Waziri wa Nishati na Madini 
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akitoa maelekezo kwa mtaalamu kutoka 
kampuni ya Symbion iliyopewa kazi ya kujenga miundombinu ya umeme katika
 kijiji cha Nyamikoma kilichopo wilayani Busega Bw. Steve Thomson 
(kushoto)
………………………………………………………………………………………….
• Vijiji 1,500 kupatiwa umeme 
Na Greyson Mwase, Busega
Imeelezwa kuwa ifikapo mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu mradi 
wa usambazaji wa umeme vijijini unaotekelezwa na Wakala wa Nishati 
Vijijini (REA) Awamu ya Pili kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Nchini
 (Tanesco) unatarajiwa kukamilika, ikiwa ni pamoja na kuvipatia umeme 
vijiji 1,500.
Hayo yalielezwa na Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter 
Muhongo kwa nyakati tofauti alipofanya ziara katika vijiji vya Ihale, 
Bukombe, Nyamikoma, Bushigwamala, Mwamagigisi, Mkula vilivyopo katika 
wilaya ya Busega mkoani Simiyu.
Profesa Muhongo anafanya ziara katika mikoa ya Simiyu, Tabora na
 Shinyanga lengo likiwa ni kukagua miradi ya umeme vijijini pamoja na 
kuzungumza na wananchi.
Alisema kuwa wakandarasi wote nchini wanaotekeleza miradi ya 
umeme vijijini inayotekelezwa na REA awamu ya pili kwa kushirikiana na 
Tanesco wanatarajiwa kukamilisha na kukabidhi miradi yao mwishoni mwa 
mwezi Juni ambapo itakuwa ni mwisho wa utekelezaji wa miradi hiyo.
Profesa Muhongo alisema kuwa mara baada ya kumalizika kwa mradi 
wa umeme vijijini awamu ya pili, mapema Julai Serikali inatarajia 
kuingia katika awamu ya tatu ya utekelezaji wa usambazaji wa nishati ya 
umeme vijijini lengo likiwa ni mwendelezo wa kuboresha maisha ya 
wananchi hasa waishio vijijini na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa 
nchi.
Alisema kuwa, kwa kutambua umuhimu wa nishati ya umeme katika 
ukuaji wa uchumi wa nchi, Serikali imeelekeza nguvu zake zote katika 
kusambaza umeme husasan vijijini kwa lengo la kuhakikisha kuwa ifikapo 
mwaka 2025 asilimia 75 ya watanzania wanapata umeme wa uhakika na hivyo 
nchi kutoka katika kundi la nchi masikini duniani na kuwa nchi yenye 
kipato cha kati.
Akizungumzia gharama ya uunganishaji wa umeme nchini kwa 
wananchi waliopo chini ya mradi wa usambazaji wa umeme vijijini 
unaotekelezwa na REA Profesa Muhongo alisema kuwa ni shilingi 27,000 
ambayo ni VAT peke yake na kuwataka wananchi walio chini ya mradi huo 
kuchangamkia fursa ili waweze kufaidi umeme kwa gharama ambayo ni ya 
chini mno.
Alisema kuwa lengo ni kuhakikisha kuwa wananchi hasa waishio 
vijijini wanamudu gharama ya kuunganishiwa umeme na kujikwamua kiuchumi.
Alisisitiza kuwa kwa wananchi waliochelewa kutuma maombi yao ili
 kuunganishiwa umeme chini ya mradi wa REA awamu ya pili, wasubiri awamu
 zingine zinazofuata, au walipe shilingi 177,000 kwa Tanesco na 
kuunganishiwa umeme muda wowote watakaohitaji
“ Kwa wale wanaohitaji kuunganishiwa umeme muda wowote na 
Tanesco nje ya kutegemea miradi ya umeme vijijini inayotekelezwa na REA 
kwa awamu watatakiwa kulipa shilingi `177,00 bila nguzo na fedha hizi 
zinaweza kulipwa kwa awamu, ‘’ alisema Profesa Muhongo.
Aliendelea kufafanua kuwa awali wananchi walitakiwa kulipa 
shilingi 467,000 lakini Serikali ikaamua kushusha bei hadi kufikia 
shilingi 177,000 ili kuwawezesha wananchi wote kuunganishiwa umeme.
Akizungumzia utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini awamu ya 
tatu, Profesa Muhongo alieleza kuwa maombi yatachukuliwa nchi nzima kwa 
vijiji vilivyokosa umeme katika awamu ya pili, na baada ya hapo mradi 
utaanza kutekelezwa kwa vijiji vichache kwa kila mkoa, kwa awamu tofauti
 lengo likiwa ni kuhakikisha panakuwepo na usawa katika kunufaika na 
miradi ya umeme vijijini.
Akizungumzia gharama ya umeme nchini Profesa Muhongo alisema 
kuwa gharama za umeme zinatarajiwa kushuka mara baada ya Tanesco kuanza 
kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia
Alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa bomba la gesi kutoka 
Mtwara hadi jijini Dar es Salaam lenye urefu wa kilometa 542, na kuanza 
kuzalisha gesi, kutapelekea kushuka kwa gharama za umeme kwani umeme 
unaozalishwa na gesi ni nafuu kuliko umeme unaozalishwa kutokana na 
mafuta mazito unaotumika sasa.
Aliongeza kuwa mbali na bomba la gesi kuchangia kushuka kwa 
gharama za umeme na kupatikana kwa umeme wa uhakika, gesi hiyo 
itapelekea kuongezeka kwa fursa nchini za uwekezaji nchini husan viwanda
 vya mbolea, sementi na kuongezeka kwa ajira
Alisema kuwa gesi hiyo itatumika katika magari na kupikia majumbani hivyo kupunguza uharibifu wa mazingira.
Akielezea mikakati mingine ya serikali katika kuhakikisha kuwa 
umeme unaopatikana unakuwa ni wa uhakika, Profesa Muhongo alisema kuwa 
serikali imebuni vyanzo vingine ya nishati ya umeme kama vile makaa ya 
mawe, jua, jotoardhi, bayogesi na upepo huku ikikaribisha wawekezaji 
kutoka ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha kuwa nishati ya umeme 
inakuwa ni ya uhakika.

No comments:
Post a Comment