Mbunge wa Maswa Magharibi John Magale Shibuda (kushoto) 
akitafsiri hotuba ya shukrani iliyotolewa kwa lugha ya kisukuma na mmoja
 wa wakazi wa kijiji cha Shishiyu mbele ya Waziri wa Nishati na Madini 
Profesa Sospeter Muhongo kabla ya kuzinduliwa rasmi kwa mradi huo.
……………………………………………………………………………………………….
Na Greyson Mwase, Simiyu
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo amesema 
kuwa serikali imetumia shilingi bilioni 25.7 kwa ajili ya kusambaza 
umeme katika vijiji 170 vilivyopo ndani ya mkoa wa Simiyu
Alisema hayo alipokuwa akizindua mradi wa umeme vijijini 
uliotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Awamu ya Pili 
iliyoanza mwaka 2013 inayotarajiwa kumalizika mwishoni mwa mwezi Juni 
mwaka huu.
Akifafanua idadi ya vijiji vilivyonufaika na REA Awamu ya Pili 
Profesa Muhongo alieleza kuwa katika Wilaya ya Bariadi vijiji 45 
vilipatiwa umeme, katika Wilaya ya Maswa vijiji 82 vilipatiwa umeme, 
katika Wilaya ya Busega vijiji 19 vilipatiwa umeme, katika Wilaya ya 
Itilima vijiji 7 vilipatiwa umeme na katika Wilaya ya Meatu vijiji 17 
vilipatiwa umeme.
Akizungumzia hali ya usambazaji wa umeme vijijini nchini Profesa
 Muhongo alisema kuwa vijiji 3734 kati ya vijiji 15,180 ambayo ni 
asilimia 24.6 vina umeme na kuongeza kuwa mara baada ya kukamilika kwa 
mradi wa REA Awamu ya Pili mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu kwa 
kuongeza vijiji 1500 idadi ya vijiji vyenye umeme itaongezeka na kufikia
 5234 ambayo ni sawa na asilimia 34.5.
Akizungumzia gharama za uunganishaji wa umeme vijijini Profesa 
Muhongo alisema kuwa katika REA Awamu ya Kwanza gharama zilishushwa 
kutoka shilingi 467,000 hadi shilingi 177,000.
Alieleza kuwa katika Awamu ya Pili ya REA Serikali ilishusha bei
 ya uunganishaji wa umeme bila nguzo kutoka shilingi 177,000 hadi 
shilingi 27,000 ili kuwawezesha wananchi hasa waishio vijijini kuweza 
kumudu gharama za uunganishaji wa umeme na kuwa na maisha bora.
Alisema mara baada ya kukamilika kwa mradi wa umeme vijijini wa 
REA Awamu ya Pili wananchi ambao wanahitaji umeme nje ya mradi wa REA 
watalipia shilingi 177,000 tu na iwapo wataona bado wanahitaji umeme 
chini ya mradi wa REA basi watatakiwa kusubiri awamu nyingine.
“ Huduma ya umeme haina itikadi ya kisiasa, kidini ni haki ya 
kila mwananchi kupata umeme wa uhakika, na sisi kama Serikali 
tutahakikisha kuwa tunatumia vyanzo vyote vya nishati ili kuwa na umeme 
wa kutosheleza nchi nzima na kupelekea nchi kuondokana na umasikini.” 
Alisema Profesa Muhongo.
Aliongeza kuwa katika utekelezaji wa mradi wa usambazaji wa 
umeme vijijini kupitia REA Awamu ya Tatu vijiji vyote nchini vitapatiwa 
umeme kwa uwiano ulio sawa na kwa awamu tofauti ili kuhakikisha kila 
wilaya na kijiji kinanufaika na mradi huo.
Alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa inatokomeza 
umasikini kwa watanzania kwa kuwapatia nishati ya umeme kwani ni mhimili
 mkubwa wa uchumi wa nchi.
“Hakuna nchi yeyote duniani iliyoendelea bila kuwa na umeme, 
tunahitaji umeme kwenye viwanda vyetu, maabara mashuleni, vituo vya afya
 na katika shughuli nyingine nyingi muhimu za kiuchumi,”alisisitiza 
Profesa Muhongo
Wakati huo huo Mbunge wa Bariadi Magharibi John Magale Shibuda 
akizungumza kupitia hotuba yake kwenye uzinduzi wa mradi huo alitumia 
fursa hiyo kumpongeza Waziri wa Nishati na Madini Profesa Muhongo kama 
kiongozi mchapakazi, mzalendo na mwenye kuitakia mema nchi.
Alisema pamoja na Wizara ya Nishati na Madini kukumbana na 
changamoto mbalimbali lakini Waziri huyo amekuwa imara katika kutekeleza
 majukumu yake kwa kusimamia vyema sekta ya nishati na madini ambayo ina
 mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi.
“Natumaini ninyi mtakuwa mashahidi wangu, tukiweka tofauti za 
itikadi za kisiasa, Profesa Muhongo ni mtendaji na ushahidi ni huu 
usambazaji wa umeme vijijini kwa kasi ya ajabu, kwani kupitia REA Awamu 
ya Pili vijiji 170 katika mkoa wa Simiyu vimeunganishwa na umeme,’’ 
alisisitiza Shibuda
No comments:
Post a Comment