Kutua Februari, apania kuzalisha akina Mayweather kibao nchini 
NDONDI ni miongoni mwa michezo maarufu mno hapa Tanzania na duniani kwa ujumla.
Wapo wanamichezo waliojipatia heshima kubwa duniani kutokana na kufanikiwa kupitia mchezo wa ndondi.
Miongoni mwa wanamichezo hao ni nguli Mohammed Ali, Mike ‘Iron’ Tyson, Evender Holyfield, Floyd Mayweather, Manny Pacquiao na wengineo wengi.
Kwa hapa nchini, wapo 
mabondia waliojitengenezea majina wakiwamo Emmanuel Mlundwa, Habibu 
Kinyogoli ‘Masta’ Michael Yombayomba, Stanley Mabesi ‘Ninja’ Rashid 
Matumla, Ibrahimu Class ‘King Class Mawe’  na wengineo wengi. 
Lakini ikumbukwe kuwa ndondi 
ndio mchezo uliotoa mwanamichezo anayelipwa zaidi duniani kwa sasa 
ambaye si mwingine bali ni Mayweather, akifuatiwa na mwanasoka raia wa 
Ureno anayekipiga katika klabu ya Real Madrid ya Hispania, Cristiano 
Ronaldo.
Anayeshika nafasi ya tatu ni 
mchezaji wa mpira wa kikapu LeBron James, wakati mwanasoka anayechezea 
Barcelona ya Hispania, Muargentina Lionel Messi akishika nafasi ya nne, 
huku wa tano akiwa ni mkali wa mpira wa kikapu, Kobe Bryant.
Pamoja na mafanikio hayo 
katika ndondi, Tanzania imeonekana kuzidi kulala usingizi wa pono katika
 suala zima la kuvumbua na kuendeleza vipaji vya mchezo huo kama sehemu 
ya kutatua tatizo sugu la ajira linaloitesa nchi yetu kwa sasa.
Unapopita huko mitaani, 
unaweza kukutana na vijana wadogo wakiwa wanafanya mazoezi ya ngumi kwa 
kutumia vifaa visivyo rasmi ambavyo mwisho wa siku, huishia kuwadumaza 
badala ya kuwajenga kama walivyotarajiwa.
Hali hiyo imetokana na 
kukosekana kwa vifaa vya kujifunzia mchezo huo, zikiwamo kumbi na hata 
wataalam wa kuwapa ujuzi wa kuwawezesha kufikia mafanikioi ya akina 
Mayweather.
Ni kwa kufahamu hilo, wapo 
wadau wa ndondi ambao wamekuwa wakijitoa kusaidia vipaji vya ndondi hapa
 nchini, miongoni mwao akiwa ni Kocha wa Kimataifa wa Ndondi nchini, 
Rajabu Mhamila ‘Super D’.
Bondia huyu wa zamani, 
ameshawahi kufanya jitihada kadha wa kadha kuendeleza ndondi hapa 
nchini, ikiwamo kutoa mafunzo kwa vijana chini ya klabu yake ya Ashanti 
Boxing Club na kupitia DVD zake zenye mapambano makali yaliyowahi 
kufanyika hapa nchini na duniani kwa ujumla, yakiwahusisha mabondia 
nyota.
Katika kuonyesha jinsi 
anavyoguswa na ndondi, Februari mwaka huu Super D atakuwa na ugeni 
mkubwa wa bondia Mtanzania anayefanya kazi zake nchini Deer Park, Victoria, Australia, Omari Kimweri ambaye anatua nchini kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wanamasumbwi wa Tanzania.
Akizungumza Dar es salaam 
jana, Super D anasema kuwa ujio wa Kimweri ni fursa nyingine adimu kwa 
mabondia wa Tanzania katika kuona ni vipi wanaweza kutimiza ndoto zao za
 kutoka kimaisha kupitia mchezo huo.
Anasema kuwa Kimweri atatua 
akiwa na vifaa mbalimbali vya masumbwi ambapo pia atatoa mafunzo na 
mbinu mpya zinazotumiwa na mabondia wa nje kwa mabondia pamoja na 
kushuhudia mapambano kadhaa yatakayofanyika kwa kipindi atakachokuwapo 
hapa nchini.
“Kimweri anakuja akiwa na 
msafara wa watu kadhaa, akiwamo mwanasoka wa kike, Melanie Gines ambaye 
ni raia wa Hispania. Akiwa hapa nchini, Melanie atapata fursa ya 
kukutana na wanasoka wa kike wa hapa , kwani amechezea timu nyingi za 
Ulaya,  Hispania,” anasema Super D.
Anasema kuwa ujio wa Kimweri 
umewezeshwa kwa kiasi kikubwa na promota wake, Brian Amatruda ambaye ni 
miongoni mwa mapromota maarufu nchini kwao Australia, akiwa amekubali 
kutoa baadhi ya vifaa vya kisasa kutoka Hispania na Marekani kwa ajili 
ya ziara hiyo.
Super D anasema kuwa Kimweri 
ambaye ni bingwa wa WBO, atatua nchini akiwa na mikanda yake yote 
aliyowahi kutwaa, ukiwamo wa ubingwa wa Australia, lengo likiwa ni 
kuwahamasisha vijana wa kitanzania kujikita zaidi katika ndondi.
“Nimezungumza na Kimweri na 
ameonyesha kuwa na uchungu wa kuwainua mabondia wa hapa nchini ili 
waweze kutimiza ndoto zao na anafanya hivyo chini ya mradi wake wa 
‘Kimweri Project’ na atakuwa hapa nchini kwa wiki moja,” anasema.
Anasema kuwa ujio wa bondia 
huyo uliochagizwa na Super D Boxing Coach and Promotion, umelenga 
kuwahamasiaha mabondia kucheza mara kwa mara ili kupandisha viwango vyao
 kwani hiyo ndio siri ya mafanikio ya wanamasumbwi wengi duniani.
Mbali ya mafunzo kutoka 
kwa Kimweri, pia katika ziara zake zote sehemu mbalimbali nchini, 
kutakuwa na uuzwaji wa DVD za Super D zenye lengo la kutoa mafunzo 
kupitia mapambano ya mabondia maarufu duniani, akiwamo Floyd 
Mayweather,Manny Paquaio, Mohamerd Alli, na wa hapa nchini kama Mbwana 
Matumla, FrancisMiyeyusho,Ibrahimu Class’ King Class Mawe’ ambaye ni bingwa 
wa WPBF Africa na wengineo.


No comments:
Post a Comment