Na JOHN DOTTO  Mwanza
WAZIRI wa Ujenzi Dk. John 
Magufuli ameagiza kufungwa kwa mfumo mpya wa kielektroniki katika vivuko
 vyote nchini ili kukabiana na wajanja wachache wanahujumu mapato katika
 vivuko hivyo.
Mbali ya hilo, ameagiza kufanywa
 kwa utaratibu utakaowezesha huduma katika vivuko zinatolewa kwa saa 24 
ili kukidhi mahitaji ya wananchi.
Dk. Magufuli alitoa maagizo hayo
 jana katika uzinduzi wa mfumo mpya wa kielektroniki katika kivuko cha 
Kigongo -busisi mkoani hapa uliowekwa na Kampuni ya Africom Tanzania.
“Tulianze pale Kigamboni na 
tukaona mafanikio, tulipokuja hapa (Kigongo) tukaboresha na mafanikio 
yameonekana kwa kiasi kikubwa. Vivuko vyote sasa vifungwe mfumo mpya wa 
kielektroniki…vivuko vyote nchini,” aliagiza Magufuli.
Alisema mfumo huo una faida 
kubwa ikiwemo kudhibiti upotevu wa mapato ambapo katika kivuko cha 
kigongo – Busisi alisema mapato yameongezeka kwa takribani asilimia 40 
baada ya kufungwa kwa mfumo huo.
Hata hivyo, Dk. Magufuli 
alikataa kutaja ni kwa shilingi ngapi mapato hayo yameongezeka kwa hofu 
kuwa watu wenye dhmira mbaya wakisikia wanaweza kwenda na kufanya 
uhalifu.
Pia, aliagiza Kivuko kwa Kigamboni nacho kiboreshwe mfumo wake kama ilivyokuwa kwa Kigongo – Busisi. 
Waziri huyo wa Ujenzi, alisema 
kutokana na mafanikio yanayopatikana katika kudhibiti upotevu wa mapato 
na kurahisisha huduma kwa wananchi, wafanyakazi husika kwa maana ya wale
 wa TEMESA maslahi yao yanapaswa kuangaliwa upya na kuboreshwa.
“Kama mapato ni mazuri, 
wafanyakazi nao walipwe vizuri, wasikae kimasikini kwani wanapaswa kuona
 mwaka 2015 ni ukombozi katika maisha yao.
Alisema serikali chini ya 
uongozi wa Rais Jakaya Kikwete imefanikiwa kujenga madaraja yote makubwa
 nchini ambapo kwa sasa kuna madaraja 4880 nchini na kuwa wakati inapata
 uhuru kulikuwa na madaraja mawili ambayo yalikuwa ya kuvutwa.
Mfumo wa kielektroniki katika 
vivuko vya Kigamboni na Kigongo Busisi ulifungwa na Kampuni ya Africom 
Tanzania ambaye Mkurugenzi Mtendaji wake Juma Rajabu alisema 
watahakikisha wanafunga mifumo ambayo itadhibiti upotevu wa mapato na 
kurahisisha huduma kwa wananchi ambao ndiyo watumiaji.

No comments:
Post a Comment