ya utawala wa rais Kikwete anakwenda 
kufanya jambo gani kubwa.
Kuna dhambi gani Waziri Muhongo akiachwa amalizie muda ambao Rais Kikwete ameubakisha.
Kwa kuwa tunaingia mwaka 2015, ni 
bora niseme ukweli maana utaniweka huru.Naamini sioni sababu ya 
kumuondoa Waziri Muhongo Wizara ya Nishati na Madini.
Tangu amekuwa Waziri wa Nishati na Madini Waziri Muhongo amefanya kazi kubwa na nzuri.Hata hao ambao leo wanamuandama wanajua.
Nikiri najua, haya ninayoeleza kuna watu nawakera lakini ni bora niwe huru kwenye kile ninachoamini.
Kauli ya Mwishehe, nakushauri Rais
 wangu, Rais Jakaya Kikwete , nakuomba umuache Waziri Muhongo amalizie 
kazi anayoifanya kwenye wizara hiyo.Binafsi sioni mahali ambapo Waziri 
Muhongo amechukua fedha za Escrow.
Sioni mahali ambapo Waziri Muhongo ameshauri fedha zitoke. Waziri Muhongo msimamo wake unajulikana wazi kuhusu fedha hizo.
Kwa bahati mbaya wanasiasa wetu 
wameng’ang’ania tu kumtaka rais amuondoe Muhongo badala ya kutoa suluhu 
ya nini kifanyike ili hayo ambayo yanatokea na kusababisha taifa 
kushindwa kuchukua kodi yake yasijirudie.
Wanasiasa wanashindana kuita vyombo vya habari kumshinikiza rais kumuondoa Waziri Muhongo.
Naamini na ndio ukweli wanafanya 
hivyo si kwasababu ya maslahi ya taifa , bali wanafanya hivyo kwa msuko 
mwingine. Ipo siku nitausema.Kwenye hili nitasimamia ukweli.
Kwenye siasa za Tanzania kuna 
mambo huwa yanakera sana. Moja ya mambo yanayokera ni pale mtu 
anaposimama kujifanya anapigania maslahi ya taifa kumbe, kichwani kwake 
anawaza tofauti.
Kuna wakati huwa najiuliza kwanini
 , wanashinikiza Prof. Muhongo aondolewe. Nawaza weee , lakini napata 
majibu tofauti tofauti. Moja ya jibu ambalo huwa nalipata ni kwamba 
wanaogombea urais nao wana yao kwenye hilo.
Tena si wa CCM tu, bali hata wa upinzani. Wanaona sakata la Escrow ni karata ya mwisho ya kufanikisha malengo yao.
Wengine wanaamini kupitia sakata hilo itakuwa njia rahisi ya kuiangusha Serikali ya Rais Kikwete bungeni.
Hivyo, kila mmoja analiangalia 
kivyake na si kweli wote wanaopigania hilo ni kwa ajili ya maslahi ya 
taifa. Ingekuwa ni maslahi ya taifa wangetuambia kwenye sh. bilioni 306 
za Escrow za umma ziko sh. ngapi?
Nimalizie kwa kueleza tunaingia 
mwaka 2015, tudumishe upendo, umoja na mshikamano wetu. Najua wapo ambao
 watakaosema nimetumwa. Sijatumwa. Sitajali.
Kubwa zaidi kila Mtanzania ana 
haki ya kutoa maoni yake kwa kile anachokiamini anaweza kuchangia alau 
kidogo hasa kwa kuzingatia mwaka 2014 umebakisha saa chache tu wa uhai 
wake.
Karibu mwaka 2015, nitumie nafasi 
hii kuwataka mafanikio mema kwenye mwaka wa uchaguzi wanasiasa wote. 
Mwaka ambao kila anayetaka kugombea udiwani, ubunge au urais anarudi 
kuomba kura kwetu.
Nawaheshimu wanasiasa wote na wa vyama vyote. Kwenye ukweli nipo pamoja nanyi na kwenye uongo nitakuwa kando yenu.
Tuwasiliane 0713833822

No comments:
Post a Comment