Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya 
Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) itakutana Zanzibar Januari 13, kwa 
kikao cha kawaida cha siku moja chini ya Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya 
Mrisho Kikwete. 
Kikao hicho cha Kamati Kuu 
kitatanguliwa na kikao cha Sekretarieti ya Halmashauri Kuu 
kitakachofanyika Januari 10, jijini Dar es Salaam.
Wakati huo huo CCM inalaani vikali
 vurugu zilizofanywa na wafuasi wa Chadema na CUF kwa viongozi wetu wa 
serikali za mitaa katika maeneo kadhaa nchini ikiwemo mikoa ya Mwanza, 
Dar es Salaam na Mbeya.
Vurugu hizo zilizosababisha baadhi
 ya viongozi wetu kujeruhiwa zimetokea katika mkoa wa Mwanza ambapo 
Ndugu Christopher Mgeta kutoka Mtaa wa Ibungilo na Ndugu Pascal Charles 
wa Mtaa wa Kitangiri A katika wilaya ya Ilemela walivamiwa na kupigwa 
wakati wa kuwaapisha.
Katika mkoa wa Dar es Salaam, 
Ndugu Sultan Jeta wa mtaa wa Ukwamani katika jimbo la Kawe alifanyiwa 
fujo na wafuasi hao na Katika Mtaa wa Msisiri A kata ya Mwananyamala 
katika jimbo la Kinondoni Ndugu Juma Mbena alipigwa na kuvunjwa mkono.
Katika Manispaa ya Ilala, wafuasi 
hao wa vyama vya upinzani walifanya vurugu wakati wa kuwaapisha viongozi
 hao wa serikali za mitaa wilayani humo na kusababisha zoezi hilo 
kuahirishwa.
Mkoani Mbeya vurugu za aina hiyo 
zimetokea katika wilaya za Kyela na Rungwe ambapo wilayani Kyela zoezi 
la kuapisha viongozi wa serikali za mitaa lilishindika na kuahirishwa 
kutokana na vurugu za kurushiwa mawe zilizofanywa na wafuasi wa Chadema 
walioletwa kutoka katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo.
Katika kijiji cha Ilundo wilayani 
Rungwe wafuasi hao wa Chadema waliwapiga mawe viongozi na wanachama wa 
CCM na baadae kufyeka mashamba yao ya migomba na kusababisha vijana sita
 kujeruhiwa na kulazwa katika hospitali ya wilaya ya Rungwe kwa sababu 
ya hasira za kushindwa uchaguzi.
Vurugu hizi ni mwendelezo wa tabia
 na mazoea ya vyama vya upinzani nchini kutoheshimu na kufuata sheria na
 taratibu za nchi.  Tabia hizi si za kiungwana na ni uthibitisho wa 
kuharibikiwa na kufa kwa vyama vya upinzani nchini.  Mara zote wamekuwa 
wakikataliwa na wananchi kwa kura, wao hukataa uamuzi huo wa wananchi 
kwa kufanya fujo na vitimbi.  Asiye kubali kushindwa si mshindani.  
Vurugu hizi sasa inatosha.

No comments:
Post a Comment