………………………………………………………….
WENYEVITI wa Vijiji, Vitongoji na 
Wajumbe wa Serikali za Vijiji wa Tarafa ya Moipo, Wilayani Simanjiro 
Mkoani Manyara, wametakiwa kuwaongoza wananchi bila kuwa na upendeleo, 
huba, chuki, hofu, uoga na kuficha siri za ofisi.
Wito huo umetolewa juzi na Hakimu 
wa Mahakama ya Mwanzo Mirerani, Gofrey Haule, wakati akiwaapisha 
wenyeviti wa vijiji, vitongoji na wajumbe wa Serikali za vijiji wa 
Tarafa hiyo ili watunze siri za ofisi.
Hakimu Haule alisema ili jamii 
iweze kuwaamini viongozi hao wanatakiwa kutokwenda kinyume na maadili ya
 kazi, kutokwenda kinyume na utaratibu wao na bila kufanya kufanya 
upendeleo wowote kwa watu watakaowaongoza.
“Uongozi ni kama kuongoza njia 
hivyo mkijenga mahusiano mema kati yenu na jamii mtaweza kutekeleza 
majukumu yenu bila kuwa na shaka ila msikiuke viapo vyenu kwani siyo 
jambo jema mbele ya wananchi,” alisema Hakimu Haule.
Hata hivyo, baadhi ya viongozi 
walioapishwa waliahidi kuwa watawatumikia wananchi bila kuwa ubaguzi 
wowote ule, kwani hivi sasa suala la siasa lilishapita na kilichobaki ni
 kupambana na maendeleo ya jamii peke yake.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa 
Kiongoji cha Tenki la Maji, Rajab Msuya alisema wananchi wakishirikiana 
naye bega kwa bega wataweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo kupitia 
fikra mpya na uongozi mpya uliopo eneo hilo.
Naye, Mwenyekiti wa kitongoji cha 
Kilimanjaro, Elizabeth Kisamo (Chadema) alisema atawatumikia wananchi 
wote wa kitongoji chake bila ubaguzi wa itikadi, dini, kabila au jinsia,
 kwani hivi sasa yeye ni kiongozi wa watu wote.
“Kwa sababu wazee ndiyo waliniomba
 niongoze hiki kijiji, nitajitahidi kuongoza kwa nguvu zangu zote ila 
busara zao bado ninazihitaji na waendelee kunipa ushirikiano wao,” 
alisema Mussa Chully, Mwenyekiti wa Kijiji cha Shambarai.

No comments:
Post a Comment